Hesabu 6:1-27

  • Nadhiri ya Unadhiri (1-21)

  • Baraka ya makuhani (22-27)

6  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mwanamume au mwanamke akiweka nadhiri ya pekee ya kuishi akiwa Mnadhiri*+ kwa Yehova,  anapaswa kujiepusha na divai na vinywaji vingine vyenye kileo. Hapaswi kunywa siki ya divai au siki ya kitu chochote chenye kileo.+ Hapaswi kamwe kunywa maji ya zabibu, wala kula zabibu zilizotoka kuchumwa au zilizokaushwa.  Siku zote atakazokuwa Mnadhiri hapaswi kula kitu chochote kinachotokana na mzabibu, kuanzia zabibu ambazo hazijaiva mpaka maganda yake.  “‘Siku zote atakazokuwa Mnadhiri hakuna wembe utakaogusa kichwa chake.+ Ataendelea kuwa mtakatifu kwa kuacha nywele za kichwa chake ziwe ndefu mpaka siku alizojitenga kwa ajili ya Yehova zitakapokwisha.  Siku zote alizojitenga kwa ajili ya Yehova hapaswi kumkaribia mtu aliyekufa.*  Hata baba yake au mama yake au ndugu yake au dada yake akifa, hapaswi kujichafua,+ kwa sababu ishara ya kwamba yeye ni Mnadhiri kwa Mungu iko juu ya kichwa chake.  “‘Atakuwa mtakatifu kwa Yehova siku zote atakazokuwa Mnadhiri.  Lakini mtu akifa ghafla kando yake+ na kuchafua nywele zake ambazo ni ishara ya kwamba amejitenga kwa ajili ya Mungu,* ni lazima anyoe kichwa chake+ siku anapothibitisha utakaso wake. Anapaswa kukinyoa siku ya saba. 10  Na siku ya nane anapaswa kumpelekea kuhani njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga kwenye mlango wa hema la mkutano. 11  Kuhani atamtoa ndege mmoja kuwa dhabihu ya dhambi na mwingine kuwa dhabihu ya kuteketezwa ili kufunika dhambi aliyotenda+ kwa kumgusa mtu aliyekufa.* Kisha anapaswa kutakasa kichwa chake siku hiyo. 12  Ni lazima ajitenge tena kwa ajili ya Yehova na kuanza upya siku za Unadhiri wake, naye ataleta mwanakondoo dume wa mwaka mmoja kuwa dhabihu ya hatia. Hata hivyo, zile siku za awali hazitahesabiwa kwa sababu aliuchafua Unadhiri wake. 13  “‘Hii ndiyo sheria inayomhusu Mnadhiri: Atakapomaliza siku zake za kuwa Mnadhiri,+ ataletwa kwenye mlango wa hema la mkutano. 14  Akiwa hapo atamtolea Yehova dhabihu zake: mwanakondoo dume wa mwaka mmoja asiye na kasoro kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa,+ mwanakondoo jike wa mwaka mmoja asiye na kasoro kwa ajili ya dhabihu ya dhambi,+ kondoo dume mmoja asiye na kasoro kwa ajili ya dhabihu ya ushirika,+ 15  kikapu cha mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyookwa kwa unga laini uliochanganywa na mafuta, mikate myembamba isiyo na chachu na iliyopakwa mafuta, na toleo la nafaka+ na matoleo ya vinywaji ya dhabihu hizo.+ 16  Kuhani atatoa vitu hivyo mbele za Yehova na kutoa dhabihu ya dhambi na dhabihu ya kuteketezwa kwa ajili ya mtu huyo. 17  Kisha atamtolea Yehova kondoo dume kwa ajili ya dhabihu ya ushirika pamoja na kikapu cha mikate isiyo na chachu, pia atatoa toleo la nafaka+ pamoja na toleo la kinywaji la dhabihu hiyo. 18  “‘Halafu ni lazima Mnadhiri huyo anyoe nywele za kichwa chake*+ kwenye mlango wa hema la mkutano, naye atachukua nywele hizo za Unadhiri wake na kuzitia katika moto ulio chini ya dhabihu ya ushirika. 19  Kisha kuhani atachukua mguu wa mbele uliochemshwa+ wa yule kondoo dume, mkate mmoja wa mviringo usio na chachu kutoka katika kile kikapu, na mkate mmoja mwembamba usio na chachu, na kuviweka mikononi mwa Mnadhiri huyo baada ya nywele zake za Unadhiri kunyolewa. 20  Halafu kuhani atavitikisa vitu hivyo kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ Ni vitu vitakatifu kwa kuhani, pamoja na kidari cha toleo la kutikiswa na mguu uliotolewa kama mchango.+ Baada ya hayo, Mnadhiri huyo anaweza kunywa divai. 21  “‘Hii ndiyo sheria inayomhusu Mnadhiri+ anayeweka nadhiri: Akiweka nadhiri na iwe kwamba anaweza kumtolea Yehova toleo ambalo halihitajiwi katika kutimiza Unadhiri wake, ni lazima atimize nadhiri yake kulingana na sheria ya Unadhiri wake.’” 22  Kisha Yehova akamwambia Musa: 23  “Mwambie hivi Haruni na wanawe: ‘Hivi ndivyo mtakavyowabariki+ Waisraeli. Waambieni: 24  “Yehova na awabariki+ na kuwalinda. 25  Yehova na awaangazie nuru ya uso wake,+ na kuwapa kibali chake. 26  Yehova na ainue uso wake kuwaelekea na kuwapa amani.”’+ 27  Ni lazima waliweke jina langu juu ya Waisraeli,+ ili niwabariki Waisraeli.”+

Maelezo ya Chini

Katika Kiebrania ni na·zirʹ, linalomaanisha “Aliyetengwa; Aliyewekwa Wakfu; Aliyewekwa Kando.”
Au “kuikaribia nafsi iliyokufa.” Angalia Kamusi.
Au “kutia unajisi kichwa cha Unadhiri wake.”
Au “kugusa nafsi iliyokufa.”
Au “kichwa cha Unadhiri wake.”