Kumbukumbu la Torati 19:1-21

  • Hatia ya damu na majiji ya makimbilio (1-13)

  • Alama za mipaka zisisogezwe (14)

  • Mashahidi mahakamani (15-21)

    • Mashahidi wawili au watatu wahitajika (15)

19  “Yehova Mungu wenu atakapoyaangamiza mataifa ambayo Yehova Mungu wenu anawapa nchi yao na mtakapokuwa mmemiliki nchi yao na kuishi katika majiji yao na nyumba zao,+  mnapaswa kutenga majiji matatu katikati ya nchi yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki.+  Mnapaswa kugawanya mara tatu eneo la nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki, nanyi mtengeneze barabara ili muuaji yeyote aweze kukimbilia katika mojawapo ya majiji hayo.  “Sasa hivi ndivyo itakavyokuwa kuhusu muuaji ambaye huenda akakimbilia humo ili kuokoa uhai wake: Akimuua jirani yake bila kukusudia naye hakuwa akimchukia;+  kwa mfano, anapoenda na jirani yake msituni kukusanya kuni, kisha anainua mkono wake ili akate mti kwa shoka, lakini shoka lichomoke kwenye mpini na kumgonga jirani yake na kumuua, muuaji huyo anapaswa kukimbilia katika mojawapo ya majiji hayo.+  Asipofanya hivyo, mtu anayelipiza kisasi cha damu+ anaweza kwa hasira kali kumkimbiza, kumkamata, na kumuua, kwa sababu jiji hilo lilikuwa mbali sana. Hata hivyo, hakustahili kufa kwa sababu hakuwa akimchukia jirani yake.+  Ndiyo sababu ninawaamuru hivi: ‘Tengeni majiji matatu.’  “Yehova Mungu wenu akipanua eneo lenu kama alivyowaapia mababu zenu+ na kuwapa nchi yote aliyoahidi kuwapa mababu zenu+  —maadamu mnashika kwa uaminifu amri hii yote ninayowapa leo, kwa kumpenda Yehova Mungu wenu na kutembea daima katika njia zake+—basi mtaongeza majiji mengine matatu zaidi ya hayo matatu.+ 10  Hivyo hakuna damu isiyo na hatia itakayomwagwa+ katika nchi yenu ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi, nanyi hamtakuwa na hatia yoyote ya damu.+ 11  “Lakini ikiwa mtu alikuwa akimchukia jirani yake,+ akamvizia, akamjeruhi vibaya sana na kumuua, na mtu huyo amekimbilia katika mojawapo ya majiji hayo, 12  basi wazee wa jiji lake wanapaswa kumwita kutoka humo na kumtia mikononi mwa yule anayelipiza kisasi cha damu, naye lazima afe.+ 13  Hampaswi kumhurumia,* nanyi lazima mwondoe hatia ya damu isiyo na hatia kutoka katika Israeli,+ ili mambo yawaendee vyema. 14  “Mtakapopokea urithi wenu katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki, hampaswi kusogeza alama ya mpaka+ wa jirani yenu kutoka mahali ambapo uliwekwa na mababu zenu. 15  “Shahidi mmoja hawezi kufanya mtu mwingine ahukumiwe kwa kosa lolote au dhambi yoyote ambayo huenda ametenda.+ Jambo hilo linapaswa kuthibitishwa kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au mashahidi watatu.+ 16  Shahidi mwenye nia ya kumdhuru mwingine akitoa ushahidi dhidi ya mtu na kumshtaki kwa kosa fulani,+ 17  watu hao wawili wanaozozana watasimama mbele za Yehova, mbele ya makuhani na waamuzi watakaokuwa wakihudumu wakati huo.+ 18  Waamuzi watachunguza jambo hilo kikamili,+ na ikiwa mtu huyo ni shahidi wa uwongo na ameleta shtaka la uwongo dhidi ya ndugu yake, 19  mnapaswa kumtendea kama alivyopanga kumtendea ndugu yake kwa hila,+ nanyi lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+ 20  Wale wanaobaki watasikia na kuogopa, nao hawatatenda tena kamwe uovu kama huo miongoni mwenu.+ 21  Hampaswi* kuwahurumia:+ Uhai utatolewa kwa uhai,* jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Jicho lenu lisimhurumie.”
Tnn., “kinywa cha.”
Tnn., “Jicho lenu halipaswi.”
Tnn., “Nafsi itatolewa kwa nafsi.”