Kutoka 19:1-25

  • Kwenye Mlima Sinai (1-25)

    • Waisraeli watakuwa ufalme wa makuhani (5, 6)

    • Watu watakaswa ili wakutane na Mungu (14, 15)

19  Katika mwezi wa tatu baada ya Waisraeli kutoka nchini Misri, siku ileile, walifika katika nyika ya Sinai.  Waliondoka Refidimu+ wakafika katika nyika ya Sinai na kupiga kambi nyikani. Waisraeli walipiga kambi huko mbele ya mlima.+  Kisha Musa akapanda mlimani kwa Mungu wa kweli, naye Yehova akamwita kutoka mlimani,+ akamwambia: “Hivi ndivyo utakavyoiambia nyumba ya Yakobo na kuwaambia Waisraeli,  ‘Mmejionea wenyewe mambo niliyowatendea Wamisri,+ ili niwabebe juu ya mabawa ya tai na kuwaleta kwangu.+  Sasa ikiwa mtaitii kabisa sauti yangu na kushika agano langu, hakika mtakuwa mali yangu ya pekee* kati ya mataifa yote,+ kwa maana dunia yote ni mali yangu.+  Mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’+ Hayo ndiyo maneno utakayowaambia Waisraeli.”  Basi Musa akaenda na kuwaita wazee wote wa Waisraeli na kuwaambia maneno hayo yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru.+  Kisha watu wote wakasema pamoja: “Mambo yote ambayo Yehova amesema, tuko tayari kufanya.”+ Mara moja Musa akamwambia Yehova maneno hayo ambayo watu walisema.  Na Yehova akamwambia Musa: “Tazama! nitakujia katika wingu lenye giza, ili watu wasikie ninapozungumza nawe na ili wakuamini wewe pia sikuzote.” Kisha Musa akamwambia Yehova maneno ambayo watu walisema. 10  Halafu Yehova akamwambia Musa: “Nenda uwatakase watu leo na kesho, nao lazima wafue nguo zao. 11  Nao lazima wawe tayari kwa ajili ya siku ya tatu, kwa sababu katika siku ya tatu mimi Yehova nitashuka juu ya Mlima Sinai mbele ya watu wote. 12  Ni lazima uwawekee watu mipaka kuzunguka mlima huu na uwaambie, ‘Jihadharini msipande mlimani wala kugusa ukingo wake. Yeyote atakayeugusa mlima huu hakika atauawa. 13  Mkono wa yeyote usimguse, atapigwa mawe au kuchomwa kwa silaha.* Awe ni mnyama au mwanadamu, hataishi.’+ Lakini pembe ya kondoo dume+ ikipigwa watu wanaweza kuukaribia mlima.” 14  Kisha Musa akashuka kutoka mlimani, akaenda kwa watu, akaanza kuwatakasa, nao wakafua nguo zao.+ 15  Akawaambia: “Jitayarisheni kwa ajili ya siku ya tatu. Msifanye ngono.”* 16  Asubuhi, siku ya tatu, kulikuwa na ngurumo na radi, na kulikuwa na wingu zito+ mlimani na sauti kubwa sana ya pembe, na watu wote kambini wakaanza kutetemeka.+ 17  Sasa Musa akawatoa watu nje ya kambi ili wakutane na Mungu wa kweli, nao wakasimama mahali pao chini ya mlima. 18  Mlima Sinai ulifuka moshi kila mahali, kwa sababu Yehova alishuka juu yake katika moto;+ na moshi huo ulikuwa ukipaa kama moshi wa tanuru,* na mlima wote ulikuwa ukitetemeka kwa nguvu sana.+ 19  Sauti ya pembe ilipozidi kuongezeka zaidi na zaidi, Musa akaongea, na sauti ya Mungu wa kweli ikamjibu. 20  Kwa hiyo Yehova akashuka juu ya kilele cha Mlima Sinai. Kisha Yehova akamwita Musa apande juu mlimani, naye Musa akapanda mlimani.+ 21  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Shuka chini ukawaonye watu wasijaribu kuvuka mpaka kuja kunitazama mimi, Yehova, la sivyo wengi wao wataangamia. 22  Nao makuhani wanaonikaribia mimi Yehova kwa ukawaida, wanapaswa kujitakasa, ili mimi, Yehova, nisiwaangamize.”+ 23  Basi Musa akamwambia Yehova: “Watu hawawezi kuukaribia Mlima Sinai kwa sababu tayari ulituonya, uliponiambia, ‘Weka mipaka kuzunguka mlima huu, ili uwe mtakatifu.’”+ 24  Hata hivyo, Yehova akamwambia: “Nenda, shuka chini, na urudi juu, wewe pamoja na Haruni, lakini usiwaruhusu makuhani na watu wavuke mpaka na kunikaribia mimi Yehova, ili nisiwaangamize.”+ 25  Basi Musa akashuka na kuwaambia watu maneno hayo.

Maelezo ya Chini

Au “mali yangu ninayothamini sana.”
Labda angechomwa kwa mkuki.
Tnn., “Msimkaribie mwanamke.”
Au “kalibu.”