Kutoka 10:1-29

  • Pigo la 8: nzige (1-20)

  • Pigo la 9: giza (21-29)

10  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao, kwa sababu nimeacha moyo wake na mioyo ya watumishi wake iwe migumu,+ ili nifanye ishara hizi zangu mbele yake,+  na ili uwatangazie wanao na wajukuu wako jinsi nilivyoiadhibu vikali Misri na ishara nilizofanya miongoni mwenu;+ nanyi hakika mtajua kwamba mimi ni Yehova.”  Basi Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kumwambia: “Yehova Mungu wa Waebrania amesema hivi: ‘Utakataa mpaka lini kujinyenyekeza kwangu?+ Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie.  Kwa maana ukiendelea kukataa kuwaruhusu watu wangu waende zao, kesho nitaleta nzige ndani ya mipaka yenu.  Nao wataifunika ardhi yote, hivi kwamba hamtaweza kuiona ardhi. Watakula kabisa mimea ambayo haikuharibiwa na mvua ya mawe ambayo mlibaki nayo, nao watakula miti yenu yote inayomea shambani.+  Watajaa ndani ya nyumba zako, nyumba za watumishi wako wote, na nyumba zote za Misri, kwa kadiri ambayo baba zenu na mababu zenu hawajawahi kamwe kuona tangu walipozaliwa katika nchi hii mpaka leo.’”+ Kisha akageuka na kuondoka mbele ya Farao.  Ndipo watumishi wa Farao wakamwambia: “Mtu huyu ataendelea kututesa* mpaka lini? Waruhusu watu hawa waende zao wakamtumikie Yehova Mungu wao. Je, bado huoni kwamba Misri imeharibiwa?”  Kwa hiyo Musa na Haruni wakarudishwa kwa Farao, akawaambia: “Nendeni, mkamtumikie Yehova Mungu wenu. Lakini ni nani hasa watakaoenda?”  Musa akamjibu: “Tutaenda na vijana wetu, wazee wetu, wana wetu, mabinti wetu, kondoo wetu, na ng’ombe wetu,+ kwa maana tutamfanyia Yehova sherehe.”+ 10  Akawaambia: “Ikiwa nitawaruhusu ninyi na watoto wenu mwende, basi kwa kweli Yehova yuko pamoja nanyi!+ Ni wazi kwamba mnakusudia kutenda jambo fulani ovu. 11  Hapana! Ni wanaume wenu peke yao watakaoenda kumtumikia Yehova, kwa sababu hilo ndilo mliloomba.” Basi wakafukuzwa kutoka mbele ya Farao. 12  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya nchi ya Misri ili nzige waje juu ya nchi ya Misri na kula mimea yote nchini, kila kitu ambacho hakikuharibiwa na mvua ya mawe.” 13  Mara moja Musa akainyoosha fimbo yake juu ya nchi ya Misri, na Yehova akasababisha upepo wa mashariki uvume nchini mchana kutwa na usiku kucha. Asubuhi ilipofika, upepo huo wa mashariki ukaleta nzige. 14  Na nzige hao wakaja juu ya nchi yote ya Misri na kufunika eneo lote la Misri.+ Walikuwa wengi kupindukia;+ nzige wengi sana hivyo hawakuwa wamewahi kuonekana, wala nzige wengi sana hivyo hawangeonekana tena kamwe. 15  Waliifunika nchi yote, na nchi ikawa na giza kwa sababu yao; walitafuna mimea yote nchini na matunda yote mitini ambayo hayakuharibiwa na mvua ya mawe; hakuna majani yoyote yaliyobaki mitini wala kwenye mimea ya shambani katika nchi yote ya Misri. 16  Basi Farao akawaita haraka Musa na Haruni na kuwaambia: “Nimemtendea dhambi Yehova Mungu wenu na ninyi pia. 17  Sasa, tafadhali, mnisamehe dhambi yangu mara hii moja tu, na kumsihi Yehova Mungu wenu angalau aniondolee pigo hili hatari.” 18  Basi akaondoka* kwa Farao na kumsihi Yehova.+ 19  Kisha Yehova akasababisha upepo huo ubadili mkondo, nao ukawa upepo wenye nguvu sana wa magharibi, ukawapeperusha nzige hao na kuwapeleka katika Bahari Nyekundu. Hakuna nzige hata mmoja aliyebaki katika eneo lote la Misri. 20  Hata hivyo, Yehova aliuacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao. 21  Basi Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako kuelekea mbinguni ili giza liifunike nchi ya Misri, giza zito sana hivi kwamba linaweza kuguswa.” 22  Mara moja Musa akaunyoosha mkono wake kuelekea mbinguni, na giza zito sana likaifunika nchi yote ya Misri kwa siku tatu.+ 23  Hawakuonana, na kwa siku tatu hakuna yeyote kati yao aliyeondoka mahali alipokuwa; lakini Waisraeli wote walikuwa na mwangaza katika makao yao.+ 24  Kisha Farao akamwita Musa na kumwambia: “Nendeni, mkamtumikie Yehova.+ Ni kondoo wenu na ng’ombe wenu tu watakaobaki. Hata watoto wenu wanaweza kwenda nanyi.” 25  Lakini Musa akasema: “Wewe mwenyewe tupatie dhabihu na matoleo ya kuteketezwa, nasi tutazitoa kwa Yehova Mungu wetu.+ 26  Tutaenda pia na mifugo yetu. Hatutamwacha mnyama yeyote,* kwa sababu tutawatoa dhabihu baadhi ya wanyama hao tunapomwabudu Yehova Mungu wetu, na hatujui ni mnyama gani tutakayemtolea Yehova kuwa dhabihu mpaka tutakapofika huko.” 27  Kwa hiyo Yehova akauacha moyo wa Farao uwe mkaidi, naye hakukubali kuwaruhusu waende zao.+ 28  Farao akamwambia: “Ondoka mbele yangu! Usithubutu kuuona uso wangu tena, kwa maana siku utakapouona uso wangu, utakufa.” 29  Ndipo Musa akasema: “Na iwe kama ulivyosema, sitathubutu kuuona uso wako tena.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “kuwa mtego kwetu.”
Inaelekea ni Musa.
Tnn., “Hatutaacha ukwato wowote.”