Ezra 6:1-22

  • Uchunguzi na agizo la Dario (1-12)

  • Ujenzi wakamilika na hekalu lazinduliwa (13-18)

  • Pasaka yaadhimishwa (19-22)

6  Ndipo Mfalme Dario akatoa agizo, nao wakafanya uchunguzi katika jengo la hifadhi* ambamo hazina ziliwekwa huko Babiloni.  Kisha kitabu cha kukunjwa kikapatikana kwenye ngome huko Ekibatana, katika mkoa* wa Umedi, nacho kilikuwa na ujumbe ufuatao:  “Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Koreshi, Mfalme Koreshi alitoa agizo hili kuhusu nyumba ya Mungu huko Yerusalemu:+ ‘Nyumba hiyo na ijengwe upya iwe mahali watakapotolea dhabihu, na misingi yake inapaswa kuwekwa; kimo chake kiwe mikono 60,* upana wake mikono 60,+  na iwe na safu tatu za mawe makubwa yaliyobingirishwa na kuwekwa mahali pake na safu moja ya mbao;+ na gharama zote zilipwe kutoka katika nyumba ya mfalme.+  Pia, vyombo vya dhahabu na fedha vya nyumba ya Mungu ambavyo Nebukadneza alivichukua katika hekalu lililokuwa Yerusalemu na kuvileta Babiloni+ virudishwe, ili viwekwe mahali pake katika hekalu huko Yerusalemu na vihifadhiwe katika nyumba ya Mungu.’+  “Basi, Tatenai gavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto,* Shethar-bozenai, na wenzenu, magavana wadogo wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto+—msikaribie mahali hapo.  Msiingilie kazi ya nyumba hiyo ya Mungu. Gavana wa Wayahudi na wazee wa Wayahudi watajenga upya nyumba hiyo ya Mungu mahali ilipokuwa zamani.  Pia, ninatoa agizo kuhusu jambo mnalopaswa kuwafanyia wazee hao wa Wayahudi kwa ajili ya kujenga upya nyumba hiyo ya Mungu: Gharama zao zote zitalipwa bila kuchelewa kutoka katika hazina ya mfalme,+ kodi inayokusanywa katika eneo lililo Ng’ambo ya Mto, ili ujenzi uendelee bila kukatizwa.+  Na chochote kinachohitajiwa—ng’ombe dume wachanga+ pamoja na kondoo dume+ na wanakondoo+ kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa kwa Mungu wa mbinguni, ngano,+ chumvi,+ divai,+ na mafuta,+ kama watakavyosema makuhani walio Yerusalemu—waendelee kupewa vitu hivyo siku baada ya siku bila kukosa, 10  ili waendelee kutoa matoleo yanayompendeza Mungu wa mbinguni na kumwombea mfalme na wanawe wawe na maisha marefu.+ 11  Pia nimetoa agizo kwamba yeyote atakayevunja amri hii, nguzo itang’olewa katika nyumba yake naye atatundikwa juu ya nguzo hiyo, na nyumba yake itafanywa kuwa choo cha umma* kwa sababu ya kosa hilo. 12  Na Mungu aliyefanya jina lake likae huko+ na ampindue mfalme yeyote na watu watakaonyoosha mkono ili kukiuka agizo hili na kuiharibu nyumba ya Mungu, iliyo Yerusalemu. Mimi, Dario, ninatoa agizo hili. Nalo litekelezwe bila kukawia.” 13  Ndipo Tatenai gavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto, Shethar-bozenai,+ na wenzao, wakatekeleza bila kukawia kila jambo ambalo Mfalme Dario alikuwa ameagiza. 14  Nao wazee wa Wayahudi wakaendelea kujenga na kufanya maendeleo,+ wakitiwa moyo na nabii Hagai+ na Zekaria+ mjukuu wa Ido; wakamaliza kujenga kulingana na agizo la Mungu wa Israeli+ na agizo la Koreshi,+ Dario,+ na Mfalme Artashasta+ wa Uajemi. 15  Wakamaliza kujenga nyumba hiyo katika siku ya tatu ya mwezi wa Adari,* katika mwaka wa sita wa utawala wa Mfalme Dario. 16  Ndipo Waisraeli, makuhani, Walawi,+ na watu wengine waliotoka uhamishoni wakaizindua* nyumba ya Mungu kwa shangwe. 17  Nao wakaleta kwa ajili ya kuzindua nyumba ya Mungu ng’ombe dume 100, kondoo dume 200, wanakondoo 400, na mbuzi dume 12 kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya Waisraeli wote, kulingana na idadi ya makabila ya Israeli.+ 18  Nao wakawapanga makuhani katika makundi yao na Walawi katika vikundi vyao kwa ajili ya utumishi wa Mungu huko Yerusalemu,+ kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Musa.+ 19  Na watu hao waliotoka uhamishoni wakasherehekea Pasaka siku ya 14 ya mwezi wa kwanza.+ 20  Makuhani na Walawi wote, walikuwa wamejitakasa,+ hivyo wote walikuwa safi; basi wakachinja mnyama wa Pasaka kwa ajili ya watu wote waliotoka uhamishoni, kwa ajili ya makuhani wenzao, na kwa ajili yao wenyewe. 21  Kisha Waisraeli waliorudi kutoka uhamishoni wakala pamoja na kila mtu aliyekuwa amejiunga nao na kujitenga na uchafu wa mataifa ya nchi hiyo ili kumwabudu* Yehova Mungu wa Israeli.+ 22  Pia, wakasherehekea kwa shangwe Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu+ kwa siku saba, kwa maana Yehova aliwafanya washangilie na alikuwa ameugeuza moyo wa mfalme wa Ashuru ili awatendee mema,+ hivi kwamba akawaunga mkono* katika kazi ya nyumba ya Mungu wa kweli, Mungu wa Israeli.

Maelezo ya Chini

Tnn., “nyumba ya kumbukumbu.”
Au “wilaya ya utawala.”
Karibu mita 26.7 (futi 87.6). Angalia Nyongeza B14.
Au “maeneo yaliyo magharibi ya Mto Efrati.”
Au labda, “eneo la takataka; rundo la mavi.”
Au “wakaiweka wakfu.”
Tnn., “kumtafuta.”
Tnn., “akaitia nguvu mikono yao.”