Hesabu 15:1-41

  • Sheria kuhusu dhabihu (1-21)

    • Sheria zilezile kwa wenyeji na wageni (15, 16)

  • Dhabihu kwa ajili ya dhambi zilizofanywa bila kukusudia (22-29)

  • Adhabu kwa ajili ya dhambi zilizofanywa kimakusudi (30, 31)

  • Aliyevunja Sabato auawa (32-36)

  • Mavazi yawe na upindo wa nyuzinyuzi (37-41)

15  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Hatimaye mtakapoingia katika nchi ninayowapa mwishi ndani yake,+  na kumtolea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto kutoka kati ya mifugo au kundi—iwe ni dhabihu ya kuteketezwa+ au dhabihu ya kutimiza nadhiri ya pekee au toleo la hiari+ au dhabihu mnayotoa wakati wa sherehe zenu za majira,+ ili kumtolea Yehova harufu inayompendeza*+  ni lazima pia mtu anayetoa dhabihu yake amtolee Yehova sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini+ uliochanganywa na robo ya hini* ya mafuta ili iwe toleo la nafaka.  Pia mnapaswa kutoa robo ya kipimo cha hini ya divai ili iwe toleo la kinywaji; mtaitoa pamoja na dhabihu ya kuteketezwa+ au pamoja na dhabihu ya kila mwanakondoo dume.  Au mtatoa kondoo dume pamoja na sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa moja ya unga laini uliochanganywa na sehemu ya tatu ya hini ya mafuta kwa ajili ya toleo la nafaka.  Nanyi mnapaswa kutoa sehemu ya tatu ya hini ya divai ili iwe toleo la kinywaji lenye harufu inayompendeza* Yehova.  “‘Lakini mkimtolea Yehova mnyama dume kutoka katika mifugo yenu ili awe dhabihu ya kuteketezwa+ au dhabihu ya kutimiza nadhiri ya pekee+ au dhabihu za ushirika,+  mnapaswa kumtoa mnyama dume huyo pamoja na sehemu tatu za kumi za kipimo cha efa moja ya unga laini uliochanganywa na nusu ya hini ya mafuta kwa ajili ya toleo la nafaka.+ 10  Mnapaswa pia kutoa nusu ya hini ya divai ili iwe toleo la kinywaji+ linalochomwa kwa moto lenye harufu inayompendeza* Yehova. 11  Hivyo ndivyo mnavyopaswa kumtoa kila ng’ombe dume au kila kondoo dume au kila mwanakondoo dume au mbuzi dume. 12  Haidhuru mnatoa wanyama wangapi, mnapaswa kutoa vitu hivyo pamoja na kila mnyama mnayemtoa, kulingana na idadi yao. 13  Hivyo ndivyo kila Mwisraeli mwenyeji anavyopaswa kutoa dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova. 14  “‘Ikiwa mgeni anayeishi nanyi au mtu mwingine ambaye ameishi pamoja nanyi kwa muda mrefu atatoa pia dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayompendeza* Yehova, anapaswa kufanya kama mnavyofanya.+ 15  Ninyi pamoja na mgeni anayeishi miongoni mwenu mtafuata sheria zilezile. Itakuwa amri ya kudumu katika vizazi vyenu vyote. Ninyi pamoja na mgeni mtakuwa sawa mbele za Yehova.+ 16  Ninyi na mgeni anayeishi miongoni mwenu mtafuata sheria zilezile na amri zilezile.’”* 17  Yehova akaendelea kumwambia Musa, 18  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mtakapoingia katika nchi ninayowapeleka 19  nanyi mle chakula chochote cha* nchi hiyo,+ mnapaswa kumtolea Yehova kiasi fulani kama mchango. 20  Mtatoa mchango wa mazao ya kwanza+ ya mikate ya mviringo iliyookwa kwa unga wenu ambao haujakobolewa. Mtautoa kama mchango unaotoka katika uwanja wa kupuria nafaka. 