Hesabu 3:1-51

  • Wana wa Haruni (1-4)

  • Walawi wachaguliwa ili kuhudumu (5-39)

  • Kukombolewa kwa wazaliwa wa kwanza (40-51)

3  Basi hawa ndio waliokuwa wazao wa* Haruni na Musa siku ambayo Yehova alizungumza na Musa kwenye Mlima Sinai.+  Haya ndiyo majina ya wana wa Haruni: Nadabu mzaliwa wa kwanza, Abihu,+ Eleazari,+ na Ithamari.+  Hayo ndiyo majina ya wana wa Haruni waliotiwa mafuta ili watumikie wakiwa makuhani.+  Hata hivyo, Nadabu na Abihu walikufa mbele za Yehova walipomtolea Yehova moto haramu+ katika nyika ya Sinai, nao hawakuwa na wana wowote. Lakini Eleazari+ na Ithamari+ waliendelea kutumikia wakiwa makuhani pamoja na Haruni baba yao.  Kisha Yehova akamwambia Musa,  “Walete watu wa kabila la Lawi+ mbele ya kuhani Haruni ili wamhudumie.+  Watatimiza wajibu wao wa kumtumikia na kuwatumikia Waisraeli wote mbele ya hema la mkutano kwa kufanya kazi za hema la ibada.  Watatunza vyombo vyote+ vya hema la mkutano na kutimiza wajibu wao wa kuwatumikia Waisraeli kwa kufanya kazi za hema la ibada.+  Utawakabidhi Walawi kwa Haruni na wanawe. Ni watu waliokabidhiwa, ambao Haruni amekabidhiwa kutoka kati ya Waisraeli.+ 10  Unapaswa kumweka rasmi Haruni na wanawe ili watekeleze majukumu yao ya ukuhani,+ na mtu yeyote asiye na idhini* atakayekaribia mahali patakatifu anapaswa kuuawa.”+ 11  Yehova akaendelea kumwambia Musa, 12  “Tazama! Mimi nawachukua Walawi kutoka miongoni mwa Waisraeli badala ya wazaliwa wote wa kwanza* wa Waisraeli;+ Walawi watakuwa wangu. 13  Kwa maana kila mzaliwa wa kwanza ni wangu.+ Siku niliyomuua kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri+ nilijitakasia kila mzaliwa wa kwanza katika Israeli kuanzia mzaliwa wa kwanza wa mwanadamu mpaka wa mnyama.+ Watakuwa wangu. Mimi ni Yehova.” 14  Yehova akaendelea kuzungumza na Musa katika nyika ya Sinai,+ akamwambia: 15  “Waandikishe wana wa Lawi kila mmoja kulingana na ukoo wake* na familia yake. Unapaswa kumwandikisha kila mwanamume, kuanzia mtoto wa umri wa mwezi mmoja na zaidi.”+ 16  Kwa hiyo Musa akawaandikisha kama alivyoagizwa na Yehova, kama alivyoamriwa. 17  Haya ndiyo majina ya wana wa Lawi: Gershoni, Kohathi, na Merari.+ 18  Haya ndiyo majina ya wana wa Gershoni kulingana na familia zao: Libni na Shimei.+ 19  Wana wa Kohathi kulingana na familia zao walikuwa Amramu, Ishari, Hebroni, na Uzieli.+ 20  Wana wa Merari kulingana na familia zao walikuwa Mali+ na Mushi.+ Hizo ndizo zilizokuwa familia za Walawi kila mmoja kulingana na ukoo wake.* 21  Familia ya Walibni+ na familia ya Washimei zilitokana na Gershoni. Hizo ndizo zilizokuwa familia za Wagershoni. 22  Wanaume wao wote walioandikishwa kuanzia umri wa mwezi mmoja na zaidi walikuwa 7,500.+ 23  Familia za Wagershoni zilipiga kambi nyuma ya hema la ibada+ upande wa magharibi. 24  Mkuu wa ukoo* wa Wagershoni alikuwa Eliasafu mwana wa Laeli. 25  Majukumu ya wana wa Gershoni+ katika hema la mkutano yalikuwa kutunza hema lenyewe pamoja+ na kifuniko chake,+ pazia+ la mlango wa hema la mkutano, 26  mapazia ya ua yanayoning’inia,+ pazia la mlango wa ua+ linalozunguka hema la ibada na madhabahu, kamba za hema, na utumishi wote uliohusiana na vitu hivyo. 27  Familia ya Waamramu, familia ya Waishari, familia ya Wahebroni, na familia ya Wauzieli zilitokana na Kohathi. Hizo ndizo zilizokuwa familia za Wakohathi.+ 28  Wanaume wote kuanzia umri wa mwezi mmoja na zaidi walikuwa 8,600; jukumu lao lilikuwa kutunza mahali patakatifu.+ 29  Familia za wana wa Kohathi zilipiga kambi upande wa kusini wa hema la ibada.