Kumbukumbu la Torati 11:1-32

  • Mmeuona ukuu wa Yehova (1-7)

  • Nchi Iliyoahidiwa (8-12)

  • Thawabu za kutii (13-17)

  • Maneno ya Mungu yakaziwe katika mioyo (18-25)

  • “Baraka na laana” (26-32)

11  “Ni lazima mumpende Yehova Mungu wenu+ na kutimiza sikuzote wajibu wenu kwake, sheria zake, maagizo yake, na amri zake.  Mnajua kwamba leo ninazungumza nanyi, si na wana wenu ambao hawajajua wala kuona nidhamu ya Yehova Mungu wenu,+ ukuu wake,+ mkono wake wenye nguvu+ na mkono wake ulionyooshwa.  Hawakuona ishara zake na matendo yake aliyotenda Misri kwa Farao mfalme wa Misri na kwa nchi yake yote;+  wala mambo aliyoyatendea majeshi ya Misri, farasi wa Farao na magari yake ya vita, ambayo yalifunikwa na maji ya Bahari Nyekundu walipokuwa wakiwafuatia ninyi, na Yehova akawaangamiza milele.*+  Hawakuona mambo aliyowatendea nyikani mpaka mlipofika mahali hapa,  wala mambo aliyowatendea Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu mwana wa Rubeni, dunia ilipofunguka na kuwameza wao pamoja na familia zao na mahema yao na kila kiumbe aliye hai aliyewafuata, mbele ya macho ya Waisraeli wote.+  Macho yenu wenyewe yameona matendo yote makuu ambayo Yehova alifanya.  “Ni lazima mshike amri yote ninayowapa leo, ili muwe imara na kuvuka ili kuimiliki nchi,  na ili mwishi muda mrefu+ katika nchi ambayo Yehova aliapa kwamba angewapa mababu zenu na uzao wao,*+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 10  “Nchi mnayoenda kumiliki si kama nchi ya Misri mlikotoka, ambako mlikuwa mkipanda mbegu zenu na kuzimwagilia maji kwa mguu wenu,* kama bustani ya mboga. 11  Lakini nchi mnayokaribia kuvuka kuingia humo ili kuimiliki ni nchi yenye milima na mabonde tambarare.+ Inanyweshwa na maji ya mvua kutoka mbinguni;+ 12  ni nchi inayotunzwa na Yehova Mungu wenu. Macho ya Yehova Mungu wenu yanaitazama daima, kuanzia mwanzo wa mwaka mpaka mwisho wa mwaka. 13  “Na ikiwa mtatii kwa bidii amri zangu ninazowaamuru leo na kumpenda Yehova Mungu wenu na kumtumikia kwa moyo wenu wote na kwa nafsi* yenu yote,+ 14  nitawapa* pia mvua kwa ajili ya nchi yenu katika majira yake, mvua ya vuli na mvua ya masika, nanyi mtakusanya nafaka yenu na divai yenu mpya na mafuta yenu.+ 15  Nami nitaotesha majani katika mashamba yenu kwa ajili ya mifugo yenu, nanyi mtakula na kushiba.+ 16  Jihadharini msiruhusu mioyo yenu ishawishiwe kukengeuka na kuabudu miungu mingine na kuiinamia.+ 17  Kama sivyo, hasira ya Yehova itawaka dhidi yenu, naye atafunga mbingu hivi kwamba mvua haitanyesha+ na ardhi haitazaa mazao yake nanyi mtaangamia upesi kutoka katika nchi nzuri ambayo Yehova anawapa ninyi.+ 18  “Ni lazima uyakazie maneno haya yangu katika moyo wako na nafsi* yako na kuyafunga kama kumbukumbu kwenye mkono wako, nayo yanapaswa kuwa kama utepe kwenye paji la uso wako.*+ 19  Wafundishe watoto wako maneno haya, na kuongea kuyahusu unapoketi nyumbani mwako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.+ 20  Yaandike kwenye miimo ya milango ya nyumba yako na kwenye malango yako, 21  ili wewe na wana wako mwishi muda mrefu+ katika nchi ambayo Yehova aliapa kwamba angewapa mababu zenu,+ sikuzote ambazo mbingu zitakuwa juu ya dunia. 22  “Ikiwa mtaishika kabisa amri hii ninayowapa na kuitekeleza, mkimpenda Yehova Mungu wenu,+ mkitembea katika njia zake zote na kushikamana naye,+ 23  Yehova atayafukuza mataifa haya yote kutoka mbele yenu,+ nanyi mtamiliki nchi ya mataifa makubwa zaidi na yenye watu wengi kuliko ninyi.+ 24  Kila mahali mtakapokanyaga kwa mguu wenu patakuwa penu.+ Mpaka wenu utaanzia nyikani mpaka Lebanoni, kuanzia ule Mto, mto Efrati, mpaka bahari ya magharibi.*+ 25  Hakuna yeyote atakayewazuia.+ Yehova Mungu wenu atawafanya wakaaji wote wa nchi mtakayokanyaga wawahofu na kuwaogopa,+ kama alivyowaahidi ninyi. 26  “Tazameni, leo ninaweka mbele yenu baraka na laana:+ 27  baraka, ikiwa mtatii amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru ninyi leo,+ 28  na laana, ikiwa hamtatii amri za Yehova Mungu wenu+ na mkigeuka kutoka katika njia ninayowaamuru mfuate leo na mkifuata miungu mingine ambayo hamjaijua. 29  “Yehova Mungu wenu atakapowaleta katika nchi ambayo mtaimiliki, ni lazima mtangaze baraka kwenye Mlima Gerizimu na laana kwenye Mlima Ebali.+ 30  Je, haiko ng’ambo ya Yordani upande wa magharibi,* katika nchi ya Wakanaani wanaoishi Araba, mbele ya Gilgali, kando ya ile miti mikubwa ya More?+ 31  Kwa maana mnavuka Yordani mwingie na kuimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ninyi.+ Mtakapoimiliki na kuishi humo, 32  ni lazima muwe waangalifu kutekeleza masharti na sheria zote ninazoweka* mbele yenu leo.+

Maelezo ya Chini

Au “mpaka leo.”
Tnn., “mbegu yao.”
Yaani, kwa kutumia mfumo fulani uliokanyagwa kwa mguu, labda mfumo unaotumia gurudumu la maji au kwa kuchimba na kufungua mitaro ya maji kwa miguu.
Angalia Kamusi.
Yaani, Mungu.
Tnn., “katikati ya macho yako.”
Angalia Kamusi.
Yaani, ile Bahari Kuu, Mediterania.
Au “machweo ya jua.”
Tnn., “maamuzi yote ya hukumu ninayoweka.”