Isaya 14:1-32

  • Waisraeli wataishi katika nchi yao (1, 2)

  • Dhihaka dhidi ya mfalme wa Babiloni (3-23)

    • Anayeng’aa ataanguka kutoka mbinguni (12)

  • Mkono wa Yehova utamponda Mwashuru (24-27)

  • Tangazo dhidi ya Ufilisti (28-32)

14  Kwa maana Yehova atamwonyesha rehema Yakobo,+ naye atawachagua tena Waisraeli.+ Atawafanya waishi* katika nchi yao,+ na wakaaji wageni watajiunga nao na kushikamana na nyumba ya Yakobo.+  Na watu watawachukua na kuwaleta mahali pao wenyewe, na nyumba ya Israeli itawamiliki katika nchi ya Yehova wakiwa watumishi wa kiume na wa kike;+ nao watawateka wale waliokuwa wamewateka, nao watawatiisha wale waliokuwa wakiwalazimisha kufanya kazi.*  Siku ambayo Yehova atakupumzisha kutokana na uchungu wako na kutokana na msukosuko wako na kutokana na utumwa mgumu uliowekwa chini yake,+  utaisema methali* hii dhidi ya mfalme wa Babiloni: “Jinsi yule anayewalazimisha wengine kufanya kazi* alivyofikia mwisho wake! Jinsi ukandamizaji ulivyokwisha!+   Yehova ameivunja fimbo ya waovu,Gongo la watawala,+   Yule anayewapiga watu kwa hasira kwa mapigo yasiyokoma,+Yule anayeyatiisha mataifa kwa hasira kwa mateso yasiyoisha.+   Dunia nzima imepumzika sasa, haina usumbufu. Watu wanapaza sauti kwa shangwe.+   Hata miberoshi inakushangilia,Pamoja na mierezi ya Lebanoni. Inasema, ‘Tangu ulipoanguka,Hakuna mkataji wa miti anayekuja kutukata.’   Hata Kaburi* chini limevurugikaIli likupokee utakapoingia. Kwa sababu yako, linawaamsha wale waliokufa ambao hawana uwezo,Viongozi wote wa dunia wanaokandamiza.* Linawafanya wafalme wote wa mataifa wasimame kutoka kwenye viti vyao vya ufalme. 10  Wote wanaanza kusema na kukuambia,‘Je, wewe pia umedhoofika kama sisi? Je, umekuwa kama sisi? 11  Kiburi chako kimeshushwa chini mpaka Kaburini,*Sauti ya vinanda vyako.+ Funza wametandikwa chini yako kama kitanda,Na blanketi lako ni minyoo.’ 12  Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni,Ewe unayeng’aa, mwana wa mapambazuko! Jinsi ulivyokatwa ukaangushwa duniani,Wewe uliyeyashinda mataifa!+ 13  Ulisema moyoni mwako, ‘Nitapanda juu mbinguni.+ Nitakiinua kiti changu cha ufalme juu ya nyota za Mungu,+Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano,Katika sehemu za mbali zaidi za kaskazini.+ 14  Nitaenda juu ya mawingu;Nitajifananisha na Aliye Juu Zaidi.’ 15  Badala yake, utashushwa chini mpaka Kaburini,*Katika sehemu zenye kina zaidi za shimo. 16  Wale wanaokuona watakukodolea macho;Watakuchunguza kwa makini, wakisema,‘Je, huyu ndiye yule mtu aliyekuwa akiitikisa dunia,Aliyekuwa akizitetemesha falme,+ 17  Aliyeifanya dunia inayokaliwa iwe kama nyikaNa kuyapindua majiji yake,+Aliyekataa kuwaruhusu wafungwa wake waende nyumbani?’+ 18  Wafalme wengine wote wa mataifa,Naam, wote, wamelala chini katika utukufu,Kila mmoja katika kaburi lake* mwenyewe. 19  Lakini wewe, umetupwa bila kaburi,Kama chipukizi* lililochukiwa,Ukiwa umevishwa watu waliouawa kwa kuchomwa upanga,Wanaoshuka chini kwenye mawe ya shimoni,Kama mzoga uliokanyagiwa chini kwa miguu. 20  Hutaungana nao kaburini,Kwa maana uliiharibu nchi yako mwenyewe,Uliwaua watu wako mwenyewe. Uzao wa watenda maovu hautatajwa tena kamwe. 21  Tayarisheni ubao wa kuwachinjia wanaweKwa sababu ya hatia ya mababu zao,Ili wasiinuke na kuimiliki duniaNa kuyajaza majiji yao katika nchi.” 22  “Nitainuka dhidi yao,”+ asema Yehova wa majeshi. “Nami nitafuta kabisa kutoka Babiloni jina na watu waliobaki na watoto na wazao,”+ asema Yehova. 23  “Nami nitamfanya kuwa makao ya nungunungu na eneo lenye umajimaji, nami nitamfagia kwa ufagio wa maangamizi,”+ asema Yehova wa majeshi. 24  Yehova wa majeshi ameapa hivi: “Kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotukia,Na kama nilivyoamua, ndivyo itakavyotimia. 25  Nitamponda Mwashuru katika nchi yanguNami nitamkanyaga-kanyaga kwenye milima yangu.+ Nira yake itaondolewa juu yao,Na mzigo wake utaondolewa juu ya bega lao.”+ 26  Hili ndilo jambo lililoamuliwa* dhidi ya dunia yote,Na huu ndio mkono ulionyooshwa* dhidi ya mataifa yote. 27  Kwa maana Yehova wa majeshi ameamua,Na ni nani anayeweza kulizuia?+ Mkono wake umenyooshwa,Ni nani anayeweza kuurudisha nyuma?+ 28  Katika mwaka ambao Mfalme Ahazi alikufa,+ tangazo hili lilitolewa: 29  “Usishangilie, ewe Ufilisti, yeyote kati yenu,Kwa sababu tu gongo la yule anayewapiga limevunjwa. Kwa maana kwenye mzizi wa nyoka+ atatoka nyoka mwenye sumu,+Na uzao wake utakuwa nyoka wa moto arukaye.* 30  Huku wazaliwa wa kwanza wa watu wa hali ya chini wakilaNa maskini wakilala kwa usalama,Nitauua mzizi wako kwa njaa kali,Na kile kitakachobaki kwako kitauawa.+ 31  Omboleza kwa sauti, ewe lango! Paza kilio, ewe jiji! Ninyi nyote mtavunjika moyo, ewe Ufilisti! Kwa maana moshi unakuja kutoka kaskazini,Na hakuna wavivu katika vikosi vyake.” 32  Watawajibuje wajumbe wa taifa lile? Kwamba Yehova ameuweka msingi wa Sayuni,+Na kwamba watu wa hali ya chini kati ya watu wake watakimbilia ndani yake.

Maelezo ya Chini

Au “Atawapumzisha.”
Au “wasimamizi wao wa kazi.”
Au “dhihaka.”
Au “msimamizi wa kazi.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “Mbuzi dume wote wa dunia wanaokandamiza.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “nyumba yake.”
Au “tawi.”
Tnn., “Hili ndilo shauri lililotolewa.”
Au “ulio tayari kupiga.”
Au “nyoka mwenye sumu anayerukaruka.”