Hesabu 32:1-42

  • Waliobaki upande wa mashariki wa Yordani (1-42)

32  Sasa wana wa Rubeni+ na wana wa Gadi+ walikuwa na mifugo mingi sana, wakaona kwamba eneo la Yazeri+ na eneo la Gileadi yalikuwa maeneo mazuri kwa mifugo.  Basi wana wa Gadi na wana wa Rubeni wakaja kwa Musa, kuhani Eleazari, na wakuu wa Waisraeli na kuwaambia hivi:  “Atarothi, Diboni, Yazeri, Nimra, Heshboni,+ Eleale, Sebamu, Nebo,+ na Beoni,+  maeneo ambayo Yehova aliyashinda mbele ya Waisraeli,+ ni maeneo mazuri kwa mifugo, nasi watumishi wenu tuna mifugo mingi.”+  Wakaendelea kusema, “Ikiwa sisi watumishi wenu tumepata kibali machoni penu, tupeni maeneo haya tuyamiliki. Msituvushe ng’ambo ya Mto Yordani.”  Lakini Musa akawaambia hivi wana wa Gadi na wana wa Rubeni: “Je, ndugu zenu wataenda vitani huku ninyi mkiendelea kukaa hapa?  Kwa nini muwavunje moyo Waisraeli wasivuke kuingia katika nchi ambayo kwa hakika Yehova atawapa?  Hivyo ndivyo baba zenu walivyofanya nilipowatuma kutoka Kadesh-barnea wakaione ile nchi.+  Walipofika kwenye Bonde la Eshkoli+ na kuiona nchi hiyo, waliwavunja moyo Waisraeli wasiingie katika nchi ambayo Yehova angewapa.+ 10  Yehova aliwaka hasira siku hiyo na kuapa hivi:+ 11  ‘Wanaume waliotoka Misri wenye umri wa kuanzia miaka 20 na zaidi hawataiona nchi+ ambayo niliapa kwamba nitampa Abrahamu, Isaka, na Yakobo,+ kwa sababu hawakunifuata kwa moyo wote— 12  isipokuwa Kalebu+ mwana wa Yefune, Mkenizi, na Yoshua+ mwana wa Nuni, kwa sababu wamenifuata mimi Yehova kwa moyo wote.’+ 13  Basi hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli naye akawafanya watangetange nyikani kwa miaka 40,+ mpaka kizazi chote kilichokuwa kikifanya maovu machoni pa Yehova kilipoangamia.+ 14  Na sasa ninyi mmekuwa kama baba zenu, kundi la watenda dhambi wanaozidisha hasira kali ya Yehova dhidi ya Waisraeli. 15  Mkigeuka na kuacha kumfuata, kwa hakika atawaacha tena watu hawa nyikani, nanyi mtasababisha watu hawa wote waangamizwe.” 16  Baadaye wakaja tena kwake na kumwambia: “Turuhusu tujenge hapa mazizi ya mawe kwa ajili ya mifugo yetu na majiji kwa ajili ya watoto wetu. 17  Lakini sisi tutaendelea kuwa tayari kwa ajili ya vita+ na tutakuwa mstari wa mbele mpaka tutakapowafikisha Waisraeli mahali pao, wakati huo watoto wetu watakaa katika majiji yenye ngome, wakiwa salama kutoka kwa wakaaji wa nchi. 18  Hatutarudi katika nyumba zetu mpaka kila Mwisraeli atakaporithi eneo lake.+ 19  Kwa maana hatutapokea urithi wowote pamoja nao katika eneo lote lililo ng’ambo ya Yordani, kwa sababu tumepokea urithi wetu upande wa mashariki wa Yordani.”