Kutoka 38:1-31

  • Madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa (1-7)

  • Beseni la shaba (8)

  • Ua (9-20)

  • Orodha ya vifaa vya hema la ibada (21-31)

38  Akatumia mbao za mshita kutengeneza madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa. Ilikuwa ya mraba, yenye urefu wa mikono mitano,* upana wa mikono mitano, na kimo cha mikono mitatu.+  Kisha akatengeneza pembe kwenye ncha zake nne. Pembe hizo zilikuwa sehemu ya hiyo madhabahu. Naye akaifunika kwa shaba.+  Baada ya hayo akatengeneza vyombo vyote vya madhabahu: ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mabakuli, nyuma,* na vyetezo. Alitengeneza vyombo hivyo vyote kwa shaba.  Pia, alitengeneza wavu wa shaba kwa ajili ya madhabahu, chini ya ukingo wake, katikati ya madhabahu.  Alitengeneza pete nne kwenye pembe nne za wavu huo karibu na wavu huo wa shaba, ili zishikilie fito.  Baada ya hayo akatengeneza fito kwa mbao za mshita na kuzifunika kwa shaba.  Kisha akazitia fito hizo kwenye zile pete zilizo kwenye pande za madhabahu ili zitumiwe kubebea madhabahu. Alitengeneza madhabahu hiyo kama sanduku la mbao lenye uwazi.  Kisha akatengeneza beseni la shaba+ na kinara chake cha shaba; alitumia vioo* vya wanawake waliotumikia kwenye mlango wa hema la mkutano kulingana na mpangilio uliowekwa.  Kisha akatengeneza ua.+ Upande wa kusini wa ua huo, alitengeneza mapazia yanayoning’inia ya kitani bora kilichosokotwa yenye urefu wa mikono 100.+ 10  Ulikuwa na nguzo 20 na vikalio 20 vya shaba, na kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 11  Pia, kulikuwa na mapazia yanayoning’inia upande wa kaskazini yenye urefu wa mikono 100. Nguzo zake 20 na vikalio vyake 20 vilikuwa vya shaba. Lakini kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 12  Hata hivyo, upande wa magharibi ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye urefu wa mikono 50. Pia ulikuwa na nguzo kumi na vikalio kumi, kulabu na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha. 13  Ua huo ulikuwa na upana wa mikono 50 upande wa mashariki, yaani, upande wa mapambazuko ya jua. 14  Upande mmoja ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15, pamoja na nguzo tatu na vikalio vitatu. 15  Upande wa pili wa mlango wa ua ulikuwa na mapazia yanayoning’inia yenye upana wa mikono 15, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. 16  Mapazia yote yanayoning’inia kuzunguka ua yalitengenezwa kwa kitani bora kilichosokotwa. 17  Vikalio vya nguzo vilikuwa vya shaba, kulabu za nguzo hizo na vitanzi* vyake vilikuwa vya fedha, sehemu za juu zilifunikwa kwa fedha, na nguzo zote za ua zilikuwa na kulabu za fedha.+ 18  Pazia la mlango wa ua lilifumwa kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora kilichosokotwa. Lilikuwa na urefu wa mikono 20 na kimo cha mikono 5, sawa na kimo cha mapazia ya ua yanayoning’inia.+ 19  Nguzo zake nne na vikalio vyake vinne vilikuwa vya shaba. Kulabu zake zilikuwa za fedha, na sehemu za juu za nguzo hizo pamoja na vitanzi* vilifunikwa kwa fedha. 20  Vigingi vyote vya hema la ibada na vya ua vilikuwa vya shaba.+ 21  Ifuatayo ni orodha ya vitu vilivyotumiwa kutengeneza hema la ibada, yaani, hema la Ushahidi.+ Orodha hii ilitayarishwa kwa amri ya Musa, na lilikuwa jukumu la Walawi+ kuitayarisha chini ya uongozi wa Ithamari+ mwana wa Haruni kuhani. 22  Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru wa kabila la Yuda alifanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa. 23  Alikuwa pamoja na Oholiabu+ mwana wa Ahisamaki wa kabila la Dani, aliyekuwa fundi, mtarizi, na mfumaji wa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa cha rangi nyekundu, na kitani bora. 24  Dhahabu yote iliyotumiwa kwa kazi zote za mahali patakatifu ndiyo dhahabu yote iliyotolewa kama toleo la kutikiswa,+ ilikuwa talanta 29* na shekeli 730* kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* 25  Fedha iliyotolewa na wale walioandikishwa ilikuwa talanta 100 na shekeli 1,775 kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* 26  Nusu shekeli iliyotolewa na kila mwanamume ilikuwa nusu shekeli kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu,* ilitolewa na kila mwanamume aliyeandikishwa mwenye umri wa kuanzia miaka 20 na zaidi,+ wote walikuwa 603,550.+ 27  Talanta 100 za fedha zilitumiwa kutengeneza vikalio vya mahali patakatifu na vikalio vya pazia; talanta 100 zilitumiwa kutengeneza vikalio 100, talanta moja kwa kila kikalio.+ 28  Alitumia zile shekeli 1,775 kutengeneza kulabu za nguzo na kufunika sehemu zake za juu na kuziunganisha pamoja. 29  Shaba iliyotolewa ikiwa toleo* ilikuwa talanta 70 na shekeli 2,400. 30  Alitumia shaba hiyo kutengeneza vikalio vya mlango wa hema la mkutano, madhabahu ya shaba na wavu wake wa shaba, vyombo vyote vya madhabahu, 31  vikalio vyote vya ua, vikalio vya mlango wa ua, vigingi vyote vya hema la ibada, na vigingi vyote+ vya ua.

Maelezo ya Chini

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Wingi wa kifaa kinachoitwa uma.
Yaani, vioo vya shaba vilivyong’arishwa sana.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Au “pete; vitanzi; vibanio” vya kushikia.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “shekeli takatifu.”
Au “shekeli takatifu.”
Au “shekeli takatifu.”
Au “toleo la kutikiswa.”