+ 30  Mkuu wa ukoo* wa familia za Wakohathi alikuwa Elisafani mwana wa Uzieli.+ 31  Majukumu yao yalikuwa kutunza Sanduku la Agano,+ meza,+ kinara cha taa,+ madhabahu,+ vyombo+ vilivyotumiwa katika utumishi wa mahali patakatifu, pazia,+ na utumishi wote uliohusiana na vitu hivyo.+ 32  Kiongozi wa wakuu wa Walawi alikuwa Eleazari+ mwana wa kuhani Haruni, naye aliwasimamia wale waliokuwa na majukumu ya kufanya kazi mahali patakatifu. 33  Familia ya Wamali na familia ya Wamushi zilizotokana na Merari. Hizo ndizo zilizokuwa familia za Merari.+ 34  Wanaume wote walioandikishwa kuanzia umri wa mwezi mmoja na zaidi walikuwa 6,200.+ 35  Mkuu wa ukoo* wa familia za Merari alikuwa Zurieli mwana wa Abihaili. Walipiga kambi upande wa kaskazini wa hema la ibada.+ 36  Wana wa Merari walikuwa na majukumu ya kusimamia viunzi+ vya hema la ibada, fito zake,+ nguzo zake,+ vikalio vyake, vyombo vyake vyote,+ na utumishi wote uliohusiana na vitu hivyo,+ 37  na pia nguzo zote zilizozunguka ua na vikalio vyake,+ vigingi vya hema, na kamba za hema hilo. 38  Musa na Haruni na wanawe walipiga kambi mbele ya hema la ibada upande wa mashariki, upande wa mapambazuko ya jua. Walikuwa na wajibu wa kutunza mahali patakatifu kwa niaba ya Waisraeli. Mtu yeyote asiye na idhini* ambaye angekaribia mahali patakatifu angeuawa.+ 39  Wanaume wote Walawi wenye umri wa kuanzia mwezi mmoja na zaidi walioandikishwa na Musa na Haruni kulingana na familia zao, kama Yehova alivyoagiza, walikuwa 22,000. 40  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Waandikishe wazaliwa wote wa kwanza wa kiume wa Waisraeli kuanzia umri wa mwezi mmoja na zaidi,+ wahesabu na kuorodhesha majina yao. 41  Wachukue Walawi kwa ajili yangu badala ya wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli,+ mimi ni Yehova, chukua pia mifugo ya Walawi badala ya wazaliwa wote wa kwanza wa mifugo ya Waisraeli.”+ 42  Ndipo Musa akawaandikisha wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli kama Yehova alivyomwamuru. 43  Wazaliwa wote wa kwanza wa kiume walioandikishwa kwa majina kuanzia umri wa mwezi mmoja na zaidi walikuwa 22,273. 44  Yehova akaendelea kumwambia Musa: 45  “Wachukue Walawi badala ya wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli, chukua pia mifugo ya Walawi badala ya mifugo ya Waisraeli, na Walawi watakuwa wangu. Mimi ni Yehova. 46  Ili kulipia bei ya fidia+ ya wale wazaliwa wa kwanza 273 wa Waisraeli ambao wanazidi idadi ya Walawi,+ 47  chukua shekeli tano* kwa ajili ya kila mmoja wao,+ kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* Shekeli moja ni sawa na gera 20.*+ 48  Utampa Haruni na wanawe pesa hizo ambazo ni bei ya fidia ya wale wanaozidi idadi yao.” 49  Kwa hiyo Musa akachukua pesa za ukombozi kutoka kwa wale waliozidi idadi ya wale waliofidiwa na Walawi. 50  Alichukua pesa hizo kutoka kwa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli, shekeli 1,365, kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu. 51  Kisha Musa akampa Haruni na wanawe pesa hizo za fidia kulingana na neno la* Yehova, kama Yehova alivyomwamuru Musa.

Maelezo ya Chini

Tnn., “hivi ndivyo vilivyokuwa vizazi vya.”
Tnn., “mgeni yeyote,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Au “kila kifungua mimba.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “Mgeni yeyote,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “shekeli takatifu.”
Gera moja ilikuwa na uzito wa gramu 0.57. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “kinywa cha.”