Kumbukumbu la Torati 17:1-20

  • Dhabihu zisiwe na kasoro (1)

  • Kushughulikia uasi imani (2-7)

  • Kuamua kesi ngumu (8-13)

  • Maagizo kwa ajili ya mfalme atakayetawala (14-20)

    • Mfalme aandike nakala ya Sheria (18)

17  “Usimtolee Yehova Mungu wako dhabihu ya ng’ombe dume au kondoo mwenye kasoro au mwenye tatizo lolote, kwa sababu jambo hilo litakuwa chukizo kwa Yehova Mungu wako.+  “Ikiwa mwanamume au mwanamke atapatikana miongoni mwenu, katika mojawapo ya majiji ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, aliye na mazoea ya kufanya uovu machoni pa Yehova Mungu wenu na kuvunja agano lake,+  naye anapotoka na kuabudu miungu mingine na kuiinamia miungu hiyo au jua au mwezi au jeshi lote la mbinguni,+ jambo ambalo sijaamuru,+  ukiambiwa au kusikia habari hiyo, unapaswa kuchunguza jambo hilo kikamili. Ikithibitishwa ni kweli+ kwamba jambo hilo lenye kuchukiza limefanywa katika Israeli,  utamtoa nje ya malango ya jiji lenu mwanamume au mwanamke ambaye amefanya uovu huo, na lazima mwanamume au mwanamke huyo auawe kwa kupigwa mawe.+  Kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au watatu+ yule anayepaswa kufa atauawa. Hapaswi kuuawa kwa ushahidi wa shahidi mmoja.+  Mikono ya mashahidi inapaswa kuwa ya kwanza kumuua, kisha mikono ya watu wengine wote. Ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+  “Ikiwa kesi ambayo ni ngumu sana kwenu kuamua inatokea katika mojawapo ya majiji yenu, iwe ni kesi ya kuua*+ au dai la kisheria limezushwa, au tendo la ukatili limefanywa, au mizozo mingine, mnapaswa kwenda mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua.+  Nendeni kwa makuhani Walawi na kwa mwamuzi+ anayehudumu wakati huo, muwapelekee mashtaka yenu, nao watafanya uamuzi.+ 10  Kisha mnapaswa kutenda kulingana na uamuzi watakaofanya mahali hapo palipochaguliwa na Yehova. Muwe waangalifu kufanya mambo yote wanayowaagiza. 11  Mnapaswa kutenda kulingana na sheria watakayowaonyesha na kulingana na uamuzi watakaowatangazia.+ Msigeuke na kuacha uamuzi watakaofanya, na kwenda kulia au kushoto.+ 12  Mtu anayetenda kwa kimbelembele kwa kukataa kumsikiliza kuhani anayemhudumia Yehova Mungu wenu au kukataa kumsikiliza mwamuzi ni lazima afe.+ Ni lazima mwondoe uovu katika Israeli.+ 13  Basi watu wote watasikia na kuogopa, nao hawatatenda tena kwa kimbelembele.+ 14  “Mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, mkaimiliki na kuishi humo, nanyi mseme, ‘Na tumweke mfalme juu yetu kama mataifa yote yanayotuzunguka,’+ 15  mnapaswa kumweka mfalme ambaye Yehova Mungu wenu atamchagua.+ Mnapaswa kumchagua mfalme kutoka miongoni mwa ndugu zenu. Hamruhusiwi kumweka mfalme ambaye ni mgeni, ambaye si ndugu yenu. 16  Hata hivyo, hapaswi kujipatia farasi wengi+ au kuwafanya watu warudi Misri kuchukua farasi wengi zaidi,+ kwa kuwa Yehova aliwaambia hivi: ‘Msirudi huko tena kamwe kupitia njia hii.’ 17  Wala hapaswi kuwa na wake wengi, ili moyo wake usipotoke;+ wala hapaswi kujipatia fedha na dhahabu nyingi sana.+ 18  Atakapoketi kwenye kiti cha ufalme wake, ni lazima ajiandikie kwenye kitabu* nakala ya Sheria hii, kwa kutumia nakala inayowekwa na makuhani Walawi.+ 19  “Anapaswa kubaki nacho, naye lazima akisome sikuzote za maisha yake,+ ili ajifunze kumwogopa Yehova Mungu wake na kushika maneno yote ya Sheria hii na masharti haya kwa kuyatekeleza.+ 20  Hivyo moyo wake hautajikweza juu ya ndugu zake, naye hataacha amri hiyo na kwenda kulia au kushoto, ili aendelee kutawala kwa muda mrefu katika ufalme wake, yeye na wanawe katika Israeli.

Maelezo ya Chini

Tnn., “kinywa cha.”
Tnn., “kumwaga damu.”
Au “hati ya kukunjwa.”