Hesabu 31:1-54

  • Wamidiani walipizwa kisasi (1-12)

    • Balaamu auawa (8)

  • Maagizo kuhusu nyara za vita (13-54)

31  Kisha Yehova akamwambia Musa:  “Walipize kisasi+ Wamidiani+ kwa sababu ya mambo waliyowatendea Waisraeli. Baadaye utakufa na kuzikwa pamoja na watu wako.”*+  Basi Musa akawaambia watu hivi: “Watayarisheni wanaume wakapigane* na Wamidiani na kulipiza kisasi cha Yehova dhidi yao.  Mtapeleka jeshini wanaume 1,000 kutoka katika kila kabila la Israeli.”  Kwa hiyo wanaume 1,000 kutoka katika kila kabila miongoni mwa maelfu ya Waisraeli,+ jumla ya wanaume 12,000, walitayarishwa kwa ajili ya vita.  Kisha Musa akawatuma vitani wanaume 1,000 kutoka katika kila kabila, wakiwa pamoja na Finehasi+ mwana wa kuhani Eleazari aliyebeba mkononi mwake vyombo vitakatifu na tarumbeta za kutangaza mwito.+  Walipigana na Wamidiani, kama Yehova alivyomwamuru Musa, wakawaua wanaume wote.  Miongoni mwa watu waliouawa kulikuwepo wafalme watano wa Midiani, yaani, Evi, Rekemu, Suri, Huru, na Reba. Pia, walimuua kwa upanga Balaamu+ mwana wa Beori.  Lakini Waisraeli waliwachukua mateka wanawake wa Midiani na watoto wao. Walichukua pia wanyama wao wote, naam, mifugo yao yote, na mali zao zote. 10  Waliteketeza majiji yote ambamo Wamidiani waliishi na kambi zao zote.* 11  Wakachukua nyara zote na mateka wote, wanadamu na wanyama. 12  Wakamletea Musa na kuhani Eleazari na Waisraeli wote mateka hao na nyara hizo kambini, katika jangwa tambarare la Moabu,+ karibu na Yordani huko Yeriko. 13  Kisha Musa na kuhani Eleazari na wakuu wote wa Waisraeli wakatoka ili kukutana nao nje ya kambi. 14  Lakini Musa alikasirishwa sana na wanaume waliowekwa kusimamia jeshi, yaani, wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia waliokuwa wakirudi kutoka vitani. 15  Musa akawauliza: “Kwa nini mmewaacha hai wanawake wote? 16  Kumbukeni kwamba hao ndio waliochochewa na Balaamu kuwashawishi Waisraeli wakose uaminifu+ kwa Yehova kule Peori,+ na kuwaletea pigo watu wa Yehova.+ 17  Sasa muueni kila mtoto wa kiume na kila mwanamke ambaye amewahi kufanya ngono na mwanamume. 18  Lakini msiwaue wasichana wote ambao hawajawahi kufanya ngono na mwanamume.+ 19  Nanyi mnapaswa kupiga kambi nje ya kambi kwa siku saba. Kila mtu miongoni mwenu ambaye amemuua mtu na kila mtu ambaye amemgusa mtu aliyeuawa+ anapaswa kujitakasa+ siku ya tatu na siku ya saba, ninyi na mateka wenu. 20  Mnapaswa pia kutakasa kutokana na dhambi kila vazi, kila kitu kilichotengenezwa kwa ngozi, kila kitu kilichotengenezwa kwa manyoya ya mbuzi, na kila kitu kilichotengenezwa kwa mbao.” 21  Ndipo kuhani Eleazari akawaambia wanaume walioenda vitani: “Hii ndiyo sheria ambayo Yehova amempa Musa, 22  ‘Ni dhahabu, fedha, shaba, chuma, bati, na madini ya risasi tu, 23  yaani, kila kitu kinachoweza kustahimili moto, ndicho mnachopaswa kupitisha motoni, nacho kitakuwa safi. Hata hivyo, kinapaswa pia kusafishwa kwa maji ya kutakasa.+ Kila kitu ambacho hakiwezi kustahimili moto, mnapaswa kukitakasa kwa maji. 24  Nanyi mnapaswa kufua mavazi yenu siku ya saba na kuwa safi, kisha mnaweza kuingia kambini.’”+ 25  Tena Yehova akamwambia Musa hivi: 26  “Wewe pamoja na kuhani Eleazari na viongozi wa koo* za Waisraeli hesabuni nyara zote, kutia ndani wanadamu na wanyama waliotekwa. 