Kutoka 12:1-51

  • Kuanzishwa kwa Pasaka (1-28)

    • Damu itanyunyizwa kwenye miimo ya mlango (7)

  • Pigo la 10: wazaliwa wa kwanza wauawa (29-32)

  • Safari ya Kutoka Misri yaanza (33-42)

    • Miaka 430 yafikia mwisho (40, 41)

  • Maagizo ya kushiriki Pasaka (43-51)

12  Sasa Yehova akawaambia Musa na Haruni katika nchi ya Misri:  “Mwezi huu utakuwa kwenu mwanzo wa miezi. Utakuwa mwezi wa kwanza wa mwaka kwenu.+  Liambieni kusanyiko lote la Waisraeli hivi: ‘Siku ya kumi ya mwezi huu, kila mmoja wao anapaswa kuchukua kondoo kwa ajili ya nyumba ya baba yake, kondoo+ mmoja kwa kila nyumba.  Lakini ikiwa familia ina watu wachache hivi kwamba hawawezi kummaliza kondoo mmoja, watagawana* na jirani yao wa karibu ndani ya nyumba yao kulingana na idadi ya watu.* Mnapofanya hesabu, kadirieni kiasi cha nyama ya kondoo kitakacholiwa na kila mtu.  Kondoo wenu anapaswa kuwa kondoo dume wa mwaka mmoja, asiye na kasoro.+ Mnaweza kuchagua mwanakondoo dume au mwanambuzi.  Mtamtunza mpaka siku ya 14 ya mwezi huu,+ na familia zote katika kusanyiko la Israeli zinapaswa kumchinja jioni kabla ya giza kuingia.*+  Watachukua kiasi fulani cha damu na kuinyunyiza kwenye miimo miwili ya mlango na kwenye kizingiti cha juu cha mlango wa nyumba ambamo watamla mnyama huyo.+  “‘Ni lazima waile nyama hiyo usiku huo.+ Wanapaswa kuichoma juu ya moto na kuila pamoja na mikate isiyo na chachu+ na mboga chungu za majani.+  Msile sehemu yoyote ya nyama hiyo ikiwa mbichi au ikiwa imechemshwa, yaani, ikiwa imepikwa kwa maji, lakini ichomeni juu ya moto, kichwa chake pamoja na miguu yake na viungo vyake vya ndani. 10  Hampaswi kuhifadhi sehemu yoyote ya nyama hiyo mpaka asubuhi, lakini sehemu yoyote itakayobaki mpaka asubuhi mnapaswa kuiteketeza kwa moto.+ 11  Na hivi ndivyo mnavyopaswa kuila, mkiwa mmejifunga mishipi,* mkiwa na viatu miguuni, na mkiwa na fimbo zenu mkononi; nanyi mnapaswa kuila haraka. Ni Pasaka ya Yehova. 12  Kwa maana nitapita katikati ya nchi ya Misri usiku huo na kumuua kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri, kuanzia mwanadamu mpaka mnyama;+ nami nitatekeleza hukumu dhidi ya miungu yote ya Misri.+ Mimi ni Yehova. 13  Ile damu itakuwa ishara inayoonyesha nyumba mtakazokuwamo; nami nitaiona damu hiyo na kupita juu yenu, na pigo halitawajia na kuwaangamiza ninyi nitakapoipiga nchi ya Misri.+ 14  “‘Siku hiyo itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mnapaswa kuisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote. Kwa kuwa ni sheria ya kudumu, mnapaswa kuisherehekea. 15  Kwa siku saba mtakula mikate isiyo na chachu.+ Naam, siku ya kwanza mtaondoa nyumbani mwenu unga uliokandwa wenye chachu, kwa sababu mtu yeyote atakayekula kitu kilichotiwa chachu kuanzia siku ya kwanza mpaka siku ya saba, ni lazima auawe kutoka katika Israeli. 16  Siku ya kwanza mtakuwa na kusanyiko takatifu, na siku ya saba, mtakuwa na kusanyiko lingine takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote siku hizo.