Kumbukumbu la Torati 24:1-22

  • Ndoa na talaka (1-5)

  • Kuheshimu uhai (6-9)

  • Kuwajali maskini (10-18)

  • Sheria kuhusu kuokota masalio (19-22)

24  “Mwanamume akimwoa mwanamke lakini hapendezwi naye kwa sababu ameona jambo fulani lisilofaa kwake, ni lazima amwandikie mwanamke huyo cheti cha talaka,+ ampe, na kumruhusu aondoke nyumbani mwake.+  Akiondoka katika nyumba hiyo, anaweza kwenda kuolewa na mwanamume mwingine.+  Mwanamume huyo wa pili akimchukia* na kumwandikia cheti cha talaka, kisha ampe na kumruhusu aondoke nyumbani mwake, au mwanamume huyo wa pili aliyemwoa akifa,  mume wake wa kwanza aliyemfukuza hataruhusiwa kumchukua tena awe mke wake baada ya mwanamke huyo kutiwa unajisi, kwa maana jambo hilo ni chukizo kwa Yehova. Hampaswi kuleta dhambi katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa kuwa urithi.  “Mwanamume aliyeoa karibuni hapaswi kutumikia jeshini wala kupewa majukumu mengine yoyote. Anapaswa kuwa huru kwa mwaka mmoja na kubaki nyumbani ili amfurahishe mke wake.+  “Hakuna mtu anayepaswa kuchukua jiwe la chini la kusagia au jiwe la juu kuwa dhamana kwa ajili ya mkopo,*+ kwa sababu kufanya hivyo ni sawa na kuchukua riziki ya* mtu kuwa dhamana.  “Ikiwa mtu atapatikana akiwa amemteka nyara ndugu yake Mwisraeli, naye amemtesa na kumuuza,+ mtekaji nyara huyo lazima auawe.+ Mnapaswa kuondoa uovu miongoni mwenu.+  “Ikiwa ugonjwa wa ukoma* umetokea na kuenea, muwe waangalifu sana kufanya mambo yote ambayo makuhani Walawi watawaagiza mfanye.+ Muwe waangalifu kufanya kama tu nilivyowaamuru.  Kumbukeni jinsi Yehova Mungu wenu alivyomtendea Miriamu mlipokuwa njiani kutoka Misri.+ 10  “Ukimkopesha jirani yako kitu chochote,+ hupaswi kuingia nyumbani mwake ili kuchukua kitu anachotoa kuwa dhamana. 11  Unapaswa kusimama nje, na mtu huyo uliyemkopesha anapaswa kukuletea nje kitu anachotoa kuwa dhamana. 12  Na ikiwa mtu huyo ni maskini, hupaswi kulala na kitu alichokupa kuwa dhamana.+ 13  Unapaswa kufanya yote uwezayo kumrudishia kitu alichokupa kuwa dhamana baada tu ya jua kutua, naye atakuwa na vazi lake anapoenda kulala,+ na atakubariki; nawe utakuwa mwadilifu mbele za Yehova Mungu wako. 14  “Usimlaghai kibarua mwenye uhitaji na maskini, awe ni mmoja wa ndugu zako au ni mkaaji mgeni katika nchi yenu, ndani ya majiji* yenu.+ 15  Unapaswa kumpa mshahara wake siku hiyohiyo,+ kabla ya jua kutua, kwa sababu ana uhitaji na uhai wake unategemea* mshahara wake. Usipofanya hivyo, atamlilia Yehova, nawe utakuwa na hatia ya dhambi.+ 16  “Akina baba hawapaswi kuuawa kwa sababu ya dhambi za wana wao, na wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya dhambi za baba zao.+ Mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.+ 17  “Usipotoshe hukumu ya mkaaji mgeni au ya yatima,+ nawe hupaswi kuchukua vazi la mjane kuwa dhamana ya mkopo.*+ 18  Kumbukeni kwamba mlikuwa watumwa nchini Misri, na Yehova Mungu wenu akawakomboa kutoka huko.+ Ndiyo sababu ninawaamuru mfanye hivyo. 19  “Unapovuna mavuno yako shambani na kusahau tita shambani, usirudi kulichukua. Linapaswa kuachwa kwa ajili ya mkaaji mgeni, yatima, na mjane,+ ili Yehova Mungu wako akubariki katika kila jambo unalofanya.+ 20  “Unapoupiga mzeituni ili kuangusha zeituni, hupaswi kurudia kufanya hivyo kwenye matawi yake. Matunda yanayobaki utamwachia mkaaji mgeni, yatima, na mjane.+ 21  “Unapokusanya zabibu katika shamba lako la mizabibu, hupaswi kurudi kukusanya zabibu zilizobaki. Unapaswa kumwachia mkaaji mgeni, yatima, na mjane. 22  Kumbukeni kwamba mlikuwa watumwa nchini Misri. Ndiyo sababu ninawaamuru mfanye hivyo.

Maelezo ya Chini

Au “akimkataa.”
Au “rehani.”
Au “kuchukua uhai wa; kuchukua nafsi ya.”
Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “ukoma” lina maana pana na linaweza kutia ndani magonjwa mbalimbali ya ngozi yanayoambukiza. Linaweza pia kutia ndani maambukizi fulani yaliyopatikana kwenye nguo na nyumba.
Tnn., “malango.”
Au “nafsi yake inategemea.”
Au “rehani.”