Kumbukumbu la Torati 22:1-30

  • Kuheshimu wanyama wa jirani (1-4)

  • Kuvaa nguo za watu wa jinsia tofauti (5)

  • Kuwatendea wanyama kwa fadhili (6, 7)

  • Ukuta unaozunguka ukingo wa paa (8)

  • Michanganyiko isiyofaa (9-11)

  • Vishada vya nguo (12)

  • Sheria kuhusu kukiuka maadili ya ngono (13-30)

22  “Ukimwona ng’ombe dume wa ndugu yako au kondoo wake akipotea njia, usimpuuze kimakusudi.+ Unapaswa kumrudisha kwa ndugu yako.  Lakini ikiwa huyo ndugu yako haishi karibu nawe au humjui, unapaswa kumpeleka mnyama huyo nyumbani kwako, naye atakaa nawe mpaka ndugu yako atakapokuja kumtafuta. Kisha utamrudishia mnyama huyo.+  Unapaswa kufanya vivyo hivyo kuhusu punda wake, nguo zake, na kitu chochote utakachopata kilichopotezwa na ndugu yako. Hupaswi kukipuuza.  “Ukimwona punda wa ndugu yako au ng’ombe dume wake akianguka barabarani hupaswi kumpuuza kimakusudi. Unapaswa kumsaidia kumwinua mnyama huyo.+  “Mwanamke hapaswi kuvaa nguo za mwanamume, na mwanamume hapaswi kuvaa nguo za mwanamke. Kwa maana mtu yeyote anayefanya hivyo ni chukizo kwa Yehova Mungu wenu.  “Ukipata njiani kiota cha ndege chenye makinda au mayai, iwe mtini au kwenye ardhi, naye mama amefunika makinda au kuatamia mayai, usimchukue mama pamoja na makinda yake.+  Hakikisha umemfukuza mama yao, lakini unaweza kuchukua makinda. Fanya hivyo ili mambo yakuendee vyema na uishi muda mrefu.  “Ukijenga nyumba mpya, ni lazima pia ujenge ukuta kuzunguka ukingo wa paa lako,+ ili mtu asianguke kutoka kwenye paa nawe uiletee familia yako hatia ya damu.  “Usipande aina mbili za mbegu katika shamba lako la mizabibu.+ La sivyo, mazao yote utakayopata kutokana na mbegu hizo na pia zabibu zitakuwa za mahali patakatifu. 10  “Usilime kwa ng’ombe dume na punda pamoja.+ 11  “Usivae nguo zilizotengenezwa kwa kuchanganya sufu na kitani.+ 12  “Unapaswa kutengeneza vishada kwenye pembe nne za nguo unazovaa.+ 13  “Mwanamume akimchukua mke na kufanya ngono naye lakini baadaye amchukie* 14  na kudai kwamba ana mwenendo mbaya na kumharibia sifa kwa kusema, ‘Nilimchukua mwanamke huyu, lakini nilipofanya ngono naye sikupata uthibitisho wa kwamba yeye ni bikira,’ 15  baba na mama ya msichana huyo wanapaswa kuwapelekea wazee walio kwenye lango la jiji uthibitisho wa kwamba msichana huyo alikuwa bikira. 16  Baba ya msichana huyo atawaambia hivi wazee hao: ‘Nilimpa mwanamume huyu binti yangu awe mke wake, lakini anamchukia* 17  na anadai kwamba ana mwenendo mbaya kwa kusema, “Nimegundua kwamba binti yenu si bikira.” Sasa huu ndio uthibitisho wa ubikira wa binti yangu.’ Kisha watatandaza nguo hiyo mbele ya wazee wa jiji. 18  Wazee wa jiji+ watamchukua mwanamume huyo na kumtia nidhamu.+ 19  Watamtoza shekeli 100 za fedha na kumpa baba ya msichana huyo, kwa sababu mtu huyo alimharibia sifa bikira wa Israeli,+ naye ataendelea kuwa mke wake. Maadamu mwanamume huyo anaishi, hataruhusiwa kumtaliki msichana huyo. 20  “Hata hivyo, ikiwa madai hayo ni ya kweli na hakuna uthibitisho kwamba msichana huyo alikuwa bikira, 21  wanapaswa kumpeleka msichana huyo kwenye mlango wa nyumba ya baba yake, na wanaume wa jiji watamuua kwa kumpiga mawe, kwa sababu ametenda jambo la aibu+ katika Israeli kwa kufanya uasherati* katika nyumba ya baba yake.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu.+ 22  “Mwanamume akipatikana akifanya ngono na mke wa mwanamume mwingine, ni lazima wote wawili wauawe pamoja, mwanamume huyo pamoja na mwanamke aliyefanya naye ngono.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu katika Israeli. 23  “Ikiwa bikira amechumbiwa na mwanamume, kisha mwanamume mwingine akutane naye jijini na kufanya naye ngono, 24  mnapaswa kuwaleta wote wawili kwenye lango la jiji na kuwaua kwa kuwapiga mawe, mtamuua msichana huyo kwa sababu hakupiga mayowe jijini na mwanamume huyo kwa sababu alimwaibisha mke wa mwanamume mwenzake.+ Kwa hiyo ni lazima mwondoe uovu miongoni mwenu. 25  “Hata hivyo, ikiwa mwanamume huyo alimkuta uwanjani msichana huyo aliyechumbiwa na kumkamata kwa nguvu na kufanya naye ngono, mwanamume huyo aliyelala naye atauawa peke yake, 26  lakini msimtendee lolote msichana huyo. Msichana huyo hajatenda dhambi inayostahili kifo. Kisa chake ni sawa na cha mtu anayemshambulia mwenzake na kumuua.+ 27  Kwa maana mwanamume huyo alimkuta uwanjani, na msichana huyo aliyechumbiwa akapiga mayowe, lakini hakukuwa na mtu wa kumwokoa. 28  “Mwanamume akikutana na bikira ambaye hajachumbiwa kisha amkamate kwa nguvu na kufanya naye ngono, nao wagunduliwe,+ 29  mwanamume aliyefanya ngono na msichana huyo anapaswa kumpa baba ya msichana huyo shekeli 50 za fedha, naye atakuwa mke wake.+ Kwa sababu mwanamume huyo alimwaibisha, hataruhusiwa kumtaliki msichana huyo maisha yake yote. 30  “Hakuna mwanamume anayepaswa kumwoa* mke wa baba yake, ili asimwaibishe baba yake.*+

Maelezo ya Chini

Au “amkatae.”
Au “anamkataa.”
Au “ukahaba.”
Tnn., “kumchukua.”
Tnn., “asimfunue nguo baba yake.”