Kutoka 1:1-22

  • Waisraeli waongezeka Misri (1-7)

  • Farao awakandamiza Waisraeli (8-14)

  • Wakunga waliomwogopa Mungu hawakuwaua watoto (15-22)

1  Sasa haya ndiyo majina ya wana wa Israeli walioingia Misri pamoja na Yakobo, kila mwanamume aliyekuja na watu wa nyumba yake:+  Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda;+  Isakari, Zabuloni, na Benjamini;  Dani na Naftali; Gadi na Asheri.+  Na wazao wote wa Yakobo* walikuwa 70, lakini tayari Yosefu alikuwa Misri.+  Mwishowe Yosefu akafa,+ na pia ndugu zake wote na kizazi hicho chote.  Na Waisraeli* wakazaana na kuanza kuongezeka sana, nao wakazidi kuwa wengi na kuwa na nguvu isivyo kawaida, hivi kwamba wakajaa nchini.+  Baada ya muda mfalme mpya ambaye hakumjua Yosefu akaanza kutawala Misri.  Akawaambia watu wake: “Tazameni! Waisraeli ni wengi zaidi na wenye nguvu kuliko sisi.+ 10  Acheni tushughulike nao kwa akili. La sivyo, wataendelea kuongezeka, na vita vikitokea, wataungana na maadui wetu na kupigana nasi na kuondoka nchini.” 11  Basi wakaweka wasimamizi wa kazi za utumwa* ili wawatumikishe na kuwakandamiza kwa kazi ngumu,+ nao wakamjengea Farao majiji yenye maghala, yaani, Pithomu na Raamsesi.+ 12  Lakini kadiri walivyozidi kuwakandamiza, ndivyo walivyozidi kuongezeka na ndivyo walivyozidi kuenea kotekote, kwa hiyo wakaogopa sana na kuchukizwa na Waisraeli.+ 13  Kwa hiyo, Wamisri wakawalazimisha Waisraeli kuwa watumwa na kuwatesa kikatili.+ 14  Wakafanya maisha yao yawe machungu kwa kazi ngumu ya kutengeneza saruji ya udongo wa mfinyanzi na matofali na katika kila aina ya utumwa shambani. Naam, waliwalazimisha wafanye kazi ngumu chini ya hali ngumu sana katika kila aina ya utumwa.+ 15  Baadaye mfalme wa Misri akazungumza na wakunga Waebrania walioitwa Shifra na Pua, 16  akawaambia: “Mnapowasaidia wanawake Waebrania kuzaa,+ wanapokuwa kwenye kiti cha kuzalia, mnapaswa kumuua mtoto huyo ikiwa ni wa kiume; lakini ikiwa ni wa kike, mwacheni aishi.” 17  Hata hivyo, wakunga hao walimwogopa Mungu wa kweli, kwa hiyo hawakufanya kama walivyoambiwa na mfalme wa Misri. Badala yake, waliwaacha watoto wa kiume waishi.+ 18  Baada ya muda mfalme wa Misri akawaita wakunga hao na kuwauliza: “Kwa nini mmewaacha watoto wa kiume waishi?” 19  Wakunga hao wakamjibu Farao: “Wanawake Waebrania si kama wanawake Wamisri. Wana nguvu nao huzaa kabla mkunga hajafika.” 20  Kwa hiyo Mungu akawatendea mema wakunga hao, na Waisraeli wakazidi kuongezeka na kuwa wenye nguvu sana. 21  Na kwa sababu wakunga hao walimwogopa Mungu wa kweli, baadaye aliwapa familia. 22  Hatimaye Farao akawaamuru hivi watu wake wote: “Mnapaswa kumtupa kwenye Mto Nile kila mtoto mchanga wa kiume anayezaliwa na Waebrania, lakini mtamwacha hai kila mtoto wa kike.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Na wote waliotoka katika kiuno cha Yakobo.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “wasimamizi wa kazi.”