Kutoka 33:1-23

  • Mungu awakaripia Waisraeli (1-6)

  • Hema la mkutano nje ya kambi (7-11)

  • Musa aomba kuona utukufu wa Yehova (12-23)

33  Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Ondoka mahali hapa pamoja na watu uliowaongoza kutoka katika nchi ya Misri. Safirini mpaka nchi niliyomwapia Abrahamu, Isaka, na Yakobo, niliposema, ‘Nitaupa uzao wenu* nchi hii.’+  Nitamtuma malaika awatangulie+ na kuwafukuza Wakanaani, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.+  Pandeni mpaka kwenye nchi inayotiririka maziwa na asali.+ Lakini sitaenda pamoja nanyi, kwa sababu ninyi ni watu wakaidi, *+ na huenda nikawaangamiza kabisa njiani.”+  Watu waliposikia maneno hayo makali, wakaanza kuomboleza, na hakuna yeyote kati yao aliyevaa mapambo yake.  Yehova akamwambia Musa: “Waambie Waisraeli, ‘Ninyi ni watu wakaidi.*+ Ninaweza kupita mara moja katikati yenu na kuwaangamiza kabisa.+ Sasa basi, msivae mapambo yenu ninapofikiria nitakavyowatendea.’”  Kwa hiyo kuanzia Mlima Horebu na kuendelea, Waisraeli hawakuvaa* mapambo yao.  Sasa Musa akachukua hema lake na kulipiga nje ya kambi, mbali kidogo na kambi, naye akaliita hema la mkutano. Mtu yeyote aliyetafuta ushauri wa Yehova+ alikuwa akienda kwenye hema la mkutano, lililokuwa nje ya kambi.  Kila mara Musa alipokuwa akienda kwenye hema hilo, watu wote walitoka na kusimama kwenye milango ya mahema yao, nao walimtazama Musa mpaka alipoingia ndani ya hema hilo.  Kila mara Musa alipoingia katika hema hilo, ile nguzo ya wingu+ ilishuka chini na kusimama kwenye mlango wa hema hilo Mungu alipokuwa akiongea na Musa.+ 10  Watu wote walipoona nguzo hiyo ya wingu ikisimama kwenye mlango wa hema, kila mmoja wao alisimama na kuinama chini kwenye mlango wa hema lake. 11  Yehova aliongea na Musa uso kwa uso,+ kama mwanadamu anavyoongea na mwanadamu mwenzake. Musa aliporudi kambini, Yoshua+ mwana wa Nuni, aliyekuwa mhudumu na mtumishi wake,+ hakuondoka hemani. 12  Sasa Musa akamwambia Yehova: “Angalia, unaniambia, ‘Waongoze watu hawa,’ lakini hujaniambia ni nani utakayemtuma pamoja nami. Isitoshe umeniambia, ‘Ninakujua kwa jina* na umepata kibali machoni pangu.’ 13  Tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nifundishe njia zako+ ili nikujue na kuendelea kuwa na kibali machoni pako. Pia, kumbuka kwamba taifa hili ni watu wako.”+ 14  Basi akasema: “Mimi mwenyewe nitakwenda* pamoja nawe,+ nami nitakupumzisha.”+ 15  Kisha Musa akamwambia: “Ikiwa wewe mwenyewe huendi* pamoja nasi, usituondoe mahali hapa. 16  Itajulikanaje kwamba mimi nimepata kibali machoni pako, mimi na watu wako? Je, haitajulikana ukienda pamoja nasi,+ ili mimi na watu wako tuonekane kuwa tofauti na watu wengine wote duniani?”+ 17  Yehova akaendelea kumwambia Musa: “Nitafanya pia jambo hilo unaloomba, kwa sababu umepata kibali machoni pangu nami nakujua wewe kwa jina.” 18  Ndipo Musa akasema: “Tafadhali nionyeshe utukufu wako.” 19  Lakini akamwambia: “Nitaufanya wema wangu wote upite mbele ya uso wako, nami nitatangaza jina langu Yehova mbele yako;+ nami nitamwonyesha kibali yule ninayetaka kumwonyesha kibali, nami nitamwonyesha rehema yule ninayetaka kumwonyesha rehema.”+ 20  Lakini akasema: “Huwezi kuuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na aendelee kuishi.” 21  Yehova akaendelea kusema: “Kuna mahali hapa karibu nami. Simama juu ya mwamba. 22  Utukufu wangu utakapokuwa ukipita, nitakuingiza kwenye shimo ndani ya mwamba, nami nitakukinga kwa mkono wangu mpaka nitakapopita. 23  Kisha nitauondoa mkono wangu, nawe utauona mgongo wangu. Lakini uso wangu hautaonekana.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Nitaipa mbegu yenu.”
Au “wenye shingo ngumu.”
Tnn., “wenye shingo ngumu.”
Tnn., “waliyavua kabisa.”
Au “Nimekuchagua.”
Tnn., “Uso wangu utaenda.”
Tnn., “Ikiwa uso wako hauendi.”