Kutoka 21:1-36

  • Waisraeli wapewa sheria (1-36)

    • Kuhusu watumwa Waebrania (2-11)

    • Kuhusu kumtendea mtu mwingine kwa ukatili (12-27)

    • Kuhusu wanyama (28-36)

21  “Hizi ndizo sheria utakazowapa* Waisraeli:+  “Ukimnunua mtumwa Mwebrania,+ atakuwa mtumwa kwa miaka sita, lakini mwaka wa saba, utamweka huru, naye hatalipa chochote.+  Ikiwa alikuja peke yake, ataondoka peke yake. Ikiwa ana mke, basi mke wake anapaswa kuondoka naye.  Ikiwa bwana wake atampa mke, na mke huyo amzalie wana au mabinti, mke huyo na watoto wake watakuwa mali ya bwana wake, na mtumwa huyo ataondoka peke yake.+  Lakini mtumwa huyo akisisitiza hivi: ‘Nampenda bwana wangu, mke wangu, na wanangu; sitaki kuachiliwa huru,’+  ni lazima bwana wake amlete mbele za Mungu wa kweli. Kisha bwana huyo atamleta kwenye mlango au kwenye mwimo wa mlango na kulitoboa sikio lake kwa sindano, naye atakuwa mtumwa wake maisha yake yote.  “Mtu akimuuza binti yake kuwa mtumwa, hataondoka kama mtumwa wa kiume anavyoondoka.  Ikiwa bwana wake hapendezwi naye na hataki awe suria wake, lakini aamue kumuuza kwa mtu mwingine,* bwana huyo hana haki ya kumuuza kwa wageni kwa sababu amemsaliti mtumwa huyo.  Akimchagua awe mke wa mwanawe, anapaswa kumpa haki anazostahili kama binti yake. 10  Ikiwa ataoa mke mwingine, hapaswi kumpunguzia mke huyo wa kwanza chakula, mavazi, na haki yake ya ndoa.+ 11  Ikiwa hatampa mambo hayo matatu, basi mtumwa huyo wa kike ataondoka bila kulipa pesa zozote. 12  “Yeyote anayempiga mtu na kumuua lazima auawe.+ 13  Lakini ikiwa alimuua bila kukusudia na Mungu wa kweli akaruhusu jambo hilo litokee, basi nitawaonyesha mahali anapoweza kukimbilia.+ 14  Mtu akimkasirikia vikali mwenzake na kumuua kwa kukusudia,+ mtu huyo lazima afe hata ikiwalazimu kumwondoa kwenye madhabahu yangu.+ 15  Mtu anayempiga baba yake au mama yake lazima auawe.+ 16  “Yeyote anayemteka nyara mtu mwingine+ na kumuuza au akipatikana amemzuilia,+ lazima auawe.+ 17  “Yeyote anayemlaani baba yake au mama yake lazima auawe.+ 18  “Hivi ndivyo mtakavyofanya wanaume wakigombana na mmoja wao ampige mwenzake kwa jiwe au ngumi* lakini asimuue bali amjeruhi hivi kwamba ashindwe kutoka kitandani: 19  Ikiwa anaweza kutoka kitandani na kutembea nje kwa kutumia fimbo, basi yule aliyempiga hataadhibiwa. Atamlipa tu fidia kwa ajili ya wakati aliopoteza alipokuwa kitandani mpaka atakapopona kabisa. 20  “Mtu akimpiga kwa fimbo mtumwa wake wa kiume au wa kike naye afie mikononi mwake, ni lazima mtumwa huyo alipiziwe kisasi.+ 21  Hata hivyo, mtumwa huyo akiendelea kuishi kwa siku moja au siku mbili, hatalipiziwa kisasi, kwa sababu alinunuliwa kwa pesa za bwana wake. 22  “Wanaume wakipambana na kumuumiza mwanamke mwenye mimba naye azae kabla ya wakati*+ lakini kifo kisitokee,* yule aliyemuumiza atalipa hasara atakayodaiwa na mume wa mwanamke huyo; naye atalipa kupitia waamuzi.+ 23  Lakini kifo kikitokea, basi ni lazima mlipe uhai kwa uhai,*+ 24  jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu,+ 25  alama ya moto kwa alama ya moto, jeraha kwa jeraha, pigo kwa pigo. 26  “Mtu akilipiga jicho la mtumwa wake wa kiume au jicho la mtumwa wake wa kike na kuliharibu, atamwachilia huru mtumwa huyo ili kufidia jicho lake.+ 27  Naye akimpiga na kumng’oa jino mtumwa wake wa kiume au wa kike, atamwachilia huru mtumwa huyo ili kufidia jino lake. 28  “Ng’ombe dume akimpiga pembe mwanamume au mwanamke na kumuua, ng’ombe dume huyo atauawa kwa kupigwa mawe+ na nyama yake haipaswi kuliwa; lakini mwenye ng’ombe dume huyo hataadhibiwa. 29  Lakini ikiwa ng’ombe dume alizoea kuwapiga watu pembe na mwenyewe akaonywa lakini hakumfunga, naye amuue mwanamume au mwanamke, ng’ombe dume huyo anapaswa kupigwa mawe na mwenye ng’ombe dume huyo anapaswa kuuawa pia. 30  Ikiwa atadaiwa fidia,* atalipa chochote atakachodaiwa ili kukomboa uhai wake.* 31  Ng’ombe dume huyo akimpiga pembe mtoto wa kiume au wa kike, mwenye ng’ombe dume huyo atatendewa kulingana na sheria hii. 32  Ng’ombe dume huyo akimpiga pembe mtumwa wa kiume au wa kike, mwenye ng’ombe dume huyo atamlipa bwana wa mtumwa huyo shekeli 30,* na ng’ombe dume huyo atauawa kwa kupigwa mawe. 33  “Mtu akiacha shimo wazi au akichimba shimo na kukosa kulifunika, na ng’ombe dume au punda aanguke humo, 34  mwenye shimo hilo atalipa fidia.+ Atamlipa mwenye mnyama huyo, na mnyama aliyekufa atakuwa wake. 35  Ng’ombe dume akimuumiza na kumuua ng’ombe dume wa mtu mwingine, basi watamuuza ng’ombe dume aliye hai na kugawana pesa hizo; wanapaswa pia kugawana ng’ombe aliyekufa. 36  Au ikiwa ilijulikana kwamba ng’ombe dume alizoea kupiga kwa pembe lakini mwenye ng’ombe dume huyo hakumfunga, lazima alipe ng’ombe dume kwa ng’ombe dume, kisha ng’ombe dume aliyekufa atakuwa wake.

Maelezo ya Chini

Tnn., “Haya ndiyo maamuzi ya hukumu utakayowapa.”
Tnn., “akombolewe.”
Au labda, “kwa kifaa.”
Tnn., “na watoto wake watoke tumboni.”
Au “na kusiwepo na majeraha mabaya.”
Au “nafsi kwa nafsi.”
Au “ridhaa.”
Au “nafsi yake.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.