Hesabu 12:1-16

  • Miriamu na Haruni wampinga Musa (1-3)

    • Musa mtu mpole zaidi kuliko watu wote (3)

  • Yehova amtetea Musa (4-8)

  • Miriamu apigwa na ukoma (9-16)

12  Miriamu na Haruni wakaanza kusema vibaya kumhusu Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa, kwa maana Musa alikuwa ameoa mwanamke Mkushi.+  Walikuwa wakisema: “Je, Yehova amezungumza kupitia Musa peke yake? Je, hajazungumza kupitia sisi pia?”+ Na Yehova alikuwa akisikiliza.+  Basi Musa alikuwa mtu mpole zaidi kuliko watu wote*+ duniani.  Kwa ghafla Yehova akamwambia Musa, Haruni, na Miriamu: “Ninyi watatu, nendeni kwenye hema la mkutano.” Basi wote watatu wakaenda.  Yehova akashuka katika nguzo ya wingu+ na kusimama kwenye mlango wa hema la mkutano, akamwita Haruni na Miriamu. Wote wawili wakaenda mbele.  Ndipo akawaambia: “Tafadhali, sikilizeni maneno yangu. Ikiwa nabii wangu, mimi Yehova, angekuwa miongoni mwenu, ningejitambulisha kwake katika maono,+ nami ningeongea naye katika ndoto.+  Lakini sijafanya hivyo kuhusiana na mtumishi wangu Musa! Nimemkabidhi nyumba yangu yote.*+  Mimi huongea naye uso kwa uso,*+ waziwazi, wala si kwa mafumbo; naye huona uwepo wangu, mimi Yehova. Kwa nini, basi, hamkuogopa kusema vibaya kumhusu Musa, mtumishi wangu?”  Kwa hiyo hasira ya Yehova ikawaka dhidi yao, naye akaenda zake. 10  Lile wingu likaondoka juu ya hema, na tazama! Miriamu alikuwa amepigwa kwa ukoma mweupe kama theluji.+ Kisha Haruni akageuka na kumtazama Miriamu, akaona kwamba alikuwa amepigwa kwa ukoma.+ 11  Mara moja Haruni akamwambia Musa: “Nakusihi, bwana wangu! Tafadhali, usituadhibu kwa sababu ya dhambi hii! Tumetenda kwa upumbavu. 12  Tafadhali, usimwache aendelee kuwa kama mtu aliyezaliwa akiwa amekufa, ambaye nusu ya mwili wake imeoza!” 13  Basi Musa akaanza kumlilia Yehova, akisema: “Ee Mungu, tafadhali mponye! Tafadhali!”+ 14  Yehova akamjibu Musa: “Ikiwa baba yake angemtemea mate usoni moja kwa moja, je, hangeaibika kwa siku saba? Acha atengwe nje ya kambi kwa siku saba,+ kisha anaweza kurudishwa kambini.” 15  Kwa hiyo Miriamu akatengwa nje ya kambi kwa siku saba,+ na watu hawakuendelea na safari hadi Miriamu aliporudishwa kambini. 16  Kisha watu wakaondoka Haserothi+ na kuanza kupiga kambi katika nyika ya Parani.+

Maelezo ya Chini

Au “mnyenyekevu zaidi, kuliko mtu mwingine yeyote.”
Tnn., “Anajithibitisha mwenyewe kuwa mwaminifu katika nyumba yangu yote.”
Tnn., “kinywa kwa kinywa.”