Hesabu 27:1-23

  • Mabinti wa Selofehadi (1-11)

  • Yoshua achaguliwa ili achukue mahali pa Musa (12-23)

27  Kisha mabinti wa Selofehadi,+ mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa koo za Manase mwana wa Yosefu, wakaja. Mabinti hao waliitwa Mala, Noa, Hogla, Milka, na Tirsa.  Wakasimama mbele ya Musa, kuhani Eleazari, mbele ya wakuu,+ na mbele ya Waisraeli wote kwenye mlango wa hema la mkutano, wakasema:  “Baba yetu alikufa nyikani, lakini hakuwa miongoni mwa kikundi kilichojiunga na Kora kumpinga Yehova,+ bali alikufa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe naye hakuwa na mtoto yeyote wa kiume.  Kwa nini jina la baba yetu lipotee kutoka katika ukoo wake kwa sababu hakuwa na mtoto wa kiume? Tupe urithi miongoni mwa ndugu za baba yetu.”  Kwa hiyo Musa akawasilisha kesi yao mbele za Yehova.+  Basi Yehova akamwambia Musa hivi:  “Mabinti wa Selofehadi wanasema ukweli. Kwa vyovyote vile unapaswa kuwapa urithi miongoni mwa ndugu za baba yao na urithi wa baba yao.+  Nawe uwaambie Waisraeli hivi: ‘Mtu akifa bila kuacha mtoto wa kiume, mtampa binti yake urithi wake.  Na ikiwa hana binti, mtawapa ndugu zake urithi wake. 10  Na ikiwa hana ndugu, mtawapa ndugu za baba yake urithi wake. 11  Na ikiwa baba yake hana ndugu, mtampa urithi wake mtu wa karibu zaidi wa ukoo aliye na uhusiano wa damu naye. Uamuzi huu utakuwa sheria kwa Waisraeli, kama Yehova alivyomwamuru Musa.’” 12  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Panda mlima huu wa Abarimu,+ uione nchi nitakayowapa Waisraeli.+ 13  Baada ya kuiona, utakufa pia na kuzikwa pamoja na watu wako,*+ kama Haruni ndugu yako alivyozikwa,+ 14  kwa sababu Waisraeli walipokuwa wakigombana nami katika nyika ya Zini, mliasi agizo langu la kunitakasa mbele yao nilipowapa maji.+ Hayo ndiyo maji ya Meriba+ huko Kadeshi+ katika nyika ya Zini.”+ 15  Kisha Musa akamwambia hivi Yehova: 16  “Yehova, Mungu anayewapa watu wote uhai,* naomba umchague mwanamume atakayewasimamia watu hawa 17  ili awatangulie na kuwaongoza katika mambo yote, ili watu hawa wa Yehova wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji.” 18  Kwa hiyo Yehova akamwambia Musa: “Mchukue Yoshua mwana wa Nuni, mwanamume aliye na roho,* na uweke mikono yako juu yake.+ 19  Kisha umsimamishe mbele ya kuhani Eleazari na mbele ya watu wote, nawe umweke kuwa kiongozi.+ 20  Utampa sehemu ya mamlaka* yako,+ ili Waisraeli wote wamsikilize.+ 21  Atasimama mbele ya kuhani Eleazari, ambaye atatumia Urimu+ kujua uamuzi wa Yehova kwa niaba yake. Kwa agizo lake, yeye na Waisraeli wote na watu wengine wote watatoka, na kwa agizo lake wataingia ndani.” 22  Kwa hiyo Musa akafanya kama Yehova alivyomwamuru. Akamchukua Yoshua na kumsimamisha mbele ya kuhani Eleazari na mbele ya watu wote, 23  akaweka mikono yake juu yake na kumweka kuwa kiongozi,+ kama Yehova alivyosema kupitia Musa.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “utakusanywa pia kwa watu wako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Tnn., “Mungu wa roho za miili yote.”
Au “mtazamo unaofaa.”
Au “heshima.”