Kumbukumbu la Torati 28:1-68

  • Baraka za kutii (1-14)

  • Laana za kutotii (15-68)

28  “Nanyi kwa hakika mkiisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kuwa waangalifu kutenda amri zake zote ninazowaamuru leo, kwa hakika Yehova Mungu wenu atawakweza juu ya mataifa mengine yote ya dunia.+  Baraka hizi zote zitawajia na kuwatangulia,+ kwa sababu mnaendelea kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu:  “Mtabarikiwa jijini na mtabarikiwa shambani.+  “Watoto wenu*+ watabarikiwa na pia mazao ya ardhi yenu na watoto wa mifugo yenu, ng’ombe wenu wachanga na wanakondoo wenu.+  “Kikapu chenu+ na bakuli lenu la kukandia litabarikiwa.+  “Mtabarikiwa mnapoingia ndani, na mtabarikiwa mnapotoka nje.  “Yehova atafanya maadui wanaowashambulia washindwe mbele yenu.+ Watawashambulia kutoka upande mmoja, lakini watawakimbia wakielekea pande saba tofauti.+  Yehova atawaagizia baraka katika maghala yenu+ na katika kila kazi mnayofanya, na kwa hakika atawabariki katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa.  Yehova atawafanya kuwa taifa lake takatifu,+ kama alivyowaapia,+ kwa sababu mnaendelea kushika amri za Yehova Mungu wenu na kutembea katika njia zake. 10  Mataifa yote duniani yatalazimika kuona kwamba mmeitwa kwa jina la Yehova,+ nayo yatawaogopa ninyi.+ 11  “Yehova atawafanya muwe na watoto wengi sana na mifugo mingi sana na mazao mengi sana+ katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zenu kwamba atawapa ninyi.+ 12  Yehova atawafungulia ghala lake zuri, mbingu, ili mvua inyeshe juu ya nchi yenu katika majira yake+ na kubariki kila jambo mnalofanya. Mtayakopesha mataifa mengi, lakini ninyi wenyewe hamtahitaji kukopa.+ 13  Yehova atawafanya kuwa kichwa wala si mkia; nanyi mtakuwa juu+ wala si chini, mkiendelea kutii amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru leo mzishike na kuzitenda. 14  Msikengeuke kutoka katika maneno yote ninayowaamuru ninyi leo, na kwenda kulia au kushoto,+ kwa kufuata miungu mingine ili kuiabudu.+ 15  “Lakini msipoisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kuwa waangalifu kutenda amri zake zote na sheria zake ninazowaamuru leo, laana hizi zote zitawajia na kuwatangulia:+ 16  “Mtalaaniwa jijini na mtalaaniwa shambani.+ 17  “Kikapu chenu+ na bakuli lenu la kukandia+ vitalaaniwa. 18  “Watoto wenu*+ na mazao ya ardhi yenu na ng’ombe wenu wachanga na wanakondoo wenu watalaaniwa.+ 19  “Mtalaaniwa mnapoingia ndani na mtalaaniwa mnapotoka nje. 20  “Yehova atawaletea laana, vurugu na adhabu katika kila kazi mnayofanya mpaka mtakapoangamizwa na kutoweka upesi, kwa sababu ya mazoea yenu maovu na kuniacha mimi.+ 21  Yehova atafanya magonjwa yawaandame mpaka atakapokuwa amewaangamiza kutoka katika nchi mnayoenda kuimiliki.+ 22  Yehova atawapiga kwa kifua kikuu, homa kali,+ mwasho, joto la homa, upanga,+ upepo unaochoma, na kuvu;+ navyo vitawaandama mpaka mtakapoangamia. 23  Anga lililo juu ya vichwa vyenu litakuwa shaba, na dunia iliyo chini yenu itakuwa chuma.+ 24  Yehova atafanya mvua ya nchi yenu iwe ungaunga na mavumbi ambayo yatawanyeshea kutoka mbinguni mpaka mtakapoangamia kabisa. 25  Yehova atafanya mshindwe mbele ya maadui wenu.+ Mtawashambulia kutoka upande mmoja, lakini mtawakimbia mkielekea pande saba tofauti; nanyi mtakuwa kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia.+ 26  Na maiti zenu zitakuwa chakula kwa kila ndege wa angani na mnyama wa ardhini, na hakuna mtu atakayewafukuza.