+ Mtatayarisha tu chakula kitakacholiwa na kila mtu. 17  “‘Mtaadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ kwa sababu siku hiyo, nitayatoa makundi yenu makubwa* katika nchi ya Misri. Nanyi mnapaswa kuiadhimisha siku hiyo katika vizazi vyenu vyote kwa kuwa ni sheria ya kudumu. 18  Katika mwezi wa kwanza, siku ya 14 ya mwezi huo, jioni, mnapaswa kula mikate isiyo na chachu mpaka siku ya 21 ya mwezi huo, jioni.+ 19  Kwa siku saba, unga uliokandwa ambao umetiwa chachu usipatikane ndani ya nyumba zenu, kwa sababu yeyote akila kitu kilichotiwa chachu, awe ni mgeni au mwenyeji wa nchi,+ mtu huyo lazima auawe kutoka katika kusanyiko la Israeli.+ 20  Hampaswi kula kitu chochote kilichotiwa chachu. Mtakula mikate isiyo na chachu katika nyumba zenu zote.” 21  Musa akawaita wazee wote wa Israeli+ bila kukawia na kuwaambia: “Nendeni mkachague wanyama wachanga* kwa ajili ya kila moja ya familia zenu, nanyi mchinje dhabihu ya Pasaka. 22  Kisha mtachovya tita la majani ya hisopo katika damu iliyo ndani ya beseni na kupiga kizingiti cha juu cha mlango na miimo yake miwili kwa tita hilo lenye damu; na mtu yeyote kati yenu asitoke nje ya mlango wa nyumba yake mpaka asubuhi. 23  Kisha Yehova atakapopita ili kuwapiga Wamisri na kuiona damu kwenye kizingiti cha juu cha mlango na kwenye miimo yake miwili, kwa hakika Yehova atapita juu ya mlango wenu, naye hataruhusu pigo la kifo liingie* katika nyumba zenu.+ 24  “Mnapaswa kuadhimisha tukio hili kwa kuwa ni sheria ya kudumu kwenu na kwa wana wenu.+ 25  Nanyi mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova atawapa kama alivyoahidi, mnapaswa kuadhimisha tukio hilo.+ 26  Na wana wenu watakapowauliza, ‘Mwadhimisho huu una maana gani kwenu?’+ 27  mnapaswa kuwaambia, ‘Tunamtolea Yehova dhabihu ya Pasaka, ambaye alipita juu ya nyumba za Waisraeli nchini Misri alipowapiga Wamisri, lakini akaacha nyumba zetu.’” Kisha watu wakainama chini na kusujudu. 28  Basi Waisraeli wakaenda na kufanya kama Yehova alivyomwamuru Musa na Haruni.+ Hivyo ndivyo walivyofanya. 29  Ndipo katikati ya usiku, Yehova akamuua kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri,+ kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao aliyeketi kwenye kiti chake cha ufalme mpaka mzaliwa wa kwanza wa mateka aliyekuwa gerezani,* na kila mzaliwa wa kwanza wa mnyama.+ 30  Farao akaamka usiku huo pamoja na watumishi wake wote na Wamisri wengine wote, na kulikuwa na kilio kikubwa sana miongoni mwa Wamisri, kwa sababu hapakuwa na nyumba hata moja ambayo haikuwa na mtu aliyekufa.+ 31  Mara moja Farao akamwita Musa na Haruni+ usiku na kuwaambia: “Amkeni! Ondokeni kati ya watu wangu, ninyi wawili na Waisraeli wengine. Nendeni mkamtumikie Yehova, kama mlivyosema.+ 32  Chukueni pia kondoo wenu na ng’ombe wenu mwende zenu, kama mlivyosema.