Kutoka 2:1-25

  • Musa azaliwa (1-4)

  • Binti ya Farao amchukua Musa kuwa mwanawe (5-10)

  • Musa akimbilia Midiani na kumwoa Sipora (11-22)

  • Mungu asikia kilio cha uchungu cha Waisraeli (23-25)

2  Karibu na wakati huo, mwanamume fulani wa nyumba ya Lawi alimwoa binti ya Lawi.+  Mwanamke huyo akapata mimba na kuzaa mwana. Alipoona kwamba mwana huyo ana sura yenye kupendeza sana, alimficha kwa miezi mitatu.+  Aliposhindwa kuendelea kumficha,+ alichukua kikapu cha mafunjo* na kukipaka lami na bereu, akamweka mtoto huyo ndani yake na kukiweka kati ya matete kando ya Mto Nile.  Lakini dada ya mtoto huyo+ akasimama mbali kidogo ili aone yatakayompata ndugu yake.  Binti ya Farao aliposhuka kwenye Mto Nile ili kuoga, watumishi wake wa kike walikuwa wakitembeatembea kando ya Mto Nile. Binti ya Farao akaona kikapu hicho kati ya matete. Mara moja akamtuma kijakazi wake akilete.+  Alipokifungua, alimwona mwana huyo akilia. Akamhurumia, lakini akasema: “Huyu ni mtoto wa Waebrania.”  Kisha dada ya mtoto huyo akamuuliza binti ya Farao: “Je, niende nikamwite mwanamke mlezi Mwebrania akunyonyeshee mtoto huyu?”  Binti ya Farao akamwambia: “Nenda!” Msichana huyo akaenda mara moja na kumwita mama ya mtoto huyo.+  Kisha binti ya Farao akamwambia: “Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, nami nitakulipa.” Basi mwanamke huyo akamchukua na kumnyonyesha. 10  Mtoto huyo alipokuwa mkubwa kidogo, akamleta kwa binti ya Farao, naye akawa mwanawe.+ Akampa jina Musa* na kusema: “Ni kwa sababu nimemtoa katika maji.”+ 11  Siku hizo, baada ya Musa kuwa mtu mzima,* alitoka kwenda kwa ndugu zake ili kuona mizigo waliyokuwa wakibeba,+ akamwona Mmisri akimpiga Mwebrania, mmoja wa ndugu zake. 12  Kwa hiyo Musa akatazama huku na kule, na alipoona kwamba hakuna yeyote, akamuua Mmisri huyo na kumficha mchangani.+ 13  Lakini Musa alitoka siku iliyofuata, akawaona wanaume wawili Waebrania wakipigana. Basi akamuuliza yule aliyekosea: “Kwa nini unampiga mwenzako?”+ 14  Akasema: “Ni nani aliyekuweka kuwa mkuu na mwamuzi wetu? Je, unapanga kuniua kama ulivyomuua yule Mmisri?”+ Basi Musa akaogopa na kusema moyoni: “Bila shaka jambo hilo limejulikana!” 15  Kisha Farao akasikia habari hizo, naye akajaribu kumuua Musa; lakini Musa akamkimbia Farao na kwenda kuishi katika nchi ya Midiani;+ alipofika huko akaketi kando ya kisima. 16  Sasa kuhani wa Midiani+ alikuwa na mabinti saba, nao wakaja kuteka maji na kujaza vyombo vya kunyweshea kondoo wa baba yao. 17  Lakini kama kawaida, wachungaji walikuja na kuwafukuza mabinti hao. Kwa hiyo Musa akainuka, akawasaidia* wanawake hao, na kuwanywesha kondoo wao. 18  Walipofika nyumbani kwa Reueli*+ baba yao, akawauliza kwa mshangao: “Mbona mmerudi upesi sana leo?” 19  Wakamjibu: “Mmisri fulani+ alituokoa kutoka mikononi mwa wachungaji, na hata alitutekea maji na kuwanywesha kondoo.” 20  Reueli akawaambia mabinti zake: “Lakini yuko wapi? Kwa nini hamkuja naye? Mwiteni, ili ale chakula pamoja nasi.” 21  Baada ya hayo Musa akakubali kuishi na mtu huyo, naye akampa Musa binti yake aliyeitwa Sipora+ ili amwoe. 22  Baadaye Sipora akazaa mwana, naye Musa akamwita mwana huyo Gershomu,*+ kwa sababu alisema: “Nimekuwa mkaaji mgeni katika nchi ya kigeni.”+ 23  Baada ya muda mrefu,* mfalme wa Misri akafa,+ lakini Waisraeli wakaendelea kulia kwa uchungu kwa sababu ya utumwa na kupaza kilio cha malalamishi, na kilio chao cha kuomba msaada kwa sababu ya utumwa kikaendelea kupanda juu kwa Mungu wa kweli.+ 24  Mwishowe Mungu akasikia kilio chao cha uchungu,+ naye akakumbuka agano lake alilofanya na Abrahamu, Isaka, na Yakobo.+ 25  Basi Mungu akawakazia uangalifu Waisraeli; na Mungu akayaona mateso yao.

Maelezo ya Chini

Au “safina; sanduku.”
Maana yake “Aliyetolewa,” yaani, aliyeokolewa kutoka katika maji.
Au “Musa alipokuwa akipata nguvu.”
Au “akawatetea.”
Yaani, Yethro.
Maana yake “Mkaaji Mgeni Huko.”
Tnn., “siku nyingi.”