Kumbukumbu la Torati 34:1-12

  • Yehova amwonyesha Musa ile nchi (1-4)

  • Kifo cha Musa (5-12)

34  Kisha Musa akatoka katika jangwa tambarare la Moabu na kupanda Mlima Nebo,+ kwenye kilele cha Pisga,+ kinachoelekeana na Yeriko.+ Yehova akamwonyesha nchi yote, kuanzia Gileadi mpaka Dani,+  na nchi yote ya Naftali na nchi ya Efraimu na Manase, na nchi yote ya Yuda mpaka bahari ya magharibi,*+  na Negebu+ na ile Wilaya,+ bonde tambarare la Yeriko, jiji la mitende, mpaka Soari.+  Kisha Yehova akamwambia hivi: “Hii ndiyo nchi ambayo nilimwapia Abrahamu, Isaka, na Yakobo, niliposema, ‘Nitaupa uzao wako* nchi hii.’+ Nimekuruhusu uione kwa macho yako mwenyewe, lakini hutavuka kuingia humo.”+  Kisha Musa mtumishi wa Yehova akafa huko katika nchi ya Moabu kama Yehova alivyosema.+  Akamzika bondeni katika nchi ya Moabu, ng’ambo ya Beth-peori, na hakuna mtu anayejua kaburi lake liko wapi mpaka leo hii.+  Musa alikuwa na umri wa miaka 120 alipokufa.+ Macho yake hayakuwa yamedhoofika, na nguvu zake hazikuwa zimeisha.  Waisraeli walimlilia Musa katika jangwa tambarare la Moabu kwa siku 30.+ Kisha siku za kumlilia na kumwombolezea Musa zikaisha.  Yoshua mwana wa Nuni alikuwa amejaa roho ya hekima, kwa kuwa Musa alikuwa ameweka mkono wake juu yake;+ na Waisraeli wakaanza kumsikiliza, nao wakafanya kama Yehova alivyokuwa amemwamuru Musa.+ 10  Lakini hajatokea tena nabii mwingine katika Israeli aliye kama Musa,+ ambaye Yehova alimjua uso kwa uso.+ 11  Alifanya ishara zote na miujiza ambayo Yehova alimtuma afanye katika nchi ya Misri kwa Farao na watumishi wake wote na nchi yake yote,+ 12  pamoja na mkono wenye nguvu na nguvu zinazoogopesha ambazo Musa alidhihirisha machoni pa Waisraeli wote.+

Maelezo ya Chini

Yaani, ile Bahari Kuu, Mediterania.
Tnn., “Nitaipa mbegu yako.”