+ 27  “Yehova atawapiga kwa majipu ya Misri, bawasiri, ukurutu, na upele wa ngozi, nanyi hamtaweza kupona magonjwa hayo. 28  Yehova atawaletea kichaa na upofu+ na kuwafanya mchanganyikiwe.* 29  Mtapapasa-papasa wakati wa adhuhuri, kama kipofu anavyopapasa-papasa gizani,+ nanyi hamtafanikiwa katika jambo lolote mnalofanya; na watu watawalaghai na kuwanyang’anya vitu vyenu daima, na hakuna atakayewaokoa.+ 30  Utamchumbia mwanamke, lakini mwanamume mwingine atambaka. Utajenga nyumba, lakini hutaishi ndani yake.+ Utapanda shamba la mizabibu, lakini hutaanza kula matunda yake.+ 31  Ng’ombe dume wako atachinjwa mbele ya macho yako, lakini hutakula nyama yake. Punda wako ataibwa mbele ya macho yako, lakini hatarudishwa. Maadui wako watapewa kondoo wako, lakini hakuna atakayekusaidia. 32  Watu wengine watapewa wana wako na mabinti wako+ huku ukitazama, na sikuzote utatamani kuwaona, lakini mikono yako haitakuwa na nguvu za kufanya chochote. 33  Mavuno ya ardhi yako na mazao yako yote yataliwa na watu usiowajua,+ na sikuzote watu watawalaghai na kuwakandamiza. 34  Mtashikwa na kichaa kwa sababu ya mambo mtakayoona kwa macho yenu. 35  “Yehova atayapiga magoti yenu na miguu yenu kwa majipu yenye maumivu makali na yasiyopona, kuanzia nyayo za miguu yenu mpaka utosini. 36  Yehova atawapeleka ninyi na mfalme mliyemchagua awe juu yenu, kwenye taifa ambalo ninyi hamlijui wala mababu zenu hawakulijua,+ na huko mtaabudu miungu mingine, miungu ya miti na ya mawe.+ 37  Nanyi mtakuwa kitu cha kutisha na cha kudharauliwa,* na kitu cha kudhihakiwa miongoni mwa mataifa yote ambako Yehova atawapeleka.+ 38  “Mtapanda mbegu nyingi shambani, lakini mtavuna mazao machache,+ kwa sababu nzige watayala.⁠ 39  Mtapanda na kupalilia mashamba ya mizabibu, lakini hamtakunywa divai kamwe wala kukusanya zabibu zozote,+ kwa sababu kiwavi atazila. 40  Mtakuwa na mizeituni katika eneo lenu lote, lakini hamtajipaka mafuta yoyote, kwa sababu zeituni zenu zitaanguka. 41  Mtazaa wana na mabinti, lakini hawataendelea kuwa wenu, kwa sababu watapelekwa utekwani.+ 42  Makundi ya wadudu* yatavamia miti yenu yote na mazao ya ardhi yenu. 43  Mkaaji mgeni aliye miongoni mwenu ataendelea kupanda juu yenu zaidi na zaidi, huku ninyi mkiendelea kushuka chini zaidi na zaidi. 44  Atawakopesha, lakini ninyi hamtamkopesha.+ Atakuwa kichwa, lakini ninyi mtakuwa mkia.+ 45  “Laana hizi zote+ hakika zitawajia na kuwafuatia na kuwatangulia mpaka mtakapokuwa mmeangamizwa,+ kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kushika amri zake na sheria zake alizowaamuru.+ 46  Nazo zitaendelea kuwaandama ninyi na wazao wenu kama ishara na dalili ya kudumu,+ 47  kwa sababu hamkumtumikia Yehova Mungu wenu kwa furaha na shangwe moyoni mlipokuwa na wingi wa kila kitu.+ 48  Yehova atawatuma maadui wenu wawashambulie, nanyi mtawatumikia+ mkiwa na njaa+ na kiu na uchi na mkiwa maskini kabisa.* Ataweka nira ya chuma kwenye shingo zenu mpaka atakapokuwa amewaangamiza. 49  “Yehova ataleta dhidi yenu taifa la mbali,+ kutoka mwisho wa dunia; litawarukia kama tai,+ taifa ambalo hamtaelewa lugha yake,+ 50  taifa lenye uso mkali ambalo haliwajali wazee wala kuwahurumia vijana.+ 51  Watu hao watawala watoto wa mifugo yenu na mazao ya ardhi yenu mpaka mtakapokuwa mmeangamizwa. Hawatawaachia nafaka yoyote, divai mpya wala mafuta, ng’ombe mchanga wala mwanakondoo mpaka watakapokuwa wamewaangamiza.