Kutoka 18:1-27

  • Yethro na Sipora wawasili (1-12)

  • Ushauri wa Yethro wa kuwaweka waamuzi (13-27)

18  Sasa Yethro kuhani wa Midiani, baba mkwe wa Musa,+ akasikia mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemtendea Musa na watu wake Waisraeli, jinsi Yehova alivyowatoa Waisraeli nchini Misri.+  Yethro, baba mkwe wa Musa, alikuwa amemchukua Sipora mke wa Musa ili amtunze, Sipora aliporudishwa  pamoja na wanawe wawili.+ Mwana mmoja aliitwa Gershomu,*+ kwa sababu Musa alisema, “Nimekuwa mkaaji mgeni katika nchi ya kigeni,”  na yule mwingine aliitwa Eliezeri,* kwa sababu Musa alisema, “Mungu wa baba yangu ni msaidizi wangu, aliyeniokoa kutokana na upanga wa Farao.”+  Basi Yethro, baba mkwe wa Musa, pamoja na wana na mke wa Musa, wakaja kwa Musa nyikani ambako alikuwa amepiga kambi karibu na mlima wa Mungu wa kweli.+  Kisha akatuma ujumbe huu kwa Musa: “Mimi, Yethro, baba mkwe wako,+ naja kwako pamoja na mke wako na wanawe wawili.”  Mara moja Musa akaenda kumpokea baba mkwe wake, akainama chini na kumbusu. Wakajuliana hali, kisha wakaingia hemani.  Musa akamsimulia baba mkwe wake mambo yote ambayo Yehova alikuwa amemtendea Farao na Wamisri kwa ajili ya Waisraeli,+ matatizo yote waliyopata safarini,+ na jinsi Yehova alivyowaokoa.  Yethro akashangilia kwa sababu ya mambo yote mema ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli kwa kuwaokoa kutoka Misri.* 10  Kisha Yethro akasema: “Yehova na asifiwe, aliyekuokoa kutoka Misri na kutoka kwa Farao, na kuwaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa Wamisri. 11  Sasa ninajua kwamba Yehova ni mkuu kuliko miungu mingine yote,+ kwa sababu ya mambo aliyowafanyia wale waliowatendea watu wake kwa kiburi.” 12  Kisha Yethro, baba mkwe wa Musa, akaleta dhabihu ya kuteketezwa na matoleo kwa ajili ya Mungu, na Haruni na wazee wote wa Israeli wakaja kula chakula pamoja na baba mkwe wa Musa, mbele za Mungu wa kweli. 13  Siku iliyofuata, Musa akaketi kama kawaida ili kusikiliza kesi za watu, na watu wakaendelea kuja na kusimama mbele ya Musa tangu asubuhi mpaka jioni. 14  Baba mkwe wake alipoona mambo yote ambayo Musa alikuwa akiwafanyia watu, akamuuliza: “Ni nini hiki unachowafanyia watu? Kwa nini unaketi hapa peke yako huku watu wote wakisimama mbele yako tangu asubuhi mpaka jioni?” 15  Musa akamwambia baba mkwe wake: “Ni kwa sababu watu wanaendelea kuja kwangu kutafuta mwongozo kutoka kwa Mungu. 16  Wakiwa na kesi, wanaileta kwangu, nami lazima niamue kesi yao, na kuwajulisha maamuzi ya Mungu wa kweli na sheria zake.”+ 17  Baba mkwe wa Musa akamwambia: “Jambo unalofanya si zuri. 18  Kwa hakika utachoka, wewe na watu hawa walio pamoja nawe, kwa sababu mzigo huu ni mkubwa sana kwako na huwezi kuubeba peke yako. 19  Sasa nisikilize. Nitakupa ushauri, na Mungu atakuwa pamoja nawe.+ Wewe uwe mwakilishi wa watu mbele za Mungu wa kweli,+ nawe lazima uwasilishe kesi zao mbele za Mungu wa kweli.+ 20  Unapaswa kuwaonya kwa kuwafundisha masharti na sheria,+ na uwajulishe njia wanayopaswa kufuata na kazi wanayopaswa kufanya. 21  Lakini unapaswa kuchagua miongoni mwa watu, wanaume wanaostahili,+ wanaomwogopa Mungu, wanaume wanaotegemeka, wanaochukia faida isiyo ya haki,+ nawe uwaweke kuwa wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, na wakuu wa makumi.+ 22  Watakuwa waamuzi wa watu kunapokuwa na kesi,* nao watakuletea kila kesi iliyo ngumu,+ lakini wao wataamua kila kesi ambayo ni ndogo. Jirahisishie mzigo huu kwa kuwaruhusu wakusaidie kuubeba.+ 23  Ukifanya hivyo, na iwe ndivyo Mungu anavyokuamuru, utaweza kustahimili mkazo huu, na kila mtu atarudi nyumbani akiwa ameridhika.” 24  Mara moja Musa akamsikiliza baba mkwe wake na kufanya yote aliyosema. 25  Musa akachagua wanaume wanaostahili miongoni mwa Waisraeli wote na kuwaweka kuwa viongozi wa watu, kuwa wakuu wa maelfu, wakuu wa mamia, wakuu wa hamsini, na wakuu wa makumi. 26  Kwa hiyo waliamua kesi walizoletewa na watu. Kesi ngumu walimletea Musa,+ lakini waliamua kila kesi ndogo. 27  Kisha Musa akamuaga baba mkwe wake,+ naye baba mkwe wake akashika njia na kurudi katika nchi yake.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Mkaaji Mgeni Huko.”
Maana yake “Mungu Wangu Ni Msaidizi.”
Tnn., “kutoka mkononi mwa Misri.”
Tnn., “kila wakati.”