Kutoka 16:1-36

  • Waisraeli wanung’unika kuhusu chakula (1-3)

  • Yehova asikia manung’uniko yao (4-12)

  • Wapewa mana na kware (13-21)

  • Hakuna mana siku ya Sabato (22-30)

  • Mana yahifadhiwa kuwa ukumbusho (31-36)

16  Baada ya kutoka Elimu, hatimaye kusanyiko lote la Waisraeli likafika katika nyika ya Sini,+ kati ya Elimu na Sinai, siku ya 15 ya mwezi wa pili baada ya kutoka katika nchi ya Misri.  Kisha kusanyiko lote la Waisraeli likaanza kuwanung’unikia Musa na Haruni nyikani.+  Waisraeli waliendelea kuwanung’unikia wakisema: “Laiti mkono wa Yehova ungetuua katika nchi ya Misri tulipokuwa tukiketi kando ya vyungu vya nyama,+ tulipokuwa tukila na kushiba mikate. Sasa mmetutoa huko na kutuleta katika nyika hii ili kuliua kusanyiko hili lote kwa njaa kali.”+  Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Tazama, ninawanyeshea mkate kutoka mbinguni,+ na kila mtu anapaswa kwenda kukusanya kiasi kinachomtosha siku baada ya siku,+ ili niwajaribu nione kama watafuata sheria yangu au la.+  Lakini siku ya sita+ wanapotayarisha kiasi walichokusanya, kinapaswa kuwa mara mbili ya kiasi wanachokusanya kila siku, siku nyinginezo.”+  Kwa hiyo Musa na Haruni wakawaambia Waisraeli wote: “Jioni mtajua kwa hakika kwamba Yehova ndiye aliyewatoa ninyi nchini Misri.+  Asubuhi mtauona utukufu wa Yehova, kwa sababu Yehova amesikia manung’uniko yenu dhidi yake. Sisi ni nani hivi kwamba mnung’unike dhidi yetu?”  Musa akaendelea kusema: “Yehova atakapowapa nyama ya kula jioni na mikate mtakayokula asubuhi na kushiba, mtajua kwamba Yehova amesikia manung’uniko yenu mnayonung’unika dhidi yake. Lakini sisi ni nani? Hamnung’uniki dhidi yetu, bali dhidi ya Yehova.”+  Kisha Musa akamwambia Haruni: “Liambie hivi kusanyiko lote la Waisraeli, ‘Karibieni mbele za Yehova, kwa maana amesikia manung’uniko yenu.’”+ 10  Mara tu Haruni alipomaliza kuzungumza na kusanyiko lote la Waisraeli, waligeuka na kutazama nyikani, na tazama! utukufu wa Yehova ukatokea katika lile wingu.+ 11  Yehova akaendelea kumwambia Musa: 12  “Nimesikia manung’uniko ya Waisraeli.+ Waambie hivi: ‘Jioni kabla ya giza kuingia* mtakula nyama, na asubuhi mtashiba mikate,+ nanyi mtajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu.’”+ 13  Basi jioni hiyo kware wakaja na kufunika kambi,+ na asubuhi utando wa umande ulizunguka kambi yote. 14  Utando huo wa umande ulipotoweka, kitu laini, kinachovunjikavunjika,+ kitu laini kama theluji, kilienea kwenye ardhi nyikani. 15  Waisraeli walipokiona, walianza kuulizana: “Ni nini hiki?” kwa maana hawakujua kilikuwa nini. Musa akawaambia: “Ni mkate ambao Yehova amewapa uwe chakula chenu.+ 16  Yehova ameamuru hivi: ‘Kila mtu anapaswa kukusanya kiasi anachoweza kula. Kila mmoja wenu atachukua kiasi cha omeri moja*+ kwa ajili ya kila mtu aliye katika hema lake.’” 17  Waisraeli wakaanza kukusanya; baadhi yao walikusanya zaidi na wengine wakakusanya kidogo. 