Hesabu 9:1-23

  • Mpango wa kuadhimisha Pasaka baadaye (1-14)

  • Wingu na moto juu ya hema la ibada (15-23)

9  Yehova akazungumza na Musa katika nyika ya Sinai katika mwezi wa kwanza+ wa mwaka wa pili baada ya wao kutoka nchini Misri, akamwambia:  “Waisraeli wanapaswa kutayarisha dhabihu ya Pasaka+ wakati wake uliopangwa.+  Siku ya 14 ya mwezi huo kabla ya giza kuingia,* mnapaswa kuitayarisha wakati wake uliopangwa. Mnapaswa kuitayarisha kulingana na sheria zake zote na utaratibu wake wote uliowekwa.”+  Basi Musa akawaambia Waisraeli waitayarishe dhabihu ya Pasaka.  Kwa hiyo wakaitayarisha dhabihu ya Pasaka katika nyika ya Sinai katika mwezi wa kwanza, siku ya 14 ya mwezi huo kabla ya giza kuingia.* Waisraeli walifanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa.  Sasa watu fulani hawakuwa safi kwa sababu waligusa mtu aliyekufa,+ hivyo hawangeweza kuitayarisha dhabihu ya Pasaka siku hiyo. Kwa hiyo wakaenda kumwona Musa na Haruni siku hiyo,+  wakamwambia Musa: “Sisi si safi kwa sababu tumemgusa mtu aliyekufa. Kwa nini tukatazwe kumtolea Yehova dhabihu kwa wakati uliopangwa pamoja na Waisraeli wengine?”+  Ndipo Musa akawaambia: “Ngojeni hapo, acheni nione Yehova ataamuru nini kuwahusu.”+  Yehova akamwambia Musa: 10  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mtu yeyote miongoni mwenu au miongoni mwa vizazi vyenu vijavyo akijichafua kwa kumgusa mtu aliyekufa+ au akisafiri mbali, bado anapaswa kumtayarishia Yehova dhabihu ya Pasaka. 11  Watu hao wanapaswa kuitayarisha katika mwezi wa pili,+ siku ya 14 kabla ya giza kuingia.* Wanapaswa kuila pamoja na mikate isiyo na chachu na mboga chungu.+ 12  Hawapaswi kuacha chochote mpaka asubuhi,+ wala hawapaswi kuvunja mfupa wowote wa dhabihu hiyo.+ Wanapaswa kuitayarisha kulingana na sheria zote za Pasaka. 13  Lakini ikiwa mtu alikuwa safi au hakuwa amesafiri naye amepuuza kuitayarisha dhabihu ya Pasaka, ni lazima mtu huyo auawe kutoka kati ya watu wake+ kwa sababu hakumtolea Yehova dhabihu hiyo kwa wakati wake uliopangwa. Mtu huyo ataadhibiwa kwa sababu ya dhambi yake. 14  “‘Ikiwa unaishi na mgeni, anapaswa pia kumtayarishia Yehova dhabihu ya Pasaka.+ Anapaswa kuitayarisha kulingana na sheria na utaratibu uliowekwa wa Pasaka.+ Ninyi nyote mtafuata sheria moja, mkaaji mgeni pamoja na mwenyeji wa nchi.’”+ 15  Siku ambayo hema la ibada lilijengwa,+ wingu lilifunika hema la ibada, yaani, hema la Ushahidi, lakini wakati wa jioni kitu kilichoonekana kama moto kilikaa juu ya hema hilo mpaka asubuhi.+ 16  Hivi ndivyo ilivyokuwa kila siku: Wingu hilo lilifunika hema wakati wa mchana, na kitu kilichoonekana kama moto kilikaa juu ya hema wakati wa usiku.+ 17  Kila mara wingu hilo lilipoinuka kutoka juu ya hema, Waisraeli waliondoka bila kukawia,+ na mahali ambapo wingu hilo lilisimama, hapo ndipo Waisraeli walipopiga kambi.+ 18  Waisraeli waliondoka kwa agizo la Yehova, na kwa agizo la Yehova walipiga kambi.+ Waliendelea kupiga kambi muda wote ambao wingu hilo lilikaa juu ya hema la ibada. 19  Wingu hilo lilipokaa juu ya hema la ibada kwa siku nyingi, Waisraeli walimtii Yehova nao hawakuondoka.+ 20  Nyakati nyingine wingu hilo lilikaa juu ya hema la ibada kwa siku chache. Waliendelea kupiga kambi kwa agizo la Yehova, na kwa agizo la Yehova waliondoka. 21  Nyakati fulani wingu hilo lilikaa juu ya hema la ibada kuanzia jioni mpaka asubuhi tu, na wingu hilo lilipoinuka asubuhi, waliondoka. Iwe liliinuka mchana au usiku, waliondoka.+ 22  Iwe ni kwa siku mbili, mwezi mmoja, au muda mrefu zaidi, muda wote ambao wingu hilo lilikaa juu ya hema la ibada, Waisraeli waliendelea kupiga kambi nao hawakuondoka. Lakini lilipoinuka waliondoka. 23  Walipiga kambi kwa agizo la Yehova, na kwa agizo la Yehova waliondoka. Walitimiza wajibu wao kwa Yehova kama Yehova alivyowaagiza kupitia Musa.

Maelezo ya Chini

Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”