Kutoka 14:1-31

  • Waisraeli wafika baharini (1-4)

  • Farao awafuatia Waisraeli (5-14)

  • Waisraeli wavuka Bahari Nyekundu (15-25)

  • Wamisri wazama baharini (26-28)

  • Waisraeli wawa na imani katika Yehova (29-31)

14  Sasa Yehova akamwambia Musa:  “Waambie Waisraeli kwamba wanapaswa kurudi na kupiga kambi mbele ya Pihahirothi, kati ya Migdoli na bahari, mbele ya Baal-sefoni.+ Mtapiga kambi mbele yake kando ya bahari.  Kisha Farao atasema hivi kuhusu Waisraeli, ‘Wanatangatanga nchini kwa sababu wamechanganyikiwa. Wamepotea nyikani.’  Nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ naye atawafuatia, nami nitajipatia utukufu kupitia Farao na jeshi lake lote;+ na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova.”+ Basi Waisraeli wakafanya hivyo.  Baadaye mfalme wa Misri akajulishwa kwamba Waisraeli wamekimbia. Mara moja, Farao na watumishi wake wakabadili nia kuwahusu Waisraeli,+ wakasema: “Kwa nini tulifanya hivyo na kuwaruhusu Waisraeli waondoke, wasiwe watumwa wetu?”  Kwa hiyo akatayarisha magari yake ya vita, akaenda pamoja na watu wake.+  Akachukua magari 600 ya vita yaliyo bora na magari mengine yote ya vita nchini Misri, na kila gari lilikuwa na mashujaa.  Kwa hiyo Yehova akauacha moyo wa Farao mfalme wa Misri uwe mkaidi, naye akawafuatia Waisraeli, ambao walikuwa wakienda zao kwa ujasiri.*+  Wamisri wakawafuatia,+ na farasi wote wa magari ya vita ya Farao na askari wake wapanda farasi na jeshi lake lilikuwa likiwakaribia Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kando ya bahari, karibu na Pihahirothi, mbele ya Baal-sefoni. 10  Farao alipokaribia, Waisraeli waliinua macho yao na kuwaona Wamisri wakiwafuatia. Waisraeli wakaogopa sana na kuanza kumlilia Yehova.+ 11  Wakamwambia Musa: “Je, ni kwa sababu hakuna makaburi huko Misri ndiyo sababu umetuleta hapa tufie nyikani?+ Ni jambo gani hili ulilotutendea kwa kututoa Misri? 12  Je, hili silo jambo tulilokuambia nchini Misri tuliposema, ‘Achana nasi, ili tuwatumikie Wamisri’? Kwa maana ni afadhali kwetu kuwatumikia Wamisri kuliko kufia nyikani.”+ 13  Ndipo Musa akawaambia watu: “Msiogope.+ Simameni imara muone jinsi Yehova atakavyowaokoa leo.+ Kwa maana Wamisri mnaowaona leo, hamtawaona tena kamwe.+ 14  Yehova mwenyewe atawapigania ninyi,+ nanyi mtakaa kimya.” 15  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Kwa nini unaendelea kunililia? Waambie Waisraeli wavunje kambi. 16  Nawe inua fimbo yako na kuunyoosha mkono wako juu ya bahari na kuigawanya, ili Waisraeli wapite kwenye nchi kavu katikati ya bahari. 17  Nami ninaiacha mioyo ya Wamisri iwe mikaidi, ili waingie humo wakiwafuatia; kwa hiyo nitajipatia utukufu kupitia Farao na jeshi lake lote, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi.+ 18  Na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova nitakapojipatia utukufu kupitia Farao, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi.”+ 19  Ndipo malaika wa Mungu wa kweli+ aliyekuwa akitangulia kambi ya Waisraeli akaondoka na kurudi nyuma yao, nayo nguzo ya wingu iliyokuwa mbele yao ikarudi nyuma na kusimama nyuma yao.+ 20  Kwa hiyo ikaja kati ya kambi ya Wamisri na kambi ya Waisraeli.+ Upande mmoja, wingu hilo lilikuwa giza. Upande mwingine, uliangaza usiku.+ Hivyo, kambi ya Wamisri haikuikaribia kambi ya Waisraeli usiku kucha. 21  Sasa Musa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari;+ naye Yehova akaisukuma bahari nyuma usiku kucha kwa upepo wenye nguvu wa mashariki, maji yakagawanyika,+ kukawa na nchi kavu+ katikati ya bahari. 22  Kwa hiyo Waisraeli wakapita kwenye nchi kavu katikati ya bahari,+ huku maji yakisimama kama ukuta upande wao wa kulia na wa kushoto.+ 23  Wamisri wakawafuatia; farasi wote wa Farao, magari yake ya vita, na askari wake wapanda farasi wakaanza kuwafuatia katikati ya bahari.+ 24  Wakati wa kesha la asubuhi,* Yehova alitazama kambi ya Wamisri kutoka kwenye ile nguzo ya moto na wingu,+ naye akaivuruga kambi ya Wamisri. 25  Alikuwa akiyang’oa magurudumu ya magari yao ya vita hivi kwamba waliyaendesha kwa shida, na Wamisri walikuwa wakisema: “Na tuwakimbie Waisraeli tusiwakaribie kamwe, kwa sababu Yehova anawapigania dhidi ya Wamisri.”+ 26  Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya bahari ili maji yarudi na kuwafunika Wamisri, magari yao ya vita, na askari wao wapanda farasi.” 27  Mara moja Musa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari, na asubuhi ilipokuwa ikikaribia, bahari ikarudia hali yake ya kawaida. Wamisri walipokuwa wakiikimbia bahari, Yehova akawakung’uta Wamisri katikati ya bahari.+ 28  Maji yaliyokuwa yakirudi yalifunika magari ya vita na askari wapanda farasi na wanajeshi wote wa Farao waliokuwa wameingia baharini kuwafuatia.+ Hakuna hata mmoja wao aliyeokoka.+ 29  Lakini Waisraeli walitembea kwenye nchi kavu katikati ya bahari,+ na maji yalisimama kama ukuta upande wao wa kulia na wa kushoto.+ 30  Kwa hiyo Yehova akawaokoa Waisraeli siku hiyo kutoka mikononi mwa Wamisri,+ nao Waisraeli wakawaona Wamisri wakiwa wamekufa kwenye ufuo wa bahari. 31  Pia Waisraeli waliona nguvu nyingi ambazo* Yehova alidhihirisha dhidi ya Wamisri, basi watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova na Musa mtumishi wake.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “kwa mkono ulioinuliwa.”
Yaani, kuanzia saa 8 hivi usiku hadi saa 12 asubuhi.
Tnn., “mkono wenye nguvu ambao.”