Hesabu 34:1-29

  • Mipaka ya Kanaani (1-15)

  • Wanaume wapewa kazi ya kuigawanya nchi (16-29)

34  Yehova akaendelea kumwambia Musa:   “Wape Waisraeli maagizo haya: ‘Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani,+ nchi mtakayoirithi, hii ndiyo itakayokuwa mipaka ya nchi hiyo ya Kanaani.+  “‘Mpaka wenu wa kusini utaanzia nyika ya Zini kando ya Edomu, na upande wa mashariki mpaka huo wa kusini utaanzia mwisho wa Bahari ya Chumvi.+  Kisha mpaka huo utapinda na kwenda upande wa kusini wa mwinuko wa Akrabimu,+ nao utaendelea mpaka Zini na kuishia upande wa kusini wa Kadesh-barnea.+ Kisha utaenda Hasar-adari+ na kuendelea mpaka Asimoni.  Mpaka huo utapinda huko Asimoni na kuelekea kwenye Bonde la Misri na kuishia kwenye Bahari ya Mediterania.+  “‘Mpaka wenu wa magharibi utakuwa Bahari Kuu* na pwani. Huo utakuwa mpaka wenu wa magharibi.+  “‘Huu ndio utakaokuwa mpaka wenu wa kaskazini: Mtaweka alama kuanzia Bahari Kuu mpaka Mlima Hori.+  Kutoka Mlima Hori mtaweka alama mpaka Lebo-hamathi,*+ nao utaishia Sedadi.+  Kisha utaendelea hadi Zifroni na kuishia Hasar-enani.+ Huo utakuwa mpaka wenu wa kaskazini. 10  “‘Kisha mtaweka alama ya mpaka wenu wa mashariki kuanzia Hasar-enani hadi Shefamu. 11  Mpaka huo utaanzia Shefamu hadi Ribla, upande wa mashariki wa Aini, nao utashuka na kuvuka mteremko wa mashariki wa Bahari ya Kinerethi.*+ 12  Kisha utaendelea mpaka Yordani na kuishia kwenye Bahari ya Chumvi.+ Hiyo ndiyo itakayokuwa nchi yenu+ na mipaka inayoizunguka.’” 13  Kwa hiyo Musa akawapa Waisraeli maagizo haya: “Hiyo ndiyo nchi mtakayoigawanya kwa kura na kuimiliki,+ kama Yehova alivyoamuru kwamba makabila tisa na nusu yapewe nchi hiyo. 14  Kwa maana kabila la Rubeni kulingana na koo zao,* kabila la Gadi kulingana na koo zao,* na nusu ya kabila la Manase tayari yamechukua urithi wao.+ 15  Makabila hayo mawili na nusu tayari yamechukua urithi wao upande wa mashariki wa Yordani karibu na Yeriko, upande wa mapambazuko ya jua.”+ 16  Yehova akaendelea kumwambia Musa, 17  “Haya ndiyo majina ya wanaume watakaowagawia nchi ili mwimiliki: kuhani Eleazari+ na Yoshua+ mwana wa Nuni. 18  Nanyi mtachukua mkuu mmoja kutoka katika kila kabila ili awasaidie kuigawanya nchi mtakayorithi.+ 19  Haya ndiyo majina ya wanaume hao: kutoka kabila la Yuda,+ Kalebu+ mwana wa Yefune; 20  kutoka kabila la wana wa Simeoni,+ Shemueli mwana wa Amihudi; 21  kutoka kabila la Benjamini,+ Elidadi mwana wa Kisloni; 22  kutoka kabila la wana wa Dani,+ mkuu mmoja, Buki mwana wa Yogli; 23  kutoka kwa wana wa Yosefu,+ kwa ajili ya kabila la wana wa Manase,+ mkuu mmoja, Hanieli mwana wa Efodi; 24  kutoka kabila la wana wa Efraimu,+ mkuu mmoja, Kemueli mwana wa Shiftani; 25  kutoka kabila la wana wa Zabuloni,+ mkuu mmoja, Elisafani mwana wa Parnaki; 26  kutoka kabila la wana wa Isakari,+ mkuu mmoja, Paltieli mwana wa Azani; 27  kutoka kabila la wana wa Asheri,+ mkuu mmoja, Ahihudi mwana wa Shelomi, 28  na kutoka kabila la wana wa Naftali,+ mkuu mmoja, Pedaheli mwana wa Amihudi.” 29  Hao ndio wanaume ambao Yehova aliamuru wawagawie Waisraeli ardhi katika nchi ya Kanaani.+

Maelezo ya Chini

Yaani, Mediterania.
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Yaani, ziwa la Genesareti, au Bahari ya Galilaya.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.