Ezra 7:1-28

  • Ezra aja Yerusalemu (1-10)

  • Barua ya Artashasta kwa Ezra (11-26)

  • Ezra amsifu Yehova (27, 28)

7  Baada ya mambo hayo, wakati wa utawala wa Mfalme Artashasta+ wa Uajemi, Ezra*+ akarudi. Alikuwa mwana wa Seraya,+ mwana wa Azaria, mwana wa Hilkia,+  mwana wa Shalumu, mwana wa Sadoki, mwana wa Ahitubu,  mwana wa Amaria, mwana wa Azaria,+ mwana wa Merayothi,  mwana wa Zeraya, mwana wa Uzi, mwana wa Buki,  mwana wa Abishua, mwana wa Finehasi,+ mwana wa Eleazari,+ mwana wa kuhani mkuu Haruni.+  Huyo Ezra alitoka Babiloni. Alikuwa mwandishi* na aliijua vizuri* Sheria ya Musa,+ iliyotolewa na Yehova Mungu wa Israeli. Mfalme alimpa kila kitu alichoomba, kwa maana mkono wa Yehova Mungu wake ulikuwa juu yake.  Baadhi ya Waisraeli, makuhani, Walawi,+ waimbaji,+ walinzi wa malango,+ na watumishi wa hekaluni,*+ wakapanda kwenda Yerusalemu katika mwaka wa saba wa utawala wa Mfalme Artashasta.  Naye Ezra akaja Yerusalemu mwezi wa tano, katika mwaka wa saba wa utawala wa mfalme huyo.  Alianza safari ya kutoka Babiloni siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, akafika Yerusalemu siku ya kwanza ya mwezi wa tano, kwa sababu mkono mwema wa Mungu wake ulikuwa juu yake.+ 10  Ezra alikuwa ameutayarisha moyo wake* kuichunguza Sheria ya Yehova na kuifuata,+ na kufundisha masharti ya sheria hiyo na maamuzi yake katika Israeli.+ 11  Ifuatayo ni nakala ya barua ambayo Mfalme Artashasta alimpa Ezra aliyekuwa kuhani na mwandishi,* mwenye ujuzi mwingi* kuhusu amri za Yehova na masharti aliyowapa Waisraeli: 12  * “Artashasta,+ mfalme wa wafalme, kwa kuhani Ezra, mwandishi* wa Sheria ya Mungu wa mbinguni: Na uwe na amani kamili. Na sasa 13  nimetoa agizo kwamba kila mtu katika milki yangu ambaye ni mmoja wa watu wa Israeli na pia makuhani wao na Walawi, ambaye angependa kwenda nawe Yerusalemu aende.+ 14  Kwa maana umetumwa na mfalme na washauri wake saba ili kuchunguza kama watu walio Yuda na Yerusalemu wanafuata Sheria ya Mungu wako uliyo nayo,* 15  na kuchukua fedha na dhahabu ambayo mfalme na washauri wake wamemtolea kwa hiari Mungu wa Israeli, ambaye makao yake yako Yerusalemu, 16  pamoja na fedha na dhahabu yote ambayo utapokea* katika mkoa wote* wa Babiloni, na pia zawadi ambazo watu na makuhani hutoa kwa hiari kwa ajili ya nyumba ya Mungu wao iliyo Yerusalemu.+ 17  Na bila kukawia utanunua kwa pesa hizo ng’ombe dume,+ kondoo dume,+ wanakondoo,+ na matoleo yao ya nafaka+ na matoleo yao ya kinywaji,+ nawe utavitoa juu ya madhabahu ya nyumba ya Mungu wenu huko Yerusalemu. 18  “Na fedha na dhahabu itakayobaki, wewe na ndugu zako mnaweza kuitumia mtakavyopenda, kulingana na mapenzi ya Mungu wenu. 19  Na vyombo vyote utakavyopewa kwa ajili ya utumishi wa nyumba ya Mungu wako, unapaswa kuvipeleka mbele za Mungu huko Yerusalemu.+ 20  Na kitu kingine chochote unachohitaji kutoa kwa ajili ya nyumba ya Mungu wako, utakitoa kutoka katika hazina ya mfalme.+ 21  “Mimi, Mfalme Artashasta, nimewaagiza waweka-hazina wote katika eneo lililo Ng’ambo ya Mto* wampe bila kukawia kila kitu atakachoomba Ezra,+ kuhani na mwandishi wa* Sheria ya Mungu wa mbinguni, 22  hata akiomba talanta 100 za fedha,* kori 100 za ngano,* bathi 100 za divai,*+ bathi 100 za mafuta,+ na chumvi isiyo na kipimo.+ 23  Kila jambo ambalo Mungu wa mbinguni ameagiza linapaswa kufanywa kwa bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu wa mbinguni,+ ili ghadhabu yake isije dhidi ya milki yangu na wanangu.+ 24  Pia ninawajulisha kwamba hairuhusiwi kuwatoza kodi, wala ushuru,+ wala ada yoyote makuhani na Walawi, wanamuziki,+ walinzi wa malango, watumishi wa hekaluni,*+ na wafanyakazi wa nyumba hii ya Mungu. 25  “Na wewe, Ezra, kulingana na hekima uliyopewa na Mungu wako,* teua mahakimu na waamuzi ili wawahukumu watu wote katika eneo lililo Ng’ambo ya Mto, wote wanaojua sheria za Mungu wako; nanyi mnapaswa kumfundisha yeyote asiyezijua.+ 26  Na kila mtu ambaye hatafuata Sheria ya Mungu wako na sheria ya mfalme anapaswa kuhukumiwa upesi, iwe ni kuuawa, kufukuzwa nchini, kutozwa faini, au kufungwa gerezani.” 27  Yehova Mungu wa mababu zetu na asifiwe, ambaye alitia ndani ya moyo wa mfalme wazo la kuipamba nyumba ya Yehova iliyo Yerusalemu!+ 28  Naye amenitendea kwa upendo mshikamanifu mbele ya mfalme,+ washauri wake,+ na wakuu wote wa mfalme wenye nguvu. Hivyo nikajipa ujasiri* kwa sababu mkono wa Yehova Mungu ulikuwa juu yangu, nami nikawakusanya wanaume waliokuwa viongozi* katika Israeli ili wapande pamoja nami.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Msaada.”
Au “Alinakili maandishi.”
Au “Alikuwa mwandishi stadi wa.”
Au “Wanethini.” Tnn., “waliotolewa.”
Au “alikuwa ameazimia moyoni mwake.”
Au “mtu aliyenakili maandishi.”
Au “aliyenakili maneno.”
Mwanzoni, maandishi ya Ezr 7:12 hadi 7:26 yaliandikwa katika Kiaramu.
Au “aliyenakili maandishi.”
Tnn., “iliyo mkononi mwako.”
Au, “wilaya yote ya utawala.”
Tnn., “utapata.”
Au “maeneo yaliyo magharibi ya Mto Efrati.”
Au “aliyenakili maandishi ya.”
Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.
Bathi ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Talanta ilikuwa sawa na kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “Wanethini.” Tnn., “waliotolewa.”
Tnn., “kulingana na hekima ya Mungu wako iliyo mkononi mwako.”
Au “nikajipa nguvu.”
Tnn., “vichwa.”