Kumbukumbu la Torati 1:1-46

  • Kuondoka Mlima Horebu (1-8)

  • Wakuu na waamuzi wawekwa (9-18)

  • Watu wakosa kutii kule Kadesh-barnea (19-46)

    • Waisraeli wakataa kuingia katika ile nchi (26-33)

    • Washindwa kuteka Kanaani (41-46)

1  Haya ndiyo maneno ambayo Musa aliwaambia Waisraeli wote walipokuwa nyikani katika eneo la Yordani, katika jangwa tambarare mbele ya Sufi, kati ya Parani, Tofeli, Labani, Haserothi, na Dizahabu.  Ni safari ya siku 11 kutoka Horebu mpaka Kadesh-barnea+ kupitia njia ya Mlima Seiri.  Katika mwaka wa 40,+ mwezi wa 11, siku ya kwanza ya mwezi huo, Musa aliwaambia Waisraeli* mambo yote ambayo Yehova alimwagiza awaambie.  Alifanya hivyo baada ya kumshinda Sihoni+ mfalme wa Waamori, aliyekuwa akikaa Heshboni, na Ogu+ mfalme wa Bashani, aliyekuwa akikaa Ashtarothi, kule Edrei.+  Katika eneo la Yordani nchini Moabu, Musa alianza kuifafanua Sheria+ akisema:  “Yehova Mungu wetu alituambia hivi kule Horebu: ‘Mmekaa muda wa kutosha katika eneo hili lenye milima.+  Geukeni na kuelekea katika eneo lenye milima la Waamori+ na kwa majirani wao wote kule Araba,+ katika eneo lenye milima, Shefela, Negebu, pwani ya bahari,+ nchi ya Wakanaani, na Lebanoni,*+ hadi kwenye ule mto mkubwa, Mto Efrati.+  Angalieni, nimeweka nchi hii mbele yenu. Ingieni mwimiliki nchi ambayo mimi Yehova niliapa kwamba nitawapa baba zenu, Abrahamu, Isaka,+ na Yakobo,+ wao pamoja na uzao wao* baada yao.’+  “Nami niliwaambia ninyi wakati huo, ‘Siwezi kuwabeba peke yangu.+ 10  Yehova Mungu wenu amewafanya mwongezeke, nanyi leo ni wengi kama nyota za mbinguni.+ 11  Yehova Mungu wa mababu zenu na awafanye mwongezeke+ mara elfu moja zaidi ya mlivyo sasa, na awabariki kama alivyowaahidi.+ 12  Mimi peke yangu ninawezaje kuwabeba ninyi ambao ni mzigo pamoja na mizigo yenu na ugomvi wenu?+ 13  Chagueni wanaume wenye hekima, busara, na wenye uzoefu kutoka katika makabila yenu, nami nitawaweka kuwa viongozi wenu.’+ 14  Mkanijibu, ‘Jambo ulilotuambia ni jema.’ 15  Basi nikawachukua viongozi wa makabila yenu, wanaume wenye hekima na uzoefu, na kuwaweka kuwa viongozi wenu, wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, wakuu wa makumi, na maofisa wa makabila yenu.+ 16  “Wakati huo niliwaagiza hivi waamuzi wenu: ‘Mnaposikiliza kesi kati ya ndugu zenu, mnapaswa kuhukumu kwa uadilifu+ kati ya mtu na ndugu yake au mkaaji mgeni.+ 17  Hampaswi kuhukumu kwa upendeleo.+ Mnapaswa kumsikiliza mdogo kama mnavyomsikiliza mkubwa.+ Msiogopeshwe na wanadamu,+ kwa sababu hukumu ni ya Mungu;+ na ikiwa kesi ni ngumu sana kwenu, ileteni kwangu, nami nitaisikiliza.’+ 18  Wakati huo niliwapa maagizo kuhusu mambo yote mnayopaswa kufanya. 19  “Kisha tukaondoka Horebu na kupitia ile nyika yote kubwa na yenye kutisha+ mliyoona njiani kuelekea kwenye eneo lenye milima la Waamori,+ kama Yehova Mungu wetu alivyotuamuru, na mwishowe tukafika Kadesh-barnea.+ 20  Halafu nikawaambia, ‘Mmefika kwenye eneo lenye milima la Waamori, ambalo Yehova Mungu wetu anatupatia. 21  Angalieni, Yehova Mungu wenu amewapa nchi hii. Pandeni, mkaimiliki, kama Yehova, Mungu wa mababu zenu alivyowaambia.+ Msiogope wala msiwe na hofu.’ 22  “Hata hivyo, ninyi nyote mlinijia na kusema, ‘Na tutume wanaume watutangulie na kuipeleleza nchi kwa ajili yetu, watuletee habari kuhusu njia tunayopaswa kufuata na ni majiji ya aina gani tutakayoyapata huko.’