Hagai 1:1-15

  • Wakemewa kwa kutojenga hekalu (1-11)

    • ‘Je, ni wakati wa kukaa katika nyumba zilizopambwa kwa mbao?’ (4)

    • “Kazieni mioyo yenu juu ya njia zenu” (5)

    • Kupanda kwa wingi kuvuna kidogo (6)

  • Watu wasikiliza sauti ya Yehova (12-15)

1  Katika mwaka wa pili wa utawala wa Mfalme Dario, katika mwezi wa sita, siku ya kwanza ya mwezi huo, neno la Yehova lilikuja kupitia nabii Hagai*+ kwa Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli, gavana wa Yuda, na kwa Yoshua mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, likisema:  “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Watu hawa wanasema, “Wakati wa kujenga nyumba ya* Yehova bado haujafika.”’”+  Na neno la Yehova likaja tena kupitia nabii Hagai,+ likisema:  “Je, ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zilizopambwa kwa mbao, huku nyumba hii ikiwa magofu?+  Sasa hivi ndivyo anavyosema Yehova wa majeshi, ‘Kazieni mioyo yenu juu ya* njia zenu.  Mmepanda mbegu nyingi, lakini mnavuna kidogo.+ Mnakula, lakini hamshibi. Mnakunywa, lakini hamtosheki. Mnavaa nguo, lakini hakuna yeyote anayepata joto. Kibarua huweka mshahara wake katika mfuko uliojaa mashimo.’”  “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Kazieni mioyo yenu juu ya* njia zenu.’  “‘Pandeni juu mlimani mkalete miti.+ Jengeni nyumba hii,+ ili niifurahie na ili nitukuzwe,’+ asema Yehova.”  “‘Mlitazamia mavuno mengi lakini mlipata kidogo; na mlipoyaleta katika nyumba hii, niliyapeperusha mbali.+ Kwa nini?’ auliza Yehova wa majeshi. ‘Kwa sababu nyumba yangu ni magofu, huku kila mmoja wenu akikimbia huku na huku ili kuitunza nyumba yake mwenyewe.+ 10  Kwa hiyo mbingu zilizo juu yenu zikazuia umande wake, na dunia ikazuia mazao yake. 11  Nami niliendelea kuuita ukame uje duniani, milimani, kwenye nafaka, kwenye divai mpya, kwenye mafuta, kwenye mimea inayoota ardhini, juu ya wanadamu na mifugo, na juu ya kazi yote ya mikono yenu.’” 12  Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli+ na Yoshua mwana wa Yehosadaki,+ kuhani mkuu, na watu wengine wote wakaisikiliza sauti ya Yehova Mungu wao na maneno ya nabii Hagai, kwa sababu Yehova Mungu wao alikuwa amemtuma; na watu wakaanza kuogopa kwa sababu ya Yehova. 13  Kisha Hagai, mjumbe wa Yehova, akawapa watu ujumbe huu kulingana na utume wake kutoka kwa Yehova: “‘Niko pamoja nanyi,’+ asema Yehova.” 14  Basi Yehova akaichochea roho+ ya Zerubabeli mwana wa Shealtieli, gavana wa Yuda,+ na roho ya Yoshua+ mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, na roho ya watu wengine wote; nao wakaja na kuanza kujenga nyumba ya Yehova wa majeshi, Mungu wao.+ 15  Ilikuwa siku ya 24 ya mwezi wa sita, katika mwaka wa pili wa Mfalme Dario.+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Aliyezaliwa Wakati wa Sherehe.”
Au “kujenga upya hekalu la.”
Au “Fikirieni kwa makini.”
Au “Fikirieni kwa makini.”