Isaya 60:1-22
60 “Inuka, Ee mwanamke,+ angaza nuru, kwa maana nuru yako imekuja.
Utukufu wa Yehova unakuangazia.+
2 Kwa maana tazama! giza litaifunika duniaNa utusitusi mzito utayafunika mataifa;Lakini Yehova atakuangazia,Na utukufu wake utaonekana juu yako.
3 Mataifa yataenda kwenye nuru yako+Na wafalme+ kwenye fahari yako inayong’aa.*+
4 Inua macho yako utazame pande zote kukuzunguka!
Wote wamekusanywa; wanakuja kwako.
Wana wako wanaendelea kuja kutoka mbali sana,+Na mabinti wako wakiwa wametegemezwa viunoni.+
5 Wakati huo utaona na kung’aa,+Na moyo wako utadundadunda na kufurika,Kwa sababu utajiri wa bahari utaelekezwa kwako;Mali za mataifa zitakuja kwako.+
6 Makundi ya ngamia yataifunika nchi yako,*Ngamia dume wachanga wa Midiani na Efa.+
Wote kutoka Sheba—watakuja;Watabeba dhahabu na ubani.
Watatangaza sifa za Yehova.+
7 Makundi yote ya Kedari+ yatakusanywa kwako.
Kondoo dume wa Nebayothi+ watakutumikia.
Watakuja kwenye madhabahu yangu wakiwa na kibali,+Nami nitairembesha nyumba yangu yenye utukufu.*+
8 Ni nani hawa wanaokuja wakiruka kama mawingu,Kama njiwa kwenye viota vyao?*
9 Kwa maana visiwa vitanitumaini;+Meli za Tarshishi zinaongoza,*Kuwaleta wana wako kutoka mbali sana,+Pamoja na fedha yao na dhahabu yao,Kwa sifa ya jina la Yehova Mungu wako na ya Mtakatifu wa Israeli,Kwa maana atakutukuza.*+
10 Wageni watazijenga kuta zako,Na wafalme wao watakuhudumia,+Kwa maana nilikupiga kwa hasira yangu,Lakini kwa kibali changu* nitakuonyesha rehema.+
11 Malango yako yatakuwa wazi daima;+Hayatafungwa mchana wala usiku,Ili kukuletea mali za mataifa,Na wafalme wao wataongoza.+
12 Kwa maana taifa lolote na ufalme wowote ambao hautakutumikia utaangamia,Nayo mataifa yataharibiwa kabisa.+
13 Utukufu wa Lebanoni utakuja kwako,+Mberoshi, mtidhari, na mvinje pamoja,+Ili kuparembesha mahali pangu patakatifu;Nitapatukuza mahali pa miguu yangu.+
14 Wana wa wale waliokukandamiza watakuja na kuinama chini mbele yako;Wote wanaokudharau watainama chini miguuni pako,Nao watalazimika kukuita jiji la Yehova,Sayuni la Mtakatifu wa Israeli.+
15 Badala ya kuwa aliyeachwa na kuchukiwa, bila yeyote kupita ndani yako,+Nitakufanya uwe chanzo cha fahari ya milele,Chanzo cha shangwe kwa vizazi vyote.+
16 Nawe kwa kweli utakunywa maziwa ya mataifa,+Utanyonya matiti ya wafalme;+Nawe hakika utajua kwamba mimi, Yehova, ni Mwokozi wako,Na Mwenye Nguvu wa Yakobo ni Mkombozi wako.+
17 Badala ya shaba nitaleta dhahabu,Na badala ya chuma nitaleta fedha,Badala ya mbao, shaba,Na badala ya mawe, chuma;Nitaweka amani kuwa waangalizi wakoNa uadilifu kuwa watu wako wanaogawa kazi.+
18 Ukatili hautasikiwa tena katika nchi yakoWala maangamizi na uharibifu katika mipaka yako.+
Nawe utaziita kuta zako Wokovu+ na malango yako Sifa.
19 Kwa maana jua halitakuwa tena nuru ya mchana kwako,Wala nuru ya mwezi haitakuangazia,Kwa maana Yehova atakuwa nuru ya milele kwako,+Na Mungu wako atakuwa urembo wako.+
20 Jua lako halitatua tena,Wala mwezi wako hautafifia,Kwa maana Yehova atakuwa nuru yako ya milele,+Na siku zako za kuomboleza zitakuwa zimekwisha.+
21 Na watu wako wote watakuwa waadilifu;Wataimiliki nchi milele.
Wao ndio chipukizi nililopanda,Kazi ya mikono yangu,+ ili nirembeshwe.+
22 Mdogo atakuwa elfuNa mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu.
Mimi mwenyewe, Yehova, nitaliharakisha jambo hilo kwa wakati wake.”