Hesabu 16:1-50

  • Uasi wa Kora, Dathani, na Abiramu (1-19)

  • Waasi wahukumiwa (20-50)

16  Kisha Kora+ mwana wa Ishari,+ mwana wa Kohathi,+ mwana wa Lawi,+ akaungana na Dathani na Abiramu wana wa Eliabu,+ na Oni mwana wa Pelethi, wazao wa Rubeni.+  Nao, pamoja na wanaume 250 Waisraeli, wakuu wa kusanyiko, wanaume maarufu waliowekwa rasmi wakaanza kumpinga Musa.  Basi wakakusanyika dhidi ya+ Musa na Haruni na kuwaambia: “Mmetuchosha! Kusanyiko lote ni takatifu,+ watu wote, na Yehova yuko miongoni mwao.+ Basi, kwa nini mnajikweza juu ya kutaniko la Yehova?”  Musa aliposikia jambo hilo, mara moja akaanguka chini kifudifudi.  Kisha akamwambia Kora na watu wote waliomuunga mkono, “Asubuhi Yehova ataonyesha ni nani aliye wake+ na ni nani aliye mtakatifu na ni nani anayepaswa kumkaribia,+ na yeyote atakayemchagua+ ndiye atakayemkaribia.  Fanyeni hivi: Wewe Kora na wote wanaokuunga mkono,+ chukueni vyetezo,+  kesho wekeni moto ndani yake na kutia uvumba juu yake mbele za Yehova, na mtu ambaye Yehova atamchagua,+ ndiye mtakatifu. Ninyi wana wa Lawi+ mmevuka mpaka!”  Kisha Musa akamwambia Kora: “Sikilizeni, tafadhali, ninyi wana wa Lawi.  Je, mnaona ni jambo dogo sana kwenu kwamba Mungu wa Israeli amewateua ninyi miongoni mwa Waisraeli+ wote na kuwaruhusu mumkaribie ili kutumikia katika hema la Yehova la ibada na kusimama mbele ya Waisraeli wote ili kuwahudumia,+ 10  na kuwaleta karibu naye ninyi pamoja na ndugu zenu wote, wana wa Lawi? Je, ni lazima pia mjaribu kunyakua ukuhani?+ 11  Kwa sababu hiyo, wewe na watu wote wanaokuunga mkono mnampinga Yehova. Haruni ni nani hivi kwamba mnung’unike kumhusu?”+ 12  Baadaye Musa akatuma ujumbe ili Dathani na Abiramu+ wana wa Eliabu waitwe, lakini wakasema: “Hatutakuja! 13  Je, unafikiri ni jambo dogo kututoa katika nchi inayotiririka maziwa na asali ili utuue nyikani?+ Sasa, je, unataka kujifanya kiongozi mwenye mamlaka kamili juu yetu?* 14  Isitoshe, hujatuleta katika nchi yoyote inayotiririka maziwa na asali+ wala kutupatia urithi wa mashamba au shamba la mizabibu. Je, unataka kutoboa macho ya watu hawa? Sisi hatutakuja!” 15  Basi Musa akakasirika sana na kumwambia Yehova: “Usikubali toleo lao la nafaka. Sijachukua hata punda mmoja kutoka kwao, wala sijamdhuru mtu yeyote kati yao.”+ 16  Kisha Musa akamwambia Kora: “Kesho, fika mbele za Yehova, wewe pamoja na watu wote wanaokuunga mkono, wewe na watu hao pamoja na Haruni. 17  Kila mmoja wenu anapaswa kuchukua chetezo chake na kuweka uvumba juu yake, na kila mmoja atapeleka chetezo chake mbele za Yehova, vyetezo 250, pia wewe na Haruni mtapeleka kila mmoja chetezo chake.” 18  Basi kila mmoja wao akachukua chetezo chake, akaweka moto na uvumba juu yake na kusimama kwenye mlango wa hema la mkutano pamoja na Musa na Haruni. 19  Kora alipokuwa amewakusanya watu wote waliomuunga mkono+ kwenye mlango wa hema la mkutano ili kumpinga Musa na Haruni, utukufu wa Yehova ukawatokea watu wote waliokusanyika.+ 20  Kisha Yehova akamwambia Musa na Haruni, 21  “Jitengeni na kikundi hiki, ili nikiangamize mara moja.”+ 22  Ndipo Musa na Haruni wakaanguka chini kifudifudi na kusema: “Ee Mungu, Mungu wa roho ya watu wote,*+ je, dhambi ya mtu mmoja ikufanye uwakasirikie watu wote waliokusanyika?”+ 23  Basi Yehova akamwambia Musa, 24  “Waambie hivi watu wote: ‘Ondokeni karibu na mahema ya Kora, Dathani, na Abiramu!’”+ 25  Kisha Musa akaondoka na kwenda kwa Dathani na Abiramu, na wazee+ wa Israeli wakaenda pamoja naye. 26  Musa akawaambia hivi watu wote: “Tafadhali, ondokeni karibu na mahema ya watu hawa waovu wala msiguse kitu chochote ambacho ni mali yao, msije mkafagiliwa mbali kwa sababu ya dhambi yao yote.” 27  Mara moja wakaondoka karibu na mahema ya Kora, Dathani, na Abiramu, wakaondoka kila upande, kisha Dathani na Abiramu wakatoka nje, wakasimama kwenye mlango wa mahema yao pamoja na wake zao, wana wao, na watoto wao wachanga. 