Kutoka 29:1-46

  • Makuhani wawekwa rasmi (1-37)

  • Matoleo ya kila siku (38-46)

29  “Hivi ndivyo utakavyowatakasa ili wanitumikie wakiwa makuhani: Chukua ng’ombe dume mchanga, kondoo dume wawili wasio na kasoro,+  mikate isiyo na chachu, mikate ya mviringo isiyo na chachu na iliyokandwa kwa mafuta, na mikate myembamba isiyo na chachu na ambayo imepakwa mafuta.+ Utaioka kwa unga laini wa ngano  na kuiweka ndani ya kikapu, nawe utaileta mbele zangu ikiwa ndani ya kikapu,+ pamoja na yule ng’ombe dume na wale kondoo dume wawili.  “Utamleta Haruni na wanawe kwenye mlango wa hema la mkutano+ na kuwaosha kwa maji.+  Kisha utachukua yale mavazi+ na kumvisha Haruni kanzu, joho la efodi lisilo na mikono, efodi, na kifuko cha kifuani, nawe utamfunga vizuri kabisa kiunoni ule mshipi uliofumwa wa efodi.+  Utamvisha kile kilemba kichwani na kuiweka ile ishara takatifu ya wakfu* kwenye kilemba hicho;+  kisha chukua mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na uyamimine juu ya kichwa chake na kumtia mafuta.+  “Halafu walete wanawe na kuwavisha kanzu+  na umfunge Haruni na wanawe ukumbuu viunoni na kuwavisha kofia zao; ukuhani utakuwa wao, nayo itakuwa sheria ya kudumu.+ Hivyo ndivyo utakavyowaweka rasmi Haruni na wanawe ili watumike wakiwa makuhani.*+ 10  “Sasa utamleta yule ng’ombe dume mbele ya hema la mkutano, na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo ng’ombe dume.+ 11  Mchinje huyo ng’ombe dume mbele za Yehova, kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 12  Chukua kiasi fulani cha damu ya huyo ng’ombe dume kwa kidole chako na kuitia kwenye pembe za madhabahu,+ kisha umwage damu yote inayobaki chini kwenye msingi wa madhabahu.+ 13  Kisha chukua mafuta yote+ yanayofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, na figo zake mbili na mafuta yaliyo juu yake, nawe uchome moto vitu hivyo ili vifuke moshi juu ya madhabahu.+ 14  Lakini nyama ya ng’ombe dume huyo na ngozi yake na mavi yake utaviteketeza nje ya kambi. Hiyo ni dhabihu ya dhambi. 15  “Kisha utamchukua kondoo dume mmoja, naye Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo kondoo dume.+ 16  Mchinje kondoo dume huyo, uchukue damu yake na kuinyunyiza pande zote za madhabahu.+ 17  Mkate kondoo dume huyo vipandevipande, uoshe matumbo yake+ na miguu yake, na kuvipanga vipande hivyo pamoja na kichwa chake. 18  Utamchoma moto huyo kondoo mzima ili afuke moshi juu ya madhabahu. Ni dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova, harufu inayompendeza.*+ Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 19  “Kisha utamchukua kondoo dume wa pili, na Haruni na wanawe wataweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.+ 20  Mchinje kondoo dume huyo na uchukue kiasi fulani cha damu yake na kuipaka kwenye ncha ya sikio la kulia la Haruni na kwenye ncha za masikio ya kulia ya wanawe na kwenye vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia, nawe unyunyize damu pande zote za madhabahu. 21  Kisha chukua kiasi fulani cha damu iliyo kwenye madhabahu na baadhi ya mafuta yanayotumiwa kutia mafuta,+ nawe umnyunyizie Haruni na mavazi yake na wanawe na mavazi yao, ili awe mtakatifu yeye na mavazi yake na wanawe na mavazi yao.+ 22  “Halafu chukua mafuta ya huyo kondoo dume, mkia wake mnono, mafuta yanayofunika matumbo, mafuta yaliyo juu ya ini, figo zake mbili na mafuta yaliyo juu yake,+ na mguu wa kulia, kwa maana huyo ni kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani.+ 23  Chukua pia mkate wa mviringo na mkate wa mviringo uliokandwa kwa mafuta na mkate mwembamba kutoka katika kile kikapu cha mikate isiyo na chachu kilicho mbele za Yehova. 