Isaya 37:1-38

  • Hezekia atafuta msaada wa Mungu kupitia Isaya (1-7)

  • Senakeribu atishia Yerusalemu (8-13)

  • Sala ya Hezekia (14-20)

  • Isaya apeleka jibu la Mungu (21-35)

  • Malaika awaua Waashuru 185,000 (36-38)

37  Mara tu Mfalme Hezekia aliposikia hilo, akayararua mavazi yake na kuvaa nguo za magunia na kuingia katika nyumba ya Yehova.+  Kisha akamtuma Eliakimu, aliyekuwa msimamizi wa nyumba,* Shebna aliyekuwa mwandishi, na wazee miongoni mwa makuhani, wakiwa wamevaa nguo za magunia, waende kwa nabii Isaya,+ mwana wa Amozi.  Wakamwambia: “Hezekia anasema hivi: ‘Leo ni siku ya taabu, ya kemeo,* na ya aibu; kwa maana watoto wako tayari kuzaliwa* lakini hakuna nguvu za kuwazaa.+  Huenda Yehova Mungu wako atayasikia maneno ya Rabshake, aliyetumwa na bwana wake mfalme wa Ashuru ili amdhihaki Mungu aliye hai,+ naye atamfanya awajibike kwa sababu ya maneno ambayo Yehova Mungu wako amesikia. Basi toa sala+ kwa niaba ya watu waliobaki ambao wameokoka.’”+  Kwa hiyo watumishi wa Mfalme Hezekia wakaenda kwa Isaya,+  naye Isaya akawaambia: “Mwambieni hivi bwana wenu, ‘Yehova anasema hivi: “Usiogope+ kwa sababu ya maneno uliyosikia, maneno ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru+ waliyasema na kunikufuru.  Sasa ninatia wazo fulani akilini mwake,* naye atasikia habari na kurudi katika nchi yake mwenyewe;+ nami nitamuua kwa upanga katika nchi yake mwenyewe.”’”+  Baada ya Rabshake kusikia kwamba mfalme wa Ashuru ameondoka Lakishi, alirudi na kumkuta akipigana vita na Libna.+  Ndipo mfalme akasikia maneno haya yakisemwa kumhusu Tirhaka mfalme wa Ethiopia: “Amekuja ili kupigana nawe.” Aliposikia hivyo, akawatuma tena wajumbe kwa Hezekia,+ akisema: 10  “Mwambieni hivi Mfalme Hezekia wa Yuda, ‘Usikubali Mungu wako unayemtumaini akudanganye akisema: “Yerusalemu halitatiwa mikononi mwa mfalme wa Ashuru.”+ 11  Tazama! Umesikia mambo ambayo wafalme wa Ashuru walizitendea nchi zote kwa kuziangamiza.+ Je, ni wewe peke yako utakayeokolewa? 12  Je, miungu ya mataifa yaliyoangamizwa na mababu zangu iliyaokoa mataifa hayo?+ Gozani, Harani,+ Resefu, na watu wa Edeni waliokuwa Tel-asari wako wapi? 13  Yuko wapi mfalme wa Hamathi, mfalme wa Arpadi, na mfalme wa majiji ya Sefarvaimu,+ na wa Hena, na wa Iva?’” 14  Hezekia akachukua barua hizo kutoka mikononi mwa wajumbe na kuzisoma. Kisha Hezekia akapanda kwenda katika nyumba ya Yehova, akazitandaza* mbele za Yehova.+ 15  Hezekia akaanza kusali kwa Yehova+ akisema: 16  “Ee Yehova wa majeshi,+ Mungu wa Israeli, unayeketi kwenye kiti cha ufalme juu ya* makerubi, wewe peke yako ndiye Mungu wa kweli wa falme zote za dunia. Uliumba mbingu na dunia. 17  Tega sikio lako, Ee Yehova, usikie!+ Fungua macho yako, Ee Yehova, uone!+ Sikia maneno yote ambayo Senakeribu amesema ili kukudhihaki wewe Mungu uliye hai.+ 18  Ee Yehova, ni kweli kwamba wafalme wa Ashuru wameharibu nchi zote,+ na pia nchi yao. 19  Nao wameitupa miungu yao motoni,+ kwa sababu haikuwa miungu bali kazi ya mikono ya wanadamu,+ miti na mawe. Ndiyo sababu waliweza kuiangamiza. 20  Lakini sasa, Ee Yehova Mungu wetu, tuokoe kutoka mikononi mwake, ili falme zote duniani zijue kwamba wewe peke yako ndiye Mungu, Ee Yehova.”