Kumbukumbu la Torati 20:1-20

  • Sheria za vita (1-20)

    • Wale ambao hawakuruhusiwa kwenda vitani (5-9)

20  “Mkienda vitani kupigana na maadui wenu na kuona kwamba farasi wao na magari yao ya vita na wanajeshi wao ni wengi kuliko ninyi, msiwaogope, kwa maana Yehova Mungu wenu aliyewatoa nchini Misri yuko pamoja nanyi.+  Mnapokaribia kwenda vitani, kuhani anapaswa kuja na kuwahutubia watu.+  Anapaswa kuwaambia hivi: ‘Sikilizeni, enyi Waisraeli, hivi punde mtapigana na maadui wenu. Msife moyo. Msiogope wala msihofu wala kutetemeka kwa sababu yao,  kwa maana Yehova Mungu wenu anapiga mwendo pamoja nanyi ili awapiganie dhidi ya maadui wenu na kuwaokoa ninyi.’+  “Maofisa pia wanapaswa kuwaambia watu hivi: ‘Ni nani ambaye amejenga nyumba mpya lakini hajaizindua? Na arudi nyumbani kwake. La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine aizindue.  Na ni nani ambaye amepanda shamba la mizabibu na hajaanza kuvuna matunda yake? Na arudi nyumbani kwake. La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine akaanza kuvuna matunda yake.  Na ni nani ambaye amemchumbia mwanamke lakini hajamwoa? Na arudi nyumbani kwake.+ La sivyo, huenda akauawa vitani na mwanamume mwingine amwoe.’  Maofisa hao wanapaswa pia kuwauliza watu, ‘Ni nani anayeogopa na aliye na moyo dhaifu?+ Anapaswa kurudi nyumbani kwake, ili asiwafanye ndugu zake wavunjike moyo kama yeye.’*+  Baada ya maofisa hao kuzungumza na watu, wanapaswa kuwaweka wakuu wa majeshi ili wawaongoze watu. 10  “Mnapokaribia jiji ili kupigana nalo, mnapaswa kulitangazia pia masharti ya amani.+ 11  Jiji hilo likikubali kufanya amani pamoja nanyi na kuwafungulia malango yake, watu wote waliomo humo watakuwa wafanyakazi wenu wa kazi za kulazimishwa, nao watawatumikia.+ 12  Lakini likikataa kufanya amani pamoja nanyi na kupigana nanyi, mnapaswa kulizingira, 13  na kwa hakika Yehova Mungu wenu atalitia mikononi mwenu, nanyi mtamuua kwa upanga kila mwanamume aliye ndani ya jiji hilo. 14  Hata hivyo, mtajichukulia wanawake, watoto, mifugo, na kila kitu kilicho jijini, nyara zake zote,+ nanyi mtakula nyara za maadui wenu ambazo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi.+ 15  “Hivyo ndivyo mtakavyoyatendea majiji yote yaliyo mbali sana nanyi ambayo si majiji ya mataifa haya yaliyo karibu. 16  Lakini katika majiji ya mataifa haya, ambayo Yehova Mungu wenu anawapa yawe urithi wenu, hampaswi kuacha hai kitu chochote kinachopumua.+ 17  Mnapaswa kuwaangamiza kabisa, Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi,+ kama Yehova Mungu wenu alivyowaamuru; 18  ili wasiwafundishe kufuata mazoea yao yote yenye kuchukiza wanayofanyia miungu yao, na hivyo kuwafanya mumtendee dhambi Yehova Mungu wenu.+ 19  “Mkilizingira jiji na kuliteka baada ya kupigana nalo kwa siku nyingi, hampaswi kuharibu miti yake kwa kuikata ovyoovyo kwa shoka. Mnaweza kula matunda yake, lakini hampaswi kuikata.+ Je, mnapaswa kuushambulia mti kama mnavyomshambulia mwanadamu? 20  Mnaweza kuharibu tu mti ambao mnajua hautumiwi kwa chakula. Mnaweza kuukata na kuutumia kulizingira jiji linalopigana nanyi, mpaka litakapoanguka.

Maelezo ya Chini

Au “asifanye mioyo ya ndugu zake iyeyuke kama moyo wake mwenyewe.”