27  Gaweni nyara hizo katika mafungu mawili, ili wanajeshi walioenda vitani wapate fungu moja na Waisraeli wengine fungu lingine.+ 28  Kutoka kwa wanajeshi walioenda vitani, mtachukua nafsi* moja kutoka kwa kila nafsi 500 za wanadamu, za ng’ombe, za punda, na kondoo ili iwe kodi ya Yehova. 29  Mnapaswa kuchukua nafsi hizo kutoka katika fungu lao na kumpa kuhani Eleazari kama mchango kwa Yehova.+ 30  Kutoka katika fungu ambalo Waisraeli watapewa, mnapaswa kuchukua nafsi moja kutoka kwa kila nafsi 50 za wanadamu, za ng’ombe, za punda, za kondoo, na za kila aina ya mnyama wa kufugwa, na kuwapa Walawi,+ wanaotimiza majukumu katika hema la Yehova la ibada.”+ 31  Basi Musa na kuhani Eleazari wakafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa. 32  Nyara na vitu vyote ambavyo watu walichukua vitani ni kondoo 675,000, 33  ng’ombe 72,000, 34  na punda 61,000. 35  Wanawake ambao hawakuwa wamefanya ngono na mwanamume+ walikuwa wanawake* 32,000. 36  Na nusu iliyokuwa fungu la wale walioenda vitani ilikuwa kondoo 337,500. 37  Kondoo 675 kati yao walichukuliwa ili kuwa kodi kwa Yehova. 38  Pia, kulikuwa na ng’ombe 36,000, na ng’ombe 72 kati yao walichukuliwa ili kuwa kodi kwa Yehova. 39  Punda walikuwa 30,500, na punda 61 kati yao walichukuliwa ili kuwa kodi kwa Yehova. 40  Wanadamu walikuwa 16,000, na 32 kati yao walichukuliwa ili kuwa kodi kwa Yehova. 41  Kisha Musa akampa kuhani Eleazari kodi hiyo iwe mchango wa Yehova,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 42  Ile nusu waliyopewa Waisraeli ambayo Musa aliitenga na nusu waliyopewa wanajeshi walioenda vitani, 43  ilikuwa kondoo 337,500, 44  ng’ombe 36,000, 45  punda 30,500, 46  na wanadamu 16,000. 47  Kisha kutoka katika nusu hiyo ambayo ni fungu la Waisraeli, Musa alichukua nafsi moja kutoka kwa kila nafsi 50 za wanadamu na za wanyama akawapa Walawi+ waliotimiza majukumu katika hema la Yehova la ibada,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 48  Kisha wanaume waliowekwa kusimamia maelfu ya wanajeshi,+ yaani, wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia, wakamfikia Musa, 49  na kumwambia: “Sisi watumishi wako tumewahesabu wanajeshi walio chini ya usimamizi wetu, na hakuna hata mmoja wao anayekosekana.+ 50  Kwa hiyo mruhusu kila mmoja wetu atoe vitu alivyopata ili viwe vya Yehova, yaani, vitu vya dhahabu, mikufu ya miguuni, bangili, pete za muhuri, vipuli, na vito vingine, ili Yehova afunike dhambi zetu.” 51  Basi Musa na kuhani Eleazari wakapokea dhahabu hiyo kutoka kwao, naam, vito vyote. 52  Dhahabu yote ambayo wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia walimtolea Yehova mchango ilikuwa shekeli 16,750.* 53  Kila mwanajeshi alikuwa amejichukulia nyara. 54  Musa na kuhani Eleazari walipokea dhahabu hiyo kutoka kwa wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia na kuileta katika hema la mkutano ili iwe kumbukumbu mbele za Yehova kwa ajili ya Waisraeli.

Maelezo ya Chini

Tnn., “utakusanywa kwa watu wako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au “Tayarisheni jeshi likapigane.”
Au “kambi zao zote zilizozingirwa na kuta.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Angalia Kamusi.
Au “nafsi.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.