+ 21  Kisha Isaya mwana wa Amozi akatuma ujumbe huu kwa Hezekia: “Yehova Mungu wa Israeli anasema, ‘Kwa sababu ulisali kwangu kuhusu Mfalme Senakeribu wa Ashuru,+ 22  Hili ndilo neno ambalo Yehova amesema dhidi yake: “Binti bikira wa Sayuni anakudharau, anakudhihaki. Binti ya Yerusalemu anakutikisia kichwa. 23  Umemdhihaki+ na kumkufuru nani? Umepaza sauti yako dhidi ya nani+Na kuinua macho yako yenye kiburi? Ni dhidi ya Mtakatifu wa Israeli!+ 24  Kupitia watumishi wako umemdhihaki Yehova+ ukisema,‘Kwa wingi wa magari yangu ya vitaNitapanda vilele vya milima,+Sehemu za mbali sana za Lebanoni. Nitakata mierezi yake mirefu sana, miberoshi yake iliyo bora. Nitaingia mahali pake palipo juu zaidi, misitu yake yenye miti mingi sana. 25  Nitachimba visima na kunywa maji;Nitavikausha vijito vya* Misri kwa nyayo za miguu yangu.’ 26  Je, hujasikia? Tangu zamani za kale liliamuliwa.* Tangu siku zilizopita nimelitayarisha.*+ Sasa nitalitimiza.+ Utayabadili majiji yenye ngome yawe marundo ya magofu yenye ukiwa.+ 27  Wakaaji wake hawatakuwa na uwezo;Wataogopeshwa na kuaibishwa. Watakuwa kama mimea ya shambani na nyasi mbichi,Kama nyasi zilizo kwenye paa zinazokaushwa na upepo wa mashariki. 28  Lakini ninajua vizuri unapoketi, unapotoka nje, unapoingia,+Na unapokuwa na ghadhabu dhidi yangu,+ 29  Kwa sababu ghadhabu yako dhidi yangu+ na mngurumo wako umefika masikioni mwangu.+ Basi nitatia kulabu yangu puani mwako na lijamu yangu+ katikati ya midomo yako,Nami nitakurudisha kupitia njia uliyotumia kuja.” 30  “‘Na hii ndiyo itakayokuwa ishara kwako:* Mwaka huu utakula mimea inayoota yenyewe;* na katika mwaka wa pili utakula nafaka inayochipuka kutoka katika mimea hiyo; lakini katika mwaka wa tatu utapanda mbegu na kuvuna, nawe utapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.+ 31  Watu wa nyumba ya Yuda watakaoponyoka, wale wanaobaki,+ watatia mizizi chini na kuzaa matunda kwenda juu. 32  Kwa maana waliobaki watatoka Yerusalemu na waokokaji watatoka katika Mlima Sayuni.+ Bidii ya Yehova wa majeshi itatenda hayo.+ 33  “‘Kwa hiyo Yehova anasema hivi kuhusu mfalme wa Ashuru:+ “Hataingia katika jiji hili+Wala hatapiga mshale humoWala kulikabili kwa ngaoWala kujenga boma la kulizingira.”’+ 34  ‘Atarudi kupitia njia aliyotumia kuja;Hataingia katika jiji hili,’ asema Yehova. 35  ‘Nitalilinda jiji hili+ na kuliokoa kwa ajili yangu+ mwenyeweNa kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu.’”+ 36  Na malaika wa Yehova akaenda na kuwaua wanaume 185,000 katika kambi ya Waashuru. Watu walipoamka asubuhi na mapema, waliona maiti zote hizo.+ 37  Basi Mfalme Senakeribu wa Ashuru akaondoka, akarudi Ninawi+ na kukaa huko.+ 38  Na alipokuwa akiinama katika nyumba ya* Nisroki mungu wake, watoto wake mwenyewe wa kiume Adrameleki na Shareza, walimuua kwa upanga+ na kutorokea nchi ya Ararati.+ Na Esar-hadoni+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “jumba la mfalme.”
Au “matusi.”
Tnn., “wamefika kwenye mlango wa tumbo la uzazi.”
Tnn., “ninatia roho fulani ndani yake.”
Tnn., “akaitandaza.”
Au labda, “katikati ya.”
Au “Nitaikausha mifereji ya Nile ya.”
Tnn., “lilifanywa.”
Au “nimelitengeneza.”
Au “nafaka zilizoanguka na kuota zenyewe.”
Yaani, Hezekia.
Au “hekalu la.”