Kumbukumbu la Torati 21:1-23

  • Mauaji yaliyofanywa na watu wasiojulikana (1-9)

  • Kuoa wanawake mateka (10-14)

  • Haki ya mzaliwa wa kwanza (15-17)

  • Mwana mkaidi (18-21)

  • Mtu aliyetundikwa mtini amelaaniwa (22, 23)

21  “Mtu akipatikana ameuawa uwanjani katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki na haijulikani ni nani aliyemuua,  wazee na waamuzi+ wenu wanapaswa kwenda na kupima umbali kutoka kwenye maiti hiyo mpaka kwenye majiji yaliyo karibu nayo.  Kisha wazee wa jiji lililo karibu na maiti hiyo wanapaswa kuchukua kutoka kati ya mifugo ng’ombe mchanga ambaye hajawahi kutumiwa kufanya kazi, ambaye hajawahi kuvuta nira,  na wazee wa jiji hilo watampeleka ng’ombe huyo mchanga kwenye bonde* linalotiririka maji ambalo halijalimwa wala kupandwa mbegu, nao wanapaswa kumvunja shingo ng’ombe huyo mchanga humo bondeni.+  “Nao makuhani, Walawi, watakuja kwa sababu Yehova Mungu wenu amewachagua wamhudumie,+ watangaze baraka katika jina la Yehova.+ Watatangaza jinsi kila mzozo unaohusisha ukatili unavyopaswa kusuluhishwa.+  Kisha wazee wote wa jiji lililo karibu zaidi na maiti hiyo wanapaswa kunawa mikono yao+ juu ya ng’ombe huyo mchanga ambaye alivunjwa shingo bondeni,  nao wanapaswa kutangaza hivi: ‘Mikono yetu haikumwaga damu hii, wala macho yetu hayakuona ikimwagwa.  Usiwahesabie hatia hiyo watu wako Waisraeli, ambao uliwakomboa,+ Ee Yehova, nawe usiache hatia ya damu isiyo na lawama ibaki miongoni mwa watu wako Waisraeli.’+ Nao hawatakuwa na hatia hiyo ya damu.  Kwa njia hiyo mtaondoa hatia ya damu isiyo na lawama kutoka miongoni mwenu kwa kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova. 10  “Mkienda vitani kupigana na maadui wenu na Yehova Mungu wenu awasaidie kuwashinda, nanyi mwachukue mateka,+ 11  ukiona mwanamke mrembo miongoni mwa mateka hao na kuvutiwa naye, nawe utake kumchukua awe mke wako, 12  unaweza kumleta nyumbani mwako. Kisha atanyoa kichwa chake, atatunza kucha zake, 13  na kuvua nguo alizokuwa amevaa alipotekwa, naye ataishi nyumbani mwako. Atamlilia baba yake na mama yake kwa mwezi mzima,+ kisha unaweza kulala naye; utakuwa mume wake naye atakuwa mke wako. 14  Lakini ikiwa hupendezwi naye, unapaswa kumruhusu aende zake+ mahali popote anapotaka. Lakini huwezi kumuuza upate pesa au kumtesa, kwa kuwa umemwaibisha. 15  “Ikiwa mwanamume ana wake wawili, naye anampenda mmoja zaidi ya mwenzake* na wote wawili wamemzalia wana na mzaliwa wa kwanza ni wa mwanamke asiyependwa sana,+ 16  siku atakapowapa wanawe urithi wake, hataruhusiwa kumtendea mwana wa mwanamke anayependwa kana kwamba ndiye mzaliwa wake wa kwanza na kumpuuza mwana wa mwanamke asiyependwa sana, ambaye ndiye mzaliwa wa kwanza. 17  Anapaswa kumtambua mwana wa mwanamke asiyependwa sana kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kumpa maradufu ya kila kitu alicho nacho, kwa sababu mwana huyo ndiye mwanzo wa nguvu zake za uzazi. Haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake.+ 18  “Ikiwa mtu ana mwana ambaye ni mkaidi na mwasi na hamtii baba yake au mama yake,+ nao wamejaribu kumrekebisha lakini anakataa kuwasikiliza,+ 19  baba yake na mama yake wanapaswa kumshika na kumpeleka kwa wazee kwenye lango la jiji lake 20  na kuwaambia hivi wazee wa jiji lake: ‘Huyu mwana wetu ni mkaidi na mwasi, anakataa kututii. Ni mlafi+ na mlevi.’+ 21  Basi watu wote wa jiji lake watamuua kwa kumpiga mawe. Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu, na Waisraeli wote watasikia na kuogopa.+ 22  “Mtu akitenda dhambi inayostahili hukumu ya kifo, naye ameuawa,+ na mmemtundika mtini,+ 23  maiti yake isibaki mtini usiku kucha.+ Badala yake, mnapaswa kuhakikisha kwamba mnaizika siku hiyohiyo, kwa sababu mtu aliyetundikwa ni kitu kilicholaaniwa na Mungu,+ nanyi hampaswi kuichafua nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa iwe urithi wenu.+

Maelezo ya Chini

Au “korongo.”
Tnn., “wake wawili, mmoja anayependwa na mwingine anayechukiwa.”