21  Baadhi ya mazao ya kwanza ya unga wenu ambao haujakobolewa mtamtolea Yehova mchango katika vizazi vyenu vyote. 22  “‘Sasa mkifanya kosa, nanyi mkose kushika amri hizi zote ambazo mimi, Yehova, nimempa Musa, 23  mambo yote ambayo mimi, Yehova, nimewaamuru ninyi kupitia Musa katika vizazi vyenu tangu siku ambayo mimi Yehova niliamuru, 24  na ikiwa kosa hilo lilifanywa bila kukusudia na bila kusanyiko lote kujua, basi ni lazima kusanyiko lote litoe dhabihu ya kuteketezwa ya ng’ombe dume mchanga ili iwe harufu inayompendeza* Yehova, pamoja na toleo lake la nafaka na toleo lake la kinywaji kulingana na utaratibu wa kawaida,+ na pia mwanambuzi mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi.+ 25  Kuhani atatoa dhabihu ya kufunika dhambi ya kusanyiko lote la Waisraeli, nao watasamehewa,+ kwa sababu lilikuwa kosa, nao walimletea Yehova dhabihu inayochomwa kwa moto na kuleta dhabihu yao ya dhambi mbele za Yehova kwa ajili ya kosa lao. 26  Kusanyiko lote la Waisraeli pamoja na wageni wanaokaa miongoni mwao watasamehewa kosa hilo kwa sababu watu wote walihusika. 27  “‘Mtu yeyote akifanya dhambi bila kukusudia, atatoa mbuzi jike wa mwaka mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi.+ 28  Kisha kuhani atatoa dhabihu ili mtu aliyetenda dhambi mbele za Yehova bila kukusudia asamehewe dhambi yake, yaani, atamtolea dhabihu ya kufunika dhambi yake, na mtu huyo atasamehewa.+ 29  Waisraeli wenyeji na pia wageni wanaoishi miongoni mwao watafuata sheria zilezile zinazomhusu mtu anayetenda kosa bila kukusudia.+ 30  “‘Lakini mtu anayetenda kosa kimakusudi,+ awe ni mwenyeji au mgeni, anamkufuru Yehova, naye lazima auawe. 31  Kwa kuwa amedharau neno la Yehova na kuvunja amri yake, ni lazima mtu huyo auawe.+ Ataadhibiwa kwa sababu ya kosa lake.’”*+ 32  Waisraeli walipokuwa nyikani, walimkuta mtu fulani akiokota kuni siku ya Sabato.+ 33  Wale waliomkuta akikusanya kuni wakamleta kwa Musa na Haruni na Waisraeli wote. 34  Wakamtia kifungoni+ kwa sababu sheria haikusema waziwazi mtu huyo afanyiwe nini. 35  Basi Yehova akamwambia Musa: “Ni lazima mtu huyo auawe,+ Waisraeli wote watampiga mawe nje ya kambi.”+ 36  Basi Waisraeli wote wakamtoa nje ya kambi, wakampiga mawe na kumuua, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 37  Yehova akaendelea kumwambia Musa: 38  “Waambie Waisraeli wajitengenezee upindo wa nyuzinyuzi kwenye ncha za mavazi yao katika vizazi vyao vyote, nao watashona uzi wa bluu juu ya upindo huo wa nyuzinyuzi.+ 39  ‘Mnapaswa kutengeneza upindo huo wa nyuzinyuzi ili muuone na kukumbuka amri zote za Yehova na kuzishika.+ Msifuate mioyo yenu na macho yenu, ambayo yanawaongoza kwenye ukahaba wa kiroho.+ 40  Upindo huo utawasaidia kukumbuka, nanyi mtashika amri zangu zote na kuwa watakatifu kwangu mimi Mungu wenu.+ 41  Mimi ni Yehova Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri ili nijithibitishe kuwa Mungu wenu.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.’”+

Maelezo ya Chini

Au “inayomtuliza.”
Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “maamuzi yaleyale ya hukumu.”
Tnn., “mkate wowote wa.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “Kosa lake litakuwa juu ya kichwa chake.”