Isaya 39:1-8

  • Wajumbe kutoka Babiloni (1-8)

39  Wakati huo mfalme wa Babiloni, Merodak-baladani mwana wa Baladani alimtumia Hezekia barua na zawadi,+ kwa maana alisikia kwamba alikuwa mgonjwa na sasa amepona.+  Hezekia akawakaribisha kwa furaha* na kuwaonyesha nyumba yake yenye hazina+—fedha, dhahabu, mafuta ya zeri na mafuta mengine yenye thamani, ghala lake lote la silaha, na kila kitu kilichokuwa katika hazina zake. Hakuna kitu chochote ambacho Hezekia hakuwaonyesha katika nyumba yake mwenyewe* na katika milki yake yote.  Kisha nabii Isaya akaenda kwa Mfalme Hezekia na kumuuliza: “Watu hawa walisema nini, nao walitoka wapi?” Hezekia akajibu: “Walitoka katika nchi ya mbali, kutoka Babiloni.”+  Kisha akauliza: “Waliona nini katika nyumba yako?”* Hezekia akajibu: “Waliona kila kitu katika nyumba yangu.* Hakuna chochote ambacho sikuwaonyesha katika hazina zangu.”  Sasa Isaya akamwambia Hezekia: “Sikia neno la Yehova wa majeshi,  ‘Tazama! Siku zinakuja, na vitu vyote vilivyo katika nyumba yako* na vitu vyote ambavyo mababu zako wamehifadhi mpaka leo hii vitapelekwa Babiloni. Hakuna chochote kitakachobaki,’+ asema Yehova.+  ‘Na baadhi ya wana wako mwenyewe utakaowazaa watachukuliwa na kuwa maofisa wa makao ya mfalme katika jumba la mfalme wa Babiloni.’”+  Ndipo Hezekia akamwambia Isaya: “Neno la Yehova ambalo umesema ni jema.” Kisha akasema: “Kwa sababu kutakuwa na amani na utulivu* wakati wa maisha yangu.”*+

Maelezo ya Chini

Tnn., “akawashangilia.”
Au “jumba lake mwenyewe la mfalme.”
Au “jumba lako la mfalme?”
Au “jumba langu la mfalme.”
Au “jumba lako la mfalme.”
Au “ukweli.”
Tnn., “katika siku zangu.”