Kutoka 25:1-40

  • Michango kwa ajili ya hema la ibada (1-9)

  • Sanduku la Agano (10-22)

  • Meza (23-30)

  • Kinara cha taa (31-40)

25  Kisha Yehova akamwambia Musa:  “Waambie Waisraeli wanitolee mchango; mnapaswa kuchukua mchango wangu kutoka kwa kila mtu ambaye moyo wake unamchochea kuchanga.+  Huu ndio mchango utakaopokea kutoka kwao: dhahabu,+ fedha,+ shaba,+  nyuzi za bluu, sufu ya zambarau,* kitambaa cha rangi nyekundu,* kitani bora, manyoya ya mbuzi,  ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za sili,* mbao za mshita,+  mafuta kwa ajili ya taa,+ mafuta ya zeri ya kutengenezea mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kwa ajili ya uvumba uliotiwa manukato,+  na mawe ya shohamu na mawe mengine ya kupambia efodi+ na kifuko cha kifuani.+  Mtanijengea mahali patakatifu, nami nitakaa* miongoni mwenu.+  Mtatengeneza mahali hapo patakatifu, yaani, hema la ibada pamoja na vyombo vyake vyote, mkifuata kikamili kielelezo nitakachowaonyesha.*+ 10  “Mtanitengenezea sanduku la mbao za mshita lenye urefu wa mikono miwili na nusu* na upana wa mkono mmoja na nusu na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 11  Kisha utalifunika kwa dhahabu safi.+ Utalifunika ndani na nje na kutengeneza ukingo wa dhahabu kulizunguka.+ 12  Nawe utatengeneza pete nne za dhahabu na kuzifunga sehemu ya juu ya miguu yake minne, pete mbili upande mmoja na pete mbili upande wa pili. 13  Nawe utatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu.+ 14  Utazitia fito hizo katika zile pete zilizo kwenye pande mbili za Sanduku ili zitumiwe kulibeba. 15  Fito hizo zitakaa kwenye pete za Sanduku; hazipaswi kuondolewa.+ 16  Nawe utaweka ndani ya sanduku hilo mabamba ya ushahidi nitakayokupa.+ 17  “Utatengeneza kifuniko cha dhahabu safi chenye urefu wa mikono miwili na nusu na upana wa mkono mmoja na nusu.+ 18  Nawe utatengeneza makerubi wawili wa dhahabu; utawatengeneza kwa nyundo kwenye miisho miwili ya kifuniko hicho.+ 19  Tengeneza kerubi mmoja kwenye mwisho mmoja na kerubi mwingine kwenye mwisho wa pili wa kifuniko. 20  Makerubi hao watakuwa wamenyoosha mabawa yao mawili kuelekea juu, na hivyo kukifunika kifuniko hicho kwa mabawa yao,+ nao wataelekeana. Nyuso za makerubi hao zitatazama kifuniko. 21  Utakiweka kifuniko+ hicho juu ya Sanduku, na ndani ya Sanduku utaweka mabamba ya ushahidi nitakayokupa. 22  Nitakutokea hapo na kuzungumza nawe kutoka juu ya kifuniko hicho.+ Kutoka katikati ya hao makerubi wawili walio juu ya sanduku la Ushahidi, nitakujulisha amri zote utakazowapa Waisraeli. 23  “Pia utatengeneza meza+ ya mbao za mshita yenye urefu wa mikono miwili na upana wa mkono mmoja na kimo cha mkono mmoja na nusu.+ 24  Utaifunika kwa dhahabu safi na kutengeneza ukingo wa dhahabu kuizunguka. 25  Utatengeneza utepe wenye upana wa kiganja kimoja* kuizunguka na ukingo wa dhahabu kuzunguka utepe huo. 26  Utaitengenezea pete nne za dhahabu na kuzitia kwenye pembe nne za miguu yake minne, sehemu ambazo miguu hiyo minne inaungana na meza. 27  Pete hizo zitakuwa karibu na utepe ili zitiwe fito za kubebea meza hiyo. 28  Utatengeneza fito za mshita na kuzifunika kwa dhahabu, nanyi mtazitumia kubebea meza hiyo. 29  “Pia utatengeneza sahani, vikombe, magudulia, na mabakuli ya meza hiyo, vitu ambavyo watatumia kumimina matoleo ya vinywaji. Utatengeneza vyombo hivyo kwa dhahabu safi.+ 30  Nawe utaweka mikate ya wonyesho juu ya meza hiyo ili iwe mbele zangu daima.+ 31  “Utatengeneza kinara cha taa+ cha dhahabu safi. Kinara hicho cha taa kitatengenezwa kwa nyundo. Sehemu yake ya chini, shina lake, matawi yake, vikombe vyake, matumba yake, na maua yake yatatengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu.+ 32  Kinara hicho kitakuwa na matawi sita, matawi matatu upande mmoja na matawi matatu upande wa pili. 33  Kila tawi litakuwa na vikombe vitatu vyenye umbo la maua ya mlozi; kila kikombe kitakuwa na ua na tumba lake. Hivyo ndivyo matawi hayo sita yatakavyotengenezwa kwenye shina la kinara hicho cha taa. 34  Kwenye shina la kinara hicho utatengeneza vikombe vinne vyenye umbo la maua ya mlozi, kila kikombe kitakuwa na ua na tumba lake. 35  Kutakuwa na tumba chini ya jozi ya kwanza ya matawi hayo sita, tumba chini ya jozi ya pili, na tumba chini ya jozi ya tatu. 36  Matumba na matawi yake na kinara chote cha taa kitatengenezwa kwa kipande kimoja cha dhahabu safi, kwa kutumia nyundo.+ 37  Utatengeneza taa saba kwa ajili ya kinara hicho, na taa hizo zinapowashwa zitaangaza mbele ya kinara hicho.+ 38  Koleo zake na vyetezo vyake vitatengenezwa kwa dhahabu safi.+ 39  Kinara hicho, pamoja na vifaa hivyo vinapaswa kutengenezwa kwa talanta moja* ya dhahabu safi. 40  Hakikisha kwamba unatengeneza vitu hivyo kwa kufuata kielelezo* ulichoonyeshwa mlimani.+

Maelezo ya Chini

Au “sufu iliyotiwa rangi ya zambarau.”
Rangi hiyo ilitoka kwa mdudu anayeitwa kochinili.
Mnyama wa baharini.
Au “nitapiga hema.”
Au “mchoro nitakaowaonyesha.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “mchoro ulioonyeshwa.”