24  Ni lazima uviweke vitu hivyo vyote mikononi mwa Haruni na mikononi mwa wanawe, nawe utavitikisa kwenda mbele na nyuma vikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova. 25  Kisha utavichukua vitu hivyo kutoka mikononi mwao na kuviteketeza juu ya madhabahu, juu ya dhabihu ya kuteketezwa, ili viwe harufu inayompendeza* Yehova. Ni dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 26  “Halafu chukua kidari cha kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani,+ anayetolewa kwa ajili ya Haruni, nawe ukitikise kwenda mbele na nyuma kikiwa toleo la kutikiswa mbele za Yehova, nacho kitakuwa fungu lako. 27  Utakitakasa kidari cha toleo la kutikiswa na ule mguu wa fungu takatifu ambao ulitikiswa na ambao ulichukuliwa kutoka kwa yule kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani,+ aliyetolewa kwa ajili ya Haruni na wanawe. 28  Vitu hivyo vitakuwa vya Haruni na wanawe kulingana na sheria ya kudumu itakayotekelezwa na Waisraeli, kwa sababu vitu hivyo ni fungu takatifu, navyo vitakuwa fungu takatifu litakalotolewa na Waisraeli.+ Ni fungu lao takatifu kwa Yehova kutoka katika dhabihu zao za ushirika.+ 29  “Mavazi matakatifu+ ya Haruni yatatumiwa na wanawe+ baada yake watakapotiwa mafuta na kuwekwa rasmi kuwa makuhani. 30  Mwana wa Haruni atakayewekwa kuwa kuhani baada yake na ambaye ataingia katika hema la mkutano ili kuhudumu mahali patakatifu atayavaa mavazi hayo kwa siku saba.+ 31  “Utamchukua yule kondoo dume wa kumweka rasmi kuhani na kuichemshia nyama yake mahali patakatifu.+ 32  Haruni na wanawe wataila+ nyama ya kondoo dume huyo na mikate iliyo katika kikapu kwenye mlango wa hema la mkutano. 33  Watakula vitu vilivyotolewa dhabihu ili kufunika dhambi wakati walipowekwa rasmi kuwa makuhani* na kutakaswa. Lakini mtu ambaye hana idhini* hapaswi kuvila, kwa maana ni vitakatifu.+ 34  Ikiwa nyama yoyote ya dhabihu ya kumweka rasmi kuhani na mkate wowote utabaki mpaka asubuhi, unapaswa kuteketeza kinachobaki.+ Hakipaswi kuliwa kwa sababu ni kitakatifu. 35  “Hivi ndivyo utakavyomfanyia Haruni na wanawe, kulingana na yote niliyokuamuru. Utatumia siku saba kuwaweka rasmi kuwa makuhani.*+ 36  Kila siku utamtoa ng’ombe dume wa dhabihu ya dhambi ili kufunika dhambi zao, nawe utaitakasa madhabahu kwa kutoa dhabihu ya kufunika dhambi ya madhabahu hiyo, nawe utaitia mafuta ili kuitakasa.+ 37  Utatumia siku saba kufunika dhambi ya madhabahu, nawe lazima uitakase ili iwe madhabahu takatifu kabisa.+ Mtu yeyote anayeigusa madhabahu hiyo anapaswa kuwa mtakatifu. 38  “Hivi ndivyo vitu utakavyotoa kwenye madhabahu: kila siku, kwa kuendelea,+ utatoa wanakondoo dume wawili wenye umri wa mwaka mmoja. 39  Mtoe mwanakondoo dume mmoja asubuhi na yule mwingine jioni kabla ya giza kuingia.*+ 40  Sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini uliochanganywa na robo ya hini* ya mafuta ya zeituni zilizopondwa, na toleo la kinywaji la robo ya hini ya divai, vitatolewa pamoja na mwanakondoo dume wa kwanza. 41  Utamtoa mwanakondoo dume wa pili jioni kabla ya giza kuingia,* pamoja na matoleo ya nafaka na kinywaji kama yale ya asubuhi. Utamtoa akiwa harufu inayopendeza,* dhabihu kwa Yehova inayochomwa kwa moto. 42  Itakuwa dhabihu ya kuteketezwa itakayotolewa kwa ukawaida katika vizazi vyenu vyote kwenye mlango wa hema la mkutano mbele za Yehova, mahali ambapo nitawatokea ili kuzungumza nanyi.+ 43  “Hapo ndipo nitakapowatokea Waisraeli, na utukufu wangu utapatakasa mahali hapo.+ 44  Nitalitakasa hema la mkutano na madhabahu, nami nitamtakasa Haruni na wanawe+ ili wanitumikie wakiwa makuhani. 45  Nitakaa* miongoni mwa Waisraeli, nami nitakuwa Mungu wao.+ 46  Nao hakika watajua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao, niliyewatoa katika nchi ya Misri ili nikae miongoni mwao.+ Mimi ni Yehova Mungu wao.

Maelezo ya Chini

Au “lile taji takatifu.”
Tnn., “Hivyo ndivyo utakavyoujaza mkono wa Haruni na mikono ya wanawe.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “ili kuijaza mikono yao.”
Tnn., “mgeni,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Tnn., “kuijaza mikono yao.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Au “inayotuliza.”
Au “Nitapiga hema.”