+ 52  Watawazingira na kuwafungia ndani ya majiji* yenu yote, katika nchi yenu yote, mpaka kuta zenu ndefu na zenye ngome mnazozitegemea zitakapoanguka. Naam, kwa hakika watawazingira katika majiji yenu yote, katika nchi yenu yote ambayo Yehova Mungu wenu amewapa ninyi.+ 53  Ndipo mtakapolazimika kuwala watoto wenu* wenyewe, nyama ya wana wenu na mabinti wenu+ ambao Yehova Mungu wenu amewapa, kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu. 54  “Hata mwanamume mpole sana na aliyedekezwa miongoni mwenu hatamhurumia ndugu yake au mke wake mpendwa au wanawe wanaobaki, 55  naye hatawagawia hata kidogo nyama ya wanawe ambayo atakula, kwa sababu hana kitu kingine chochote cha kula kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu katika majiji yenu.+ 56  Na mwanamke mpole sana na aliyedekezwa miongoni mwenu ambaye hata hawezi kuthubutu kukanyaga chini kwa wayo wa mguu wake kwa sababu ya kudekezwa sana+ hatamhurumia mume wake mpendwa wala mwanawe wala binti yake, 57  wala hata kondo la nyuma linalotoka katikati ya miguu yake wala wana anaozaa, kwa sababu atawala kwa siri kwa sababu ya kuzingirwa kabisa na kwa sababu ya mateso yatakayosababishwa na adui yenu katika majiji yenu. 58  “Ikiwa hamtashika kwa uangalifu maneno yote ya Sheria hii ambayo yameandikwa katika kitabu hiki+ na msipoliogopa jina hili tukufu na lenye kuogopesha,+ la Yehova+ Mungu wenu, 59  Yehova atawatesa ninyi na wazao wenu kwa mapigo makali sana, mapigo makubwa yanayodumu,+ na magonjwa hatari yanayodumu. 60  Atawaletea tena magonjwa yote ya Misri mliyokuwa mkiogopa, nayo kwa hakika yatawaandama ninyi. 61  Isitoshe, Yehova atawaletea pia kila ugonjwa au pigo ambalo halijaandikwa katika kitabu hiki cha Sheria mpaka mtakapoangamia. 62  Ingawa mmekuwa wengi sana kama nyota za mbinguni,+ ni wachache sana miongoni mwenu watakaobaki,+ kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu. 63  “Na kama Yehova alivyopendezwa wakati mmoja kuwafanikisha na kuwafanya mwongezeke, ndivyo Yehova atakavyopendezwa kuwaharibu na kuwaangamiza; nanyi mtang’olewa kutoka katika nchi mnayokaribia kuimiliki. 64  “Yehova atawatawanya miongoni mwa mataifa yote, kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho mwingine wa dunia,+ na huko mtalazimika kuabudu miungu ya miti na mawe, ambayo wala ninyi wala mababu zenu hamwijui.+ 65  Hamtakuwa na amani miongoni mwa mataifa hayo+ wala mahali pa kupumzisha wayo wa mguu wenu. Badala yake, mkiwa huko Yehova atawapa moyo wenye mahangaiko+ na macho yanayodhoofika na hisia za kukata tamaa.*+ 66  Uhai wenu utakabili hatari kubwa, nanyi mtaogopa usiku na mchana; nanyi hamtakuwa na uhakika wa kuokoka. 67  Asubuhi mtasema, ‘Laiti ingekuwa jioni!’ na jioni mtasema, ‘Laiti ingekuwa asubuhi!’ kwa sababu ya woga mtakaohisi mioyoni mwenu na kwa sababu ya mambo ambayo macho yenu yataona. 68  Na hakika Yehova atawarudisha Misri kwa meli, kupitia ile njia niliyowaambia hivi kuihusu: ‘Hamtaiona tena kamwe,’ na huko mtalazimika kujiuza kwa maadui wenu ili kuwa watumwa wa kiume na wa kike, lakini hakutakuwa na mtu wa kuwanunua.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “Wazao wa tumbo lenu.”
Tnn., “Wazao wa tumbo lenu.”
Au “mvurugike moyoni.”
Tnn., “methali.”
Au “Wadudu wanaoruka.”
Au “bila kitu chochote.”
Tnn., “malango.”
Tnn., “wazao wa tumbo lenu.”
Au “nafsi iliyokata tamaa.”