+ 23  Pendekezo hilo lilionekana zuri kwangu, kwa hiyo nikawachagua wanaume 12 miongoni mwa wanaume wenu, mwanamume mmoja kwa ajili ya kila kabila.+ 24  Wakaondoka na kupanda kwenda kwenye eneo lenye milima,+ wakafika kwenye Bonde la Eshkoli na kuipeleleza nchi. 25  Wakachukua baadhi ya matunda ya nchi hiyo na kutuletea, nao wakatuletea habari hii: ‘Nchi ambayo Yehova Mungu wetu anatupatia ni nzuri.’+ 26  Lakini mlikataa kupanda kwenda huko, nanyi mkaliasi agizo la Yehova Mungu wenu.+ 27  Mliendelea kunung’unika katika mahema yenu na kusema, ‘Yehova alituchukia ndiyo sababu alitutoa katika nchi ya Misri ili atutie mikononi mwa Waamori watuangamize. 28  Tunaenda mahali pa aina gani? Ndugu zetu walituvunja moyo*+ waliposema, “Watu hao wana nguvu zaidi na ni warefu zaidi kuliko sisi, na majiji yao ni makubwa na yana ngome zinazofika mbinguni,*+ na huko tuliwaona wana wa Waanaki.”’+ 29  “Kwa hiyo nikawaambia, ‘Msiwe na hofu wala msiogope kwa sababu yao.+ 30  Yehova Mungu wenu atawatangulia na kuwapigania,+ kama alivyofanya kule Misri mbele ya macho yenu wenyewe.+ 31  Nanyi mliona nyikani jinsi Yehova Mungu wenu alivyowabeba kama baba anavyombeba mwana wake, aliwabeba kila mahali mlipoenda mpaka mlipofika mahali hapa.’ 32  Lakini licha ya hayo yote, hamkuwa na imani katika Yehova Mungu wenu,+ 33  aliyekuwa akiwatangulia njiani ili apeleleze mahali mtakapopiga kambi. Alitokea kwa moto wakati wa usiku na kwa wingu wakati wa mchana ili awaonyeshe njia mnayopaswa kufuata.+ 34  “Wakati huo wote Yehova alisikia mambo mliyokuwa mkisema, akakasirika na kuapa hivi:+ 35  ‘Hakuna mtu hata mmoja wa kizazi hiki kiovu atakayeona nchi nzuri niliyoapa kwamba nitawapa baba zenu,+ 36  isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune. Yeye ataiona, nami nitampa yeye na wanawe nchi hiyo aliyoikanyaga kwa miguu yake, kwa sababu amenifuata mimi Yehova kwa moyo wote.*+ 37  (Yehova alinikasirikia mimi pia kwa sababu yenu, akasema, “Wewe pia hutaingia humo.+ 38  Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wako,*+ ndiye atakayeingia katika nchi hiyo.+ Mwimarishe,*+ kwa maana atawawezesha Waisraeli kuirithi nchi hiyo.”) 39  Isitoshe, watoto wenu ambao mlisema watakuwa nyara+ na wana wenu ambao leo hawajui lililo jema wala baya, hao ndio watakaoingia katika nchi hiyo, nami nitawapa ili waimiliki.+ 40  Lakini ninyi, geukeni na kwenda nyikani kupitia njia ya Bahari Nyekundu.’+ 41  “Ndipo mliponiambia, ‘Tumemtendea Yehova dhambi. Sasa tutapanda kwenda kupigana, kama Yehova Mungu wetu alivyotuamuru!’ Basi kila mmoja wenu akajivika silaha zake za vita, nanyi mlifikiri ni rahisi kupanda mlimani.+ 42  Lakini Yehova akaniambia, ‘Waambie, “Msipande kwenda kupigana, kwa sababu sitakuwa pamoja nanyi.+ Mkienda, maadui wenu watawashinda.”’ 43  Basi nikaongea nanyi, lakini hamkusikiliza. Badala yake, mliasi agizo la Yehova na kujaribu kwa kimbelembele kupanda mlimani. 44  Kisha Waamori waliokuwa wakikaa kwenye mlima huo wakatoka ili kuwashambulia, wakawakimbiza kama nyuki wanavyofanya na kuwatawanya kuanzia Seiri mpaka Horma. 45  Basi mkarudi na kuanza kumlilia Yehova, lakini Yehova hakuwasikiliza wala kuwakazia uangalifu. 46  Ndiyo sababu mliendelea kukaa Kadeshi kwa muda wote mliokaa huko.

Maelezo ya Chini

Tnn., “wana wa Israeli.”
Inaonekana ni safu ya milima ya Lebanoni.
Tnn., “mbegu yao.”
Tnn., “walifanya moyo wetu uyeyuke.”
Yaani, yana kuta ndefu sana.
Tnn., “kikamilifu; kabisa.”
Tnn., “anayesimama mbele yako.”
Au labda, “Mungu amemwimarisha.”