Hesabu 11:1-35

  • Mungu aleta moto kwa sababu ya malalamiko (1-3)

  • Watu walilia nyama (4-9)

  • Musa ahisi hastahili (10-15)

  • Yehova awapa roho wazee 70 (16-25)

  • Eldadi na Medadi; Yoshua aona wivu kwa ajili ya Musa (26-30)

  • Kware waletwa; watu waadhibiwa kwa sababu ya pupa (31-35)

11  Sasa watu wakaanza kulalamika kwa uchungu mbele za Yehova. Yehova aliposikia malalamiko yao, alikasirika sana, na moto kutoka kwa Yehova ukaanza kuwateketeza na kuwaangamiza baadhi ya watu waliokuwa kandokando ya kambi.  Watu walipoanza kumlilia Musa, alimwomba Yehova dua,+ nao moto ukazimika.  Kwa hiyo mahali hapo pakaitwa Tabera,* kwa sababu moto kutoka kwa Yehova uliwateketeza watu.+  Kisha umati wa watu waliochangamana nao*+ ukaanza kutamani chakula kwa pupa,+ basi Waisraeli wakaanza kulia tena na kusema: “Ni nani atakayetupatia nyama tule?+  Tunakumbuka sana samaki wa bure tuliokuwa tukila nchini Misri, pamoja na matango, matikiti, vitunguu vya majani, vitunguu maji, na vitunguu saumu!+  Lakini sasa tunadhoofika. Hatuoni kitu kingine chochote isipokuwa hii mana.”+  Kwa kweli, mana+ ilikuwa kama mbegu za giligilani,+ na ilionekana kama utomvu wa mbedola.  Watu walikuwa wakienda kila mahali kuiokota, kisha waliisaga kwa mawe ya kusagia au waliitwanga kwenye kinu. Halafu waliichemsha katika vyungu vya kupikia au waliitumia kuoka mikate ya mviringo,+ na ladha yake ilikuwa kama ladha ya keki tamu iliyookwa kwa mafuta.  Umande ulipoanguka kambini usiku, mana pia ilianguka pamoja na umande huo.+ 10  Musa akawasikia watu wakilia katika kila familia, kila mtu kwenye mlango wa hema lake. Basi Yehova akakasirika sana,+ na Musa pia akachukizwa sana na jambo hilo. 11  Kisha Musa akamwambia Yehova: “Kwa nini unanitesa mimi mtumishi wako? Kwa nini hupendezwi nami, hivi kwamba umenitwika mzigo wa watu wote hawa?+ 12  Je, ni mimi niliyebeba mimba ya watu hawa wote? Je, ni mimi niliyewazaa ndiyo sababu unaniambia, ‘Wabebe kifuani pako, kama mlezi* anavyombeba mtoto mchanga,’ na kuwapeleka katika nchi uliyoapa kwamba utawapa mababu zao?+ 13  Nitapata wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwa sababu wanaendelea kunililia wakisema, ‘Tupe nyama tule!’ 14  Siwezi kuwabeba watu hawa wote peke yangu; ni mzigo mzito sana kwangu.+ 15  Ikiwa utaendelea kunitendea hivi, tafadhali niue sasa hivi.+ Ikiwa nimepata kibali machoni pako, usiache niendelee kutaabika.” 16  Yehova akamjibu Musa: “Nikusanyie wanaume 70 miongoni mwa wazee wa Israeli, wanaume ambao unajua kwamba ni wazee na maofisa wa watu,+ nawe uwapeleke kwenye hema la mkutano, na kuwaagiza wasimame hapo pamoja nawe. 17  Nitashuka+ na kuzungumza nawe hapo,+ nami nitachukua kiasi fulani cha roho+ iliyo juu yako na kuiweka juu yao, nao watakusaidia kubeba mzigo wa watu hawa ili usiubebe peke yako.+ 18  Unapaswa kuwaambia watu, ‘Jitakaseni kwa ajili ya kesho,+ kwa maana hakika mtakula nyama, kwa sababu Yehova amewasikia mkilia+ na kusema: “Ni nani atakayetupatia nyama tule? Hali yetu ilikuwa nzuri zaidi nchini Misri.”