Kutoka 28:1-43

  • Mavazi ya kuhani (1-5)

  • Efodi (6-14)

  • Kifuko cha kifuani (15-30)

    • Urimu na Thumimu (30)

  • Joho lisilo na mikono (31-35)

  • Kilemba chenye bamba la dhahabu (36-39)

  • Mavazi mengine ya kuhani (40-43)

28  “Utamleta Haruni+ ndugu yako pamoja na wanawe,+ Nadabu na Abihu,+ Eleazari na Ithamari+ kutoka miongoni mwa Waisraeli ili wanitumikie+ wakiwa makuhani.  Utamtengenezea Haruni ndugu yako mavazi matakatifu ili awe na utukufu na fahari.+  Waambie mafundi wote wenye ustadi,* ambao nimewajaza roho ya hekima,+ wamtengenezee Haruni mavazi ili kumtakasa, ili anitumikie akiwa kuhani.  “Haya ndiyo mavazi watakayotengeneza: kifuko cha kifuani,+ efodi,+ joho lisilo na mikono,+ kanzu yenye miraba, kilemba,+ na ukumbuu;+ watamtengenezea Haruni na wanawe mavazi haya matakatifu ili wanitumikie wakiwa makuhani.  Mafundi hao stadi watatumia dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora.  “Watatengeneza efodi kwa dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya rangi ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa, nacho kinapaswa kutariziwa.+  Efodi itakuwa na vipande viwili vitakavyounganishwa kwenye miisho miwili mabegani.  Mshipi uliofumwa+ unaoshikilia kwa nguvu efodi unapaswa kutengenezwa kwa vitu hivyohivyo, yaani, dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya rangi ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa.  “Utachukua mawe mawili ya shohamu+ na kuchonga juu yake majina ya wana wa Israeli,+ 10  majina sita juu ya jiwe moja na majina mengine sita juu ya jiwe lingine, kulingana na umri wao. 11  Mchonga mawe atachonga majina ya wana wa Israeli kwenye mawe hayo mawili kama mtu anavyochonga muhuri.+ Kisha mawe hayo yatatiwa katika vifuko vya dhahabu. 12  Utayaweka mawe hayo mawili kwenye vipande vya mabegani vya efodi, nayo yatakuwa mawe ya ukumbusho kwa wana wa Israeli,+ naye Haruni atayabeba majina yao kwenye vipande viwili vya efodi mabegani mwake kama ukumbusho mbele za Yehova. 13  Utatengeneza vifuko vya dhahabu 14  na minyororo miwili ya dhahabu safi iliyosokotwa kama kamba,+ utaifunga minyororo hiyo kwenye vifuko hivyo.+ 15  “Utamwagiza fundi wa kutarizi atengeneze kifuko cha kifuani cha maamuzi.+ Atakitengeneza kama efodi, kwa kutumia dhahabu, nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa.+ 16  Kifuko hicho kinapaswa kuwa cha mraba kinapokunjwa mara mbili, urefu wake uwe shubiri moja* na upana wake shubiri moja. 17  Unapaswa kuweka kwenye kifuko hicho mawe yaliyopangwa katika safu nne. Safu ya kwanza itakuwa na zabarijadi, topazi, na zumaridi. 18  Safu ya pili itakuwa na feruzi, yakuti, na yaspi. 19  Safu ya tatu itakuwa na jiwe la leshemi,* akiki, na amethisti. 20  Safu ya nne itakuwa na krisolito, shohamu, na yashefi. Mawe hayo yatawekwa kwenye vifuko vya dhahabu. 21  Mawe hayo yatalingana na majina 12 ya wana wa Israeli. Kila jina linapaswa kuchongwa kama muhuri unavyochongwa, na kila jina litawakilisha mojawapo ya makabila 12 ya wana wa Israeli. 22  “Utakitengenezea kifuko cha kifuani minyororo iliyosokotwa, kama kamba za dhahabu safi.+ 23  Pia utakitengenezea pete mbili za dhahabu na kuzitia kwenye pembe mbili za juu za kifuko hicho. 24  Utatia zile kamba mbili za dhahabu katika pete mbili zilizo kwenye pembe za kifuko cha kifuani. 