+ 20  Musa akawaambia: “Ikiwa mtafanya hivi: Ikiwa mtachukua silaha mbele za Yehova kwa ajili ya vita;+ 21  na ikiwa kila mmoja wenu atachukua silaha na kuvuka Yordani mbele za Yehova anapowafukuza maadui wake kutoka mbele zake+ 22  mpaka mtakaposhinda na kuichukua nchi mbele za Yehova,+ mnaweza kurudi+ nanyi hamtakuwa na hatia mbele za Yehova na Waisraeli. Ndipo Yehova atakapokubali mmiliki nchi hii.+ 23  Lakini msipofanya hivyo, mtakuwa mmemtendea dhambi Yehova. Nanyi mjue kwamba mtaadhibiwa kwa sababu ya dhambi yenu. 24  Kwa hiyo mnaweza kujenga majiji kwa ajili ya watoto wenu na mazizi kwa ajili ya mifugo yenu,+ lakini ni lazima mfanye mambo mliyoahidi.” 25  Wana wa Gadi na wana wa Rubeni wakamwambia Musa hivi: “Bwana wetu, sisi watumishi wako tutafanya kama unavyotuamuru. 26  Watoto wetu, wake zetu, mifugo yetu, na wanyama wetu wote watabaki hapa katika majiji ya Gileadi,+ 27  lakini sisi watumishi wako tutavuka, kila mwanamume aliyechukua silaha ili kupigana vita mbele za Yehova,+ kama unavyosema bwana wetu.” 28  Basi Musa akampa kuhani Eleazari, Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi wa koo* za makabila ya Waisraeli amri kuwahusu. 29  Musa akawaambia hivi: “Ikiwa wana wa Gadi na wana wa Rubeni watavuka Yordani pamoja nanyi, yaani, kila mwanamume aliyechukua silaha ili kupigana vita mbele za Yehova, nanyi mshinde na kuchukua eneo hilo, basi mtawapa eneo la Gileadi ili walimiliki.+ 30  Lakini ikiwa hawatachukua silaha na kuvuka pamoja nanyi, basi wataishi pamoja nanyi katika nchi ya Kanaani.” 31  Basi wana wa Gadi na wana wa Rubeni wakajibu: “Sisi watumishi wako tutafanya mambo ambayo Yehova ametuambia. 32  Tutachukua silaha na kuvuka mbele za Yehova kuingia nchi ya Kanaani,+ lakini urithi wetu utakuwa upande huu wa Yordani.” 33  Hivyo Musa akawapa—wana wa Gadi, wana wa Rubeni,+ na nusu ya kabila la Manase+ mwana wa Yosefu—ufalme wa Sihoni+ mfalme wa Waamori na ufalme wa Ogu+ mfalme wa Bashani, maeneo hayo na majiji yaliyokuwemo na pia majiji jirani. 34  Wana wa Gadi wakajenga* Diboni,+ Atarothi,+ Aroeri,+ 35  Atroth-shofani, Yazeri,+ Yogbeha,+ 36  Beth-nimra,+ Beth-harani,+ majiji yenye ngome, na mazizi ya mawe kwa ajili ya mifugo. 37  Nao wana wa Rubeni wakajenga Heshboni,+ Eleale,+ Kiriathaimu,+ 38  Nebo,+ na Baal-meoni+—majina ya majiji hayo yalibadilishwa—na Sibma; nao wakaanza kuyapa majina mapya majiji waliyojenga upya. 39  Wana wa Makiri+ mwana wa Manase walishambulia eneo la Gileadi, wakaliteka, na kuwafukuza Waamori waliokaa humo. 40  Kwa hiyo Musa akampa Makiri mwana wa Manase, Gileadi, akaanza kukaa katika eneo hilo.+ 41  Na Yairi mwana wa Manase akawashambulia wakaaji wa eneo hilo na kuteka vijiji vyao vya mahema, akaviita Hawoth-yairi.*+ 42  Naye Noba akashambulia na kuliteka jiji la Kenathi na miji yake, naye akaliita Noba, jina lake mwenyewe.

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “wakajenga upya.”
Maana yake “Vijiji vya Mahema vya Yairi.”