+ Hakika Yehova atawapa nyama, nanyi mtaila.+ 19  Hamtaila kwa siku moja tu, au siku 2, au siku 5, au siku 10, au hata siku 20, 20  bali kwa mwezi mzima, mpaka itakapotokea kwenye mianzi ya pua zenu na kuwachukiza,+ kwa sababu mlimkataa Yehova aliye kati yenu, nanyi mlilia mbele zake mkisema: “Kwa nini tumetoka Misri?”’”+ 21  Kisha Musa akasema: “Niko miongoni mwa wanaume 600,000+ wanaotembea kwa miguu, nawe unasema, ‘Nitawapa nyama, nao watakula nyama ya kutosha kwa mwezi mzima’! 22  Je, makundi mazima ya kondoo na ng’ombe yakichinjwa, yatawatosha? Au samaki wote wa baharini wakivuliwa, je, watawatosha?” 23  Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Je, mkono wa Yehova ni mfupi?+ Sasa utaona ikiwa jambo ninalosema litatimia kwako au la.” 24  Basi Musa akatoka na kuwaambia watu maneno ya Yehova. Akawakusanya wanaume 70 miongoni mwa wazee wa watu na kuwaagiza wasimame kuzunguka hema la mkutano.+ 25  Kisha Yehova akashuka katika wingu+ na kuzungumza naye,+ akachukua kiasi fulani cha roho+ iliyokuwa juu yake na kuiweka juu ya kila mmoja wa wale wazee 70. Na mara tu roho hiyo iliposhuka juu yao, wakaanza kutenda kama manabii,*+ lakini hawakufanya hivyo tena. 26  Wawili kati ya wanaume hao walibaki kambini. Mmoja aliitwa Eldadi na mwingine Medadi. Na roho ikaanza kushuka juu yao, kwa maana walikuwa kati ya wale ambao majina yao yalikuwa yameandikwa lakini hawakwenda kwenye hema la mkutano. Basi wakaanza kutenda kama manabii kambini. 27  Mwanamume mmoja kijana akakimbia na kumwambia Musa: “Eldadi na Medadi wanatenda kama manabii kambini!” 28  Ndipo Yoshua+ mwana wa Nuni, aliyekuwa mtumishi wa Musa tangu ujanani, akasema: “Bwana wangu Musa, wakataze!”+ 29  Lakini Musa akamwambia: “Je, unaona wivu kwa ajili yangu? Usifanye hivyo, laiti watu wote wa Yehova wangekuwa manabii na laiti Yehova angeweka roho yake juu yao!” 30  Baadaye Musa akarudi kambini pamoja na wazee wa Israeli. 31  Kisha upepo kutoka kwa Yehova ukavuma ghafla na kuanza kuleta kware kutoka baharini na kuwaangusha kotekote kambini,+ kwenye eneo la umbali wa siku moja hivi kila upande kuzunguka kambi, wakafikia kimo cha mikono miwili* hivi kutoka ardhini. 32  Basi siku hiyo yote, mchana na usiku wote, na siku nzima iliyofuata waliendelea kuokota kware. Hakuna aliyeokota chini ya homeri kumi,* nao waliwaanika kila mahali kambini. 33  Lakini nyama ilipokuwa ingali katikati ya meno yao, kabla hawajaitafuna, hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya watu, na Yehova akaanza kuwapiga watu kwa maangamizi makubwa sana.+ 34  Kwa hiyo wakapaita mahali hapo Kibroth-hataava,*+ kwa sababu hapo ndipo walipowazika watu waliokuwa na tamaa na pupa.+ 35  Kutoka Kibroth-hataava watu wakasafiri mpaka Haserothi+ na kukaa huko.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Kuteketea,” yaani, moto mkali.
Inaonekana ni watu ambao hawakuwa Waisraeli.
Au “mlezi wa kiume.”
Au “wakaanza kutabiri.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Homeri ni kipimo sawa na lita 220. Angalia Nyongeza B14.
Maana yake “Makaburi ya Watu Wenye Tamaa.”