28  Halafu Musa akasema: “Hivi ndivyo mtakavyojua kwamba Yehova amenituma nifanye mambo haya yote, na kwamba sijayatunga moyoni mwangu:* 29  Watu hawa wakifa kama wanavyokufa wanadamu wengine wote na kuadhibiwa kama wanadamu wengine wote, basi Yehova hajanituma.+ 30  Lakini Yehova akiwatendea jambo lisilo la kawaida, ardhi ifunguke* na kuwameza watu hawa pamoja na vitu vyao vyote, nao waingie Kaburini* wakiwa hai, mtajua kwa hakika kwamba wamemdharau Yehova.” 31  Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, ardhi ikafunguka chini yao.+ 32  Naam, dunia ikafunguka* na kuwameza watu hao pamoja na familia zao na watu wote wa Kora+ na mali zao zote. 33  Kwa hiyo watu hao pamoja na watu wao wote wakaingia Kaburini* wakiwa hai, dunia ikawafunika, nao wakaangamia kutoka kati ya kutaniko.+ 34  Waisraeli wote waliokuwa wamewazunguka waliposikia vilio vyao wakakimbia wakisema: “Tunaogopa dunia itatumeza!” 35  Kisha moto ukashuka kutoka kwa Yehova+ na kuwateketeza wale wanaume 250 waliokuwa wakifukiza uvumba.+ 36  Kisha Yehova akamwambia Musa, 37  “Mwambie Eleazari mwana wa kuhani Haruni achukue vyetezo+ hivyo kutoka motoni kwa sababu ni vitakatifu. Mwambie pia autawanye moto huo mbali kidogo na mahali hapo. 38  Vyetezo vya wanaume waliouawa kwa sababu ya dhambi yao vinapaswa kunyooshwa ili viwe mabamba membamba ya kufunika madhabahu,+ kwa sababu walivipeleka mbele za Yehova, navyo vikawa vitakatifu. Vinapaswa kuwa onyo kwa Waisraeli.”+ 39  Basi kuhani Eleazari akachukua vyetezo vya shaba vilivyoletwa na wale wanaume waliokuwa wameteketezwa, akavipiga na kuvinyoosha ili vifunike madhabahu, 40  kama Yehova alivyomwambia kupitia Musa. Viliwakumbusha Waisraeli kwamba mtu yeyote asiye na idhini* ambaye si mzao wa Haruni hapaswi kukaribia madhabahu ili kumfukizia Yehova+ uvumba na kwamba mtu yeyote asiwe kama Kora na wale waliomuunga mkono.+ 41  Siku iliyofuata, kusanyiko lote la Waisraeli likaanza kumnung’unikia Musa na Haruni,+ likisema: “Ninyi wawili mmewaua watu wa Yehova.” 42  Watu wote walipokuwa wamekusanyika dhidi ya Musa na Haruni, waligeuka kuelekea hema la mkutano, na tazama! wingu lilifunika hema hilo, na utukufu wa Yehova ukaanza kuonekana.+ 43  Musa na Haruni wakaenda mbele ya hema la mkutano,+ 44  na Yehova akamwambia Musa, 45  “Ninyi wanaume, jitengeni na kusanyiko hili ili niliangamize mara moja.”+ Ndipo Musa na Haruni wakaanguka chini kifudifudi.+ 46  Kisha Musa akamwambia Haruni, “Chukua chetezo uweke moto ndani yake kutoka katika madhabahu+ na uweke uvumba juu yake, nawe uende haraka kwao na kuufukiza ili dhambi yao ifunikwe,+ kwa sababu Yehova amekasirika. Pigo limeanza!” 47  Mara moja Haruni akachukua chetezo, kama Musa alivyomwambia, akakimbia katikati ya kusanyiko hilo, na pigo lilikuwa limeanza kuwaathiri watu. Basi akaweka uvumba juu ya chetezo, akaanza kuufukiza ili dhambi yao ifunikwe. 48  Akaendelea kusimama katikati ya watu waliokufa na walio hai, hatimaye pigo hilo likaisha. 49  Watu waliokufa kutokana na pigo hilo walikuwa 14,700, bila kuwahesabu wale waliokufa kwa sababu ya Kora. 50  Mwishowe Haruni aliporudi kwa Musa kwenye mlango wa hema la mkutano, pigo hilo lilikuwa limekomeshwa.

Maelezo ya Chini

Au “kupiga ubwana juu yetu.”
Tnn., “roho za miili yote.”
Au “si matakwa yangu mwenyewe.”
Tnn., “ifungue kinywa chake.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “ikafungua kinywa chake.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “mgeni yeyote.”