25  Kisha utatia ncha mbili za zile kamba mbili katika vile vifuko viwili vya mabegani, nawe unapaswa kuzifunga ncha hizo kwenye vipande viwili vya efodi, sehemu ya mbele. 26  Utatengeneza pete mbili za dhahabu na kuziweka kwenye pembe mbili za chini, upande wa ndani wa kifuko cha kifuani, upande wa efodi.+ 27  Utatengeneza pete nyingine mbili za dhahabu upande wa mbele wa efodi, chini ya vipande viwili vya mabegani vya efodi, karibu na mahali inapoungana, juu ya mshipi uliofumwa wa efodi.+ 28  Pete za kifuko cha kifuani zitafungwa pamoja na pete za efodi kwa kamba ya bluu. Hivyo, kifuko cha kifuani kitabaki mahali pake kwenye efodi, juu ya mshipi uliofumwa. 29  “Haruni atayabeba majina ya wana wa Israeli juu ya moyo wake kwenye kile kifuko cha kifuani cha maamuzi anapoingia Patakatifu kama ukumbusho wa daima mbele za Yehova. 30  Utaweka Urimu na Thumimu*+ ndani ya kifuko cha kifuani cha maamuzi, nazo zitakuwa juu ya moyo wa Haruni anapoingia mbele za Yehova, naye Haruni atabeba daima juu ya moyo wake vitu hivyo vya kufanyia maamuzi kwa ajili ya Waisraeli mbele za Yehova. 31  “Utatengeneza joho lisilo na mikono la efodi kwa nyuzi za bluu peke yake.+ 32  Litakuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati upande wa juu. Sehemu hiyo itakuwa na ukingo uliofumwa kuizunguka. Itakuwa na ukingo kama wa koti la vita ili isiraruke. 33  Kwenye upindo wake wote, utatengeneza makomamanga ya nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kutia kengele za dhahabu katikati ya makomamanga. 34  Utatia kengele ya dhahabu kisha komamanga, kengele ya dhahabu kisha komamanga, kwenye upindo wote wa joho hilo lisilo na mikono. 35  Ni lazima Haruni alivae anapohudumu, na sauti ya kengele hizo inapaswa kusikika anapoingia patakatifu mbele za Yehova na anapotoka nje, ili asife.+ 36  “Utatengeneza bamba linalong’aa la dhahabu safi na kuchonga maneno haya juu yake kama muhuri unavyochongwa: ‘Utakatifu ni wa Yehova.’+ 37  Ni lazima ulifunge bamba hilo kwenye kilemba+ kwa kamba ya bluu; litakuwa daima upande wa mbele wa kilemba. 38  Nalo litakuwa kwenye paji la uso wa Haruni, naye Haruni atawajibika Mwisraeli anapotenda kosa dhidi ya vitu vitakatifu+ vinavyotakaswa na Waisraeli wakati wanapovitoa kuwa zawadi takatifu. Ni lazima bamba hilo likae sikuzote kwenye paji la uso wake, ili wapate kibali mbele za Yehova. 39  “Utafuma kanzu ya kitani bora yenye miraba, utatengeneza kilemba cha kitani bora, na kufuma ukumbuu.+ 40  “Pia utawatengenezea wana wa Haruni kanzu,+ ukumbuu, na kofia, ili wawe na utukufu na fahari.+ 41  Utamvisha Haruni ndugu yako na wanawe mavazi hayo, nawe utawatia mafuta+ na kuwaweka rasmi*+ na kuwatakasa, nao watanitumikia wakiwa makuhani. 42  Pia watengenezee suruali fupi* za kitani ili kufunika uchi wao.+ Suruali hizo zitawafunika kuanzia kiunoni mpaka mapajani. 43  Haruni na wanawe watazivaa wanapoingia kwenye hema la mkutano au wanapokaribia madhabahu kuhudumu mahali patakatifu, ili wasipatwe na hatia na kufa. Ni sheria ya kudumu kwa Haruni na uzao wake.*

Maelezo ya Chini

Au “wenye hekima moyoni.”
Yaani, upana wa kiganja cha mkono kuanzia kidole gumba hadi kidole kidogo, karibu sentimita 22.2 (inchi 8.75). Angalia Nyongeza B14.
Jiwe la thamani ambalo jina lake halijatajwa, huenda ni jiwe la kaharabu, hayasinthi, opali, au tumalini.
Angalia Kamusi.
Tnn., “na kuijaza mikono yao.”
Au “nguo za ndani.”
Tnn., “mbegu yake.”