+ Lakini mnapaswa kunibariki pia.” 33  Na Wamisri wakaanza kuwahimiza Waisraeli waondoke haraka+ nchini “kwa sababu,” kama walivyosema, “sisi ni kama watu ambao tayari wamekufa!”+ 34  Basi Waisraeli wakachukua unga wao uliokandwa ambao haukuwa umetiwa chachu, pamoja na vyombo vyao vya* kukandia vikiwa vimefungwa katika nguo zao mabegani mwao. 35  Waisraeli walifanya kama Musa alivyokuwa amewaambia, wakawaomba Wamisri vito vya fedha na vya dhahabu na pia mavazi.+ 36  Yehova akawafanya Waisraeli wapate kibali machoni pa Wamisri, hivi kwamba wakawapa walichoomba, nao wakachukua mali za Wamisri.+ 37  Kisha Waisraeli wakaondoka Ramesesi+ kwenda Sukothi,+ wanaume wapatao 600,000 waliotembea kwa miguu, bila kuhesabu watoto.+ 38  Pia, kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu*+ lilienda pamoja nao, na vilevile kondoo na ng’ombe, naam, mifugo wengi sana. 39  Wakaanza kuoka mikate ya mviringo isiyo na chachu kwa kutumia unga uliokandwa waliobeba kutoka Misri. Haukuwa umetiwa chachu kwa sababu walifukuzwa ghafla kutoka Misri hivi kwamba hawakuwa wamejitayarishia chakula chochote.+ 40  Waisraeli walikuwa wameishi nchini Misri+ kwa miaka 430.+ 41  Mwishoni mwa miaka hiyo 430, siku hiyohiyo, makundi yote makubwa ya watu wa* Yehova yalitoka nchini Misri. 42  Wanapaswa kuadhimisha usiku huo kwa sababu Yehova aliwatoa nchini Misri. Watu wote wa Israeli katika vizazi vyao vyote wanapaswa kumheshimu Yehova kwa kuadhimisha usiku huo.+ 43  Kisha Yehova akawaambia Musa na Haruni, “Hii ndiyo sheria ya Pasaka: Hakuna mgeni anayepaswa kuila.+ 44  Lakini ikiwa mtu yeyote ana mtumwa wa kiume aliyenunuliwa kwa pesa, unapaswa kumtahiri.+ Ndipo mtumwa huyo atakaposhiriki kuila. 45  Mhamiaji na kibarua hawataila. 46  Italiwa ndani ya nyumba moja. Hampaswi kutoa nyama yoyote nje ya nyumba, nanyi hampaswi kuvunja mfupa wowote wa mnyama wa Pasaka.+ 47  Kusanyiko lote la Israeli litasherehekea Pasaka. 48  Ikiwa mgeni anaishi pamoja nawe, naye anataka kusherehekea Pasaka ya Yehova, ni lazima kila mwanamume wa familia yake atahiriwe. Kisha anaweza kukaribia ili kuisherehekea, naye atakuwa kama mwenyeji wa nchi. Lakini mwanamume yeyote ambaye hajatahiriwa hapaswi kuila Pasaka.+ 49  Sheria ileile itafuatwa na mwenyeji na mgeni anayeishi miongoni mwenu.”+ 50  Basi Waisraeli wote wakafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa na Haruni. Hivyo ndivyo walivyofanya. 51  Siku hiyohiyo, Yehova aliwatoa Waisraeli pamoja na makundi yao makubwa* kutoka katika nchi ya Misri.

Maelezo ya Chini

Tnn., “atagawana na jirani yake.”
Au “nafsi.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Tnn., “mkiwa mmevifunga viuno vyenu.”
Tnn., “majeshi yenu.”
Yaani, wanakondoo au wanambuzi.
Tnn., “maangamizi yaingie.”
Tnn., “katika nyumba ya tangi la maji.”
Au “mabakuli yao ya.”
Yaani, kundi kubwa lenye mchanganyiko wa watu ambao hawakuwa Waisraeli, kutia ndani Wamisri.
Tnn., “majeshi yote ya.”
Tnn., “majeshi yao.”