Ezra 9:1-15

  • Waisraeli waoa wanawake wa kigeni (1-4)

  • Sala ya Ezra ya kuungama (5-15)

9  Baada ya mambo hayo kufanywa, wakuu wakaja na kuniambia: “Watu wa Israeli na makuhani na Walawi hawajajitenga na watu wa mataifa ya nchi mbalimbali na mazoea yao yanayochukiza,+ ya Wakanaani, Wahiti, Waperizi, Wayebusi, Waamoni, Wamoabu, Wamisri,+ na Waamori.+  Wamejichukulia baadhi ya mabinti wa mataifa hayo kuwa wake zao na kuwachukulia wana wao pia.+ Sasa wao, uzao mtakatifu,*+ wamechanganyika na watu wa mataifa ya nchi mbalimbali.+ Wakuu na watawala wasaidizi ndio wanaoongoza katika ukosefu huu wa uaminifu.”  Mara tu niliposikia jambo hilo, nikalirarua vazi langu na joho langu lisilo na mikono na kung’oa baadhi ya nywele za kichwa changu na ndevu zangu, nami nikaketi chini kwa mshtuko.  Kisha kila mtu aliyehofu* maneno ya Mungu wa Israeli akakusanyika kunizunguka kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu wa watu waliotoka uhamishoni, nami nilikuwa nimeketi chini kwa mshtuko mpaka wakati wa toleo la nafaka la jioni.+  Wakati wa toleo la nafaka la jioni,+ niliinuka kutoka mahali nilipokuwa nimeketi kwa aibu, vazi langu na joho langu lisilo na mikono likiwa limeraruka, nikapiga magoti na kumnyooshea mikono Yehova Mungu wangu.  Nikasema: “Ee Mungu wangu, ninaona aibu na haya kuuinua uso wangu kwako, Ee Mungu wangu, kwa sababu makosa yetu yameongezeka juu ya vichwa vyetu na hatia yetu imerundamana mpaka mbinguni.+  Tangu siku za mababu zetu mpaka leo hii tumekuwa na hatia kubwa;+ na kwa sababu ya makosa yetu, sisi, wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa mikononi mwa wafalme wa nchi nyingine, tumeuawa kwa upanga,+ tumepelekwa utekwani,+ tumeporwa,+ tumetiwa aibu, kama ilivyo leo.+  Lakini sasa kwa muda mfupi, Yehova Mungu wetu ametuonyesha kibali kwa kuruhusu baadhi yetu tuponyoke na kutupatia sehemu salama* mahali pake patakatifu,+ ili kuyafanya macho yetu yang’ae, Ee Mungu wetu, na kutupumzisha kidogo kutoka katika utumwa wetu.  Ingawa sisi ni watumwa,+ Mungu wetu hajatuacha utumwani; bali ametutendea kwa upendo mshikamanifu mbele ya wafalme wa Uajemi,+ ili kutupumzisha tuweze kuisimamisha nyumba ya Mungu wetu+ na kuijenga upya nyumba hiyo ambayo ni magofu na kutupatia ukuta wa mawe* katika Yuda na Yerusalemu. 10  “Lakini tuseme nini sasa, Ee Mungu wetu, baada ya hayo? Kwa maana tumeziacha amri zako, 11  ulizotupatia kupitia watumishi wako manabii, ukisema: ‘Nchi ambayo mnaingia kuimiliki ni nchi chafu kwa kuwa watu waliomo ni wachafu, kwa sababu ya matendo yao yanayochukiza ambayo wameyajaza kutoka mwisho mmoja hadi mwingine kwa uchafu wao.+ 12  Kwa hiyo, msiwaruhusu mabinti zenu waolewe na wana wao, wala msikubali wana wenu wawaoe mabinti zao;+ msiwatakie kamwe amani wala mafanikio,+ ili mzidi kupata nguvu na kula mema ya nchi na kuimiliki ili wana wenu wairithi milele.’ 13  Baada ya yote yaliyotupata kwa sababu ya matendo yetu maovu na hatia yetu kubwa—kwa maana wewe, Ee Mungu wetu, hujatutendea kulingana na makosa yetu,+ nawe umeruhusu sisi tulio hapa tuponyoke+ 14  je, tuvunje tena amri zako na kufanya mapatano ya ndoa* na watu wanaotenda mambo haya yanayochukiza?+ Je, hutatukasirikia vikali na kutuangamiza kabisa, hata kusiwe na yeyote atakayebaki wala kuokoka? 15  Ee Yehova Mungu wa Israeli, wewe ni mwadilifu,+ kwa maana tumeokoka na kubaki mpaka leo. Sasa tumesimama mbele zako tukiwa na hatia, kwa maana hatuwezi kusimama mbele zako kwa sababu ya jambo hili.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu takatifu.”
Tnn., “aliyetetemeka kwa sababu ya.”
Tnn., “kigingi.”
Au “ukuta wa ulinzi.”
Au “na kuoana.”