18  Walipopima kwa omeri, yule aliyekusanya zaidi hakuwa na ziada na yule aliyekusanya kidogo hakupungukiwa.+ Kila mmoja alikusanya kiasi alichoweza kula. 19  Kisha Musa akawaambia: “Hakuna yeyote anayepaswa kuubakiza mkate huo mpaka asubuhi.”+ 20  Lakini hawakumsikiliza Musa. Baadhi yao walipoubakiza mpaka asubuhi, ulipata mabuu na kunuka, hivyo Musa akawakasirikia sana. 21  Waliuokota asubuhi baada ya asubuhi, kila mtu kulingana na kiasi alichoweza kula. Jua lilipokuwa kali, uliyeyuka. 22  Siku ya sita, waliokota kiasi mara mbili,+ vipimo viwili vya omeri kwa kila mtu. Kwa hiyo wakuu wote wa kusanyiko wakaja na kumwambia Musa jambo hilo. 23  Musa akawaambia: “Hivyo ndivyo alivyosema Yehova. Kesho kutakuwa na pumziko kamili,* sabato takatifu kwa Yehova.+ Okeni mnachohitaji kuoka, na chemsheni mnachohitaji kuchemsha;+ kisha chochote kitakachobaki mkihifadhi mpaka asubuhi.” 24  Basi wakakihifadhi mpaka asubuhi, kama Musa alivyowaamuru, nacho hakikunuka wala kuwa na mabuu. 25  Kisha Musa akasema: “Kuleni chakula hicho leo, kwa sababu leo ni sabato kwa Yehova. Leo hamtakipata kwenye ardhi. 26  Mtakiokota kwa siku sita, lakini siku ya saba ni Sabato,+ hakitakuwepo.” 27  Lakini baadhi ya watu walienda kukiokota siku ya saba, lakini hawakupata chochote. 28  Kwa hiyo Yehova akamwambia Musa: “Mtakataa kushika amri na sheria zangu mpaka lini?+ 29  Zingatieni kwamba mimi, Yehova, nimewapa Sabato.+ Ndiyo sababu katika siku ya sita ninawapa mkate wa siku mbili. Kila mtu anapaswa kukaa mahali alipo; hakuna yeyote anayepaswa kutoka kwake siku ya saba.” 30  Kwa hiyo watu wakaadhimisha Sabato* siku ya saba.+ 31  Watu wa nyumba ya Israeli waliuita mkate huo “mana.”* Ulikuwa mweupe kama mbegu za mgiligilani, na ladha yake ilikuwa kama ya keki bapa zenye asali.+ 32  Kisha Musa akasema: “Yehova ameamuru hivi: ‘Jazeni mkate huo katika kipimo cha omeri ili uwe kitu kitakachohifadhiwa katika vizazi vyenu vyote,+ ili watoto wenu waone mkate niliowapa mle nyikani nilipokuwa nikiwatoa katika nchi ya Misri.’” 33  Basi Musa akamwambia Haruni: “Chukua mtungi na kutia humo omeri moja ya mana, nawe uiweke mbele za Yehova ili iwe kitu kitakachohifadhiwa katika vizazi vyenu vyote.”+ 34  Haruni akafanya kama Yehova alivyomwamuru Musa, akaiweka mbele ya sanduku la Ushahidi*+ ili ihifadhiwe. 35  Waisraeli walikula mana kwa miaka 40,+ mpaka walipofika katika nchi iliyokaliwa na watu.+ Walikula mana mpaka walipofika mpakani mwa nchi ya Kanaani.+ 36  Sasa omeri ni sehemu ya kumi ya kipimo cha efa.*

Maelezo ya Chini

Tnn., “Katikati ya zile jioni mbili.”
Karibu lita 2.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “mwadhimisho wa sabato.”
Au “wakapumzika.”
Labda linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Ni nini hiki?”
Vitu muhimu vilihifadhiwa katika sanduku hili.
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.