Kumbukumbu la Torati 12:1-32

  • Abuduni mahali ambapo Mungu amechagua (1-14)

  • Waruhusiwa kula nyama lakini si damu (15-28)

  • Msinaswe na miungu mingine (29-32)

12  “Haya ndiyo masharti na sheria ambazo mnapaswa kuwa waangalifu kutekeleza sikuzote mtakazokuwa hai katika nchi ambayo Yehova Mungu wa mababu zenu atawapa mwimiliki.  Mnapaswa kuharibu sehemu zote ambazo watu wa mataifa mtakaomiliki nchi yao wamekuwa wakiabudia miungu yao,+ iwe ni juu ya milima mirefu au kwenye vilima au chini ya mti wowote wenye majani mengi.  Mnapaswa kubomoa madhabahu zao, kuvunjavunja nguzo zao takatifu,+ kuteketeza kwa moto miti yao mitakatifu,* na kukatakata sanamu za kuchongwa za miungu yao,+ na kuondoa kabisa majina ya miungu yao kutoka sehemu hizo.+  “Hampaswi kumwabudu Yehova Mungu wenu kwa njia hiyo.+  Badala yake, mtafuteni Yehova Mungu wenu mahali popote atakapochagua kuweka jina lake na mahali atakapokaa miongoni mwa makabila yote, mwende mahali hapo.+  Hapo ndipo mnapopaswa kupeleka dhabihu zenu za kuteketezwa,+ matoleo yenu, sehemu zenu za kumi,+ mchango kutoka mkononi mwenu,+ dhabihu zenu za nadhiri, matoleo yenu ya hiari,+ na wazaliwa wa kwanza wa ng’ombe na kondoo wenu.+  Ni lazima ninyi na familia zenu mle hapo mbele za Yehova Mungu wenu+ na kushangilia katika kazi zenu zote,+ kwa sababu Yehova Mungu wenu amewabariki.  “Msifanye kama tunavyofanya hapa leo, kila mtu anafanya jambo analoona ni jema machoni pake mwenyewe,*  kwa sababu bado hamjafika mahali pa kupumzika+ na katika urithi ambao Yehova Mungu wenu atawapa. 10  Mtakapovuka Yordani+ na kuishi katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu atawapa ili mwimiliki, kwa hakika atawapumzisha kutokana na maadui wenu wote wanaowazunguka, nanyi mtakaa kwa usalama.+ 11  Mtaleta vitu vyote ninavyowaamuru mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua jina lake likae hapo+—dhabihu zenu za kuteketezwa, matoleo yenu, sehemu zenu za kumi,+ mchango kutoka mkononi mwenu, na kila dhabihu ya nadhiri mnayoweka nadhiri kwa Yehova. 12  Mtashangilia mbele za Yehova Mungu wenu,+ ninyi na wana wenu, binti zenu, watumwa wenu wa kiume na wa kike, na Mlawi yeyote aliye ndani ya majiji* yenu, kwa sababu hana fungu wala urithi pamoja nanyi.+ 13  Jihadharini msitoe dhabihu za kuteketezwa mahali pengine popote mtakapoona.+ 14  Mnapaswa kutoa dhabihu zenu za kuteketezwa mahali tu ambapo Yehova atachagua katika mojawapo ya maeneo ya makabila yenu, na huko ndiko mtakapofanya yote ninayowaamuru ninyi.+ 15  “Lakini wakati wowote mnapotamani nyama, mtamchinja mnyama na kula nyama yake+ kulingana na baraka ambayo Yehova Mungu wenu amewapa katika majiji* yenu yote. Mtu asiye safi na mtu aliye safi anaweza kula, kama mnavyokula swala au paa. 16  Lakini msile damu kamwe;+ mnapaswa kuimwaga ardhini kama maji.+ 17  Hamtaruhusiwa kula ndani ya majiji* yenu sehemu ya kumi ya nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu, wazaliwa wa kwanza wa ng’ombe na kondoo wenu,+ dhabihu yoyote mnayoweka nadhiri, matoleo yenu ya hiari, au mchango kutoka mkononi mwenu. 18  Mnapaswa kula vitu hivyo mbele za Yehova Mungu wenu mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua+—ninyi na wana wenu, mabinti wenu, watumishi wenu wa kiume na vijakazi wenu, na Mlawi yeyote aliye ndani ya majiji* yenu; nanyi mtashangilia mbele za Yehova Mungu wenu katika kazi zenu zote. 19  Jihadharini msimpuuze Mlawi+ yeyote sikuzote mtakazoishi katika nchi yenu. 20  “Yehova Mungu wenu atakapopanua eneo lenu,+ kama alivyowaahidi,+ nanyi mseme, ‘Nataka kula nyama,’ kwa sababu mnatamani* kula nyama, mnaweza kula nyama wakati wowote mnapotamani kuila.+ 21  Ikiwa mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua kuweka jina lake+ ni mbali kutoka kwenu, basi mnapaswa kuwachinja baadhi ya ng’ombe wenu au kondoo wenu ambao Yehova amewapa, kama nilivyowaamuru, nanyi mnapaswa kuwala ndani ya majiji* yenu wakati wowote mnapotamani nyama. 22  Mnaweza kuwala kama mnavyokula swala na paa;+ mtu asiye safi na mtu aliye safi anaweza kuila. 23  Ila tu mwazimie kwa uthabiti kutokula damu,+ kwa sababu damu ndiyo uhai,* nanyi hampaswi kula uhai*+ pamoja na nyama. 24  Msiile. Mnapaswa kuimwaga ardhini kama maji.+ 25  Msiile, ili mambo yawaendee vyema ninyi na watoto wenu baada yenu, kwa sababu mnafanya lililo sawa machoni pa Yehova. 26  Mnapaswa kuleta tu vitu vitakatifu ambavyo ni vyenu na dhabihu zenu za nadhiri mnapokuja mahali ambapo Yehova atachagua. 27  Mtatoa mahali hapo dhabihu zenu za kuteketezwa, nyama na damu,+ juu ya madhabahu ya Yehova Mungu wenu, na damu ya dhabihu zenu inapaswa kumwagwa kando ya madhabahu+ ya Yehova Mungu wenu, lakini mnaweza kula nyama. 28  “Muwe waangalifu kutii maneno haya yote ninayowaamuru ninyi, ili mambo yawaendee vyema sikuzote ninyi pamoja na wana wenu baada yenu, kwa sababu mnafanya mambo mema na yaliyo sawa machoni pa Yehova Mungu wenu. 29  “Yehova Mungu wenu atakapoyaangamiza mataifa ambayo mtamiliki nchi yao,+ na mtakapokuwa mkiishi katika nchi yao, 30  jihadharini msinaswe baada ya mataifa hayo kuangamizwa kutoka mbele yenu. Msiulize hivi kuhusu miungu yao: ‘Mataifa haya yaliabuduje miungu yake? Mimi pia nitafanya vivyo hivyo.’+ 31  Msimfanyie hivyo Yehova Mungu wenu, kwa sababu mataifa hayo yanaifanyia miungu yao kila jambo linalochukiza ambalo Yehova anachukia, hata kuwateketeza motoni wana na mabinti wao kwa ajili ya miungu yao.+ 32  Mnapaswa kutenda kwa uangalifu kila neno ninalowaamuru.+ Msiongeze wala kupunguza jambo lolote katika maneno hayo.+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “analofikiri linafaa.”
Tnn., “malango.”
Tnn., “ndani ya malango.”
Tnn., “malango.”
Tnn., “malango.”
Au “nafsi zenu zinatamani.”
Tnn., “malango.”
Au “nafsi.”
Au “nafsi.”