Hesabu 20:1-29

  • Miriamu afa kule Kadeshi (1)

  • Musa aupiga mwamba na hivyo kutenda dhambi (2-13)

  • Waedomu wawazuia Waisraeli kupita (14-21)

  • Kifo cha Haruni (22-29)

20  Katika mwezi wa kwanza, Waisraeli wote walifika katika nyika ya Zini, wakaanza kukaa Kadeshi.+ Miriamu+ akafa na kuzikwa huko.  Mahali hapo hapakuwa na maji kwa ajili ya Waisraeli,+ basi wakakusanyika dhidi ya Musa na Haruni.  Watu wakagombana na Musa+ wakisema: “Laiti tungekufa ndugu zetu walipokufa mbele za Yehova!  Kwa nini mmelileta kutaniko la Yehova katika nyika hii ili sisi na mifugo yetu tufie humu?+  Na kwa nini mlitutoa Misri na kutuleta mahali hapa paovu?+ Huku hakuna mbegu na tini na mizabibu na makomamanga, wala hakuna maji ya kunywa.”+  Basi Musa na Haruni wakatoka mbele yao na kwenda kwenye mlango wa hema la mkutano, wakaanguka chini kifudifudi, na utukufu wa Yehova ukaanza kuwatokea.+  Kisha Yehova akamwambia Musa,  “Ichukue ile fimbo, kisha wewe na Haruni ndugu yako muwakusanye watu wote, halafu uzungumze na mwamba mbele ya macho yao ili utoe maji, nawe utatoa maji katika mwamba huo na kuwapa watu wote pamoja na mifugo yao maji ya kunywa.”+  Kwa hiyo, Musa akachukua fimbo kutoka mbele za Yehova,+ kama Alivyomwamuru. 10  Basi Musa na Haruni wakawakusanya watu wote mbele ya mwamba huo, akawaambia, “Sikilizeni sasa, enyi waasi! Je, ni lazima tuwatolee maji katika mwamba huu?”+ 11  Ndipo Musa akainua mkono wake na kuupiga mwamba huo mara mbili kwa fimbo yake, na maji mengi yakaanza kububujika, watu wakaanza kunywa pamoja na mifugo yao.+ 12  Baadaye Yehova akamwambia hivi Musa na Haruni: “Kwa sababu hamkuonyesha kwamba mna imani kwangu na kunitakasa mbele ya Waisraeli, hamtawaingiza watu hawa katika nchi ambayo nitawapa.”+ 13  Hayo ndiyo maji ya Meriba,*+ mahali ambapo Waisraeli waligombana na Yehova, naye akawathibitishia kwamba yeye ni mtakatifu. 14  Kisha Musa akawatuma wajumbe kutoka Kadeshi ili waende kwa mfalme wa Edomu,+ wamwambie: “Ndugu yako Israeli+ anasema hivi: ‘Unajua vizuri matatizo yote tuliyopata. 15  Baba zetu walienda Misri,+ nasi tuliishi Misri kwa miaka mingi,*+ nao Wamisri walitutesa sisi na baba zetu.+ 16  Mwishowe tulimlilia Yehova,+ naye akasikia kilio chetu na kumtuma malaika;+ akatutoa Misri, na sasa tuko hapa Kadeshi, jiji linalopakana na eneo lako. 17  Tafadhali turuhusu tupite katika nchi yako. Hatutapita katika mashamba yenu au shamba lolote la mizabibu, nasi hatutakunywa maji ya kisima chochote. Tutafuata Barabara ya Mfalme bila kugeuka kulia au kushoto mpaka tutakapokuwa tumepita katika eneo lako.’”+ 18  Hata hivyo, mfalme wa Edomu akamwambia, “Usipite katika eneo letu. Ukipita, nitatoka na kukushambulia kwa upanga.” 19  Basi Waisraeli wakamwambia, “Tutafuata barabara kuu, na ikiwa sisi na mifugo yetu tutakunywa maji yako, tutalipa.+ Sisi tunataka tu kupita kwa miguu, hatutaki kitu kingine chochote.”+ 20  Lakini bado akasema, “Hamtapita.”+ Ndipo mfalme wa Edomu akatoka ili kumshambulia akiwa na watu wengi na jeshi lenye nguvu.* 21  Basi mfalme wa Edomu akakataa kuwaruhusu Waisraeli wapite katika eneo lake; kwa hiyo Waisraeli wakageuka na kumwacha.+ 22  Waisraeli wote wakaondoka Kadeshi na kufika kwenye Mlima Hori.+ 23  Kisha Yehova akamwambia hivi Musa na Haruni kwenye Mlima Hori karibu na mpaka wa nchi ya Edomu: 24  “Haruni atakufa na kuzikwa kama watu wake walivyozikwa.*+ Hataingia katika nchi nitakayowapa Waisraeli, kwa sababu ninyi wawili mliasi agizo nililowapa kuhusu maji ya Meriba.+ 25  Mchukue Haruni na Eleazari mwanawe, uwalete juu kwenye Mlima Hori. 26  Mvue Haruni mavazi yake+ umvishe Eleazari+ mwanawe, kisha Haruni atafia huko.”* 27  Basi Musa akafanya kama Yehova alivyomwamuru, nao wakapanda Mlima Hori watu wote wakiwatazama. 28  Kisha Musa akamvua Haruni mavazi yake na kumvisha Eleazari mwanawe. Baada ya hayo, Haruni akafa juu ya mlima huo.+ Kisha Musa na Eleazari wakateremka kutoka mlimani. 29  Waisraeli wote walipoona kwamba Haruni amekufa, nyumba yote ya Israeli ikamwombolezea Haruni kwa siku 30.+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Kugombana.”
Tnn., “siku nyingi.”
Tnn., “mkono wenye nguvu.”
Tnn., “atakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Tnn., “atakusanywa na kufia huko.”