Hesabu 19:1-22

  • Ng’ombe mwekundu na maji ya kutakasa (1-22)

19  Yehova akamwambia tena Musa na Haruni,  “Hii ndiyo sheria ambayo mimi Yehova nimeamuru, ‘Waambieni Waisraeli wawaletee ng’ombe mwekundu ambaye hana kasoro yoyote+ na ambaye hajawahi kufungwa nira.  Mtampa kuhani Eleazari ng’ombe huyo, naye atampeleka nje ya kambi na kuchinjwa mbele yake.  Kisha kuhani Eleazari atachukua kwa kidole chake kiasi kidogo cha damu ya ng’ombe huyo na kuinyunyiza mara saba kuelekea upande wa mbele wa hema la mkutano.+  Kisha ng’ombe huyo atateketezwa mbele ya macho yake. Ngozi yake na nyama yake na damu yake pamoja na mavi yake yatateketezwa.+  Halafu kuhani atachukua tawi la mwerezi, tawi la hisopo,+ na kitambaa chekundu na kutupa vitu hivyo katika moto unaomteketeza ng’ombe huyo.  Kisha kuhani atafua mavazi yake na kuoga kwenye maji, halafu anaweza kurudi kambini; lakini kuhani huyo hatakuwa safi mpaka jioni.  “‘Mtu aliyemteketeza ng’ombe huyo atafua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye hatakuwa safi mpaka jioni.  “‘Mtu aliye safi atayakusanya majivu ya ng’ombe huyo+ na kuyapeleka mahali safi nje ya kambi, yatahifadhiwa na Waisraeli ili yatumiwe kutengenezea maji ya kutakasa.+ Ni dhabihu ya dhambi. 10  Yule anayekusanya majivu ya ng’ombe huyo atafua mavazi yake, na hatakuwa safi mpaka jioni. “‘Hiyo itakuwa sheria ya kudumu kwa Waisraeli na wageni wanaoishi miongoni mwao.+ 11  Mtu yeyote anayemgusa mtu aliyekufa* hatakuwa safi kwa siku saba.+ 12  Mtu huyo anapaswa kujitakasa kwa maji hayo siku ya tatu, na siku ya saba atakuwa safi. Lakini asipojitakasa siku ya tatu, hatakuwa safi siku ya saba. 13  Mtu yeyote anayemgusa mtu aliyekufa lakini hajitakasi amechafua hema la Yehova la ibada,+ na ni lazima mtu huyo auawe kutoka katika Israeli.+ Kwa sababu hajanyunyiziwa maji ya kutakasa,+ ataendelea kuwa mchafu. Yeye bado ni mchafu. 14  “‘Hii ndiyo sheria kuhusu mtu anayefia ndani ya hema: Kila mtu anayeingia katika hema hilo na kila mtu aliyekuwa ndani ya hema hilo wakati huo, hatakuwa safi kwa siku saba. 15  Kila chombo kilichofunuliwa ambacho kifuniko chake hakijafungwa kwa kamba si safi.+ 16  Kila mtu aliye uwanjani anayemgusa mtu aliyeuawa kwa upanga au maiti au mfupa wa mtu au kaburi hatakuwa safi kwa siku saba.+ 17  Kwa ajili ya mtu huyo asiye safi, watachukua majivu ya dhabihu ya dhambi iliyoteketezwa na kuyamiminia maji ya kijito katika chombo. 18  Kisha mtu aliye safi+ atachukua tawi la hisopo+ na kulichovya ndani ya maji hayo na kunyunyizia hema na vyombo vyote na watu waliokuwa ndani ya hema hilo na mtu aliyegusa mfupa au mtu aliyeuawa au maiti au kaburi. 19  Siku ya tatu na siku ya saba, mtu aliye safi atamnyunyizia maji hayo mtu asiye safi na kumtakasa dhambi yake siku ya saba;+ kisha atafua mavazi yake na kuoga kwenye maji, naye atakuwa safi jioni. 20  “‘Lakini mtu asiye safi ambaye hatajitakasa ni lazima auawe kutoka kutanikoni+ kwa sababu amechafua mahali patakatifu pa Yehova. Kwa kuwa hakunyunyiziwa maji ya kutakasa, yeye si safi. 21  “‘Hii itakuwa sheria ya kudumu kwa ajili yao: Yule anayenyunyiza maji ya kutakasa+ anapaswa kufua mavazi yake, na yule anayegusa maji ya kutakasa hatakuwa safi mpaka jioni. 22  Kitu chochote kinachoguswa na mtu asiye safi hakitakuwa safi, na mtu anayekigusa hatakuwa safi mpaka jioni.’”+

Maelezo ya Chini

Au “nafsi iliyokufa ya mwanadamu yeyote.” Angalia Kamusi.