Kutoka 40:1-38

  • Ujenzi wa hema la ibada (1-33)

  • Utukufu wa Yehova wajaa katika hema la ibada (34-38)

40  Kisha Yehova akamwambia Musa:  “Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, utajenga hema la ibada, yaani, hema la mkutano.+  Weka sanduku la Ushahidi ndani yake,+ na ulifunike sanduku hilo kwa pazia.+  Ingiza meza+ na upange vyombo vyake juu yake, kisha ulete kinara cha taa+ na kuwasha taa zake.+  Halafu uweke madhabahu ya dhahabu ya kufukizia uvumba+ mbele ya sanduku la Ushahidi na kuweka pazia la mlango wa hema la ibada.+  “Utaweka madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ mbele ya mlango wa hema la ibada, yaani, hema la mkutano,  na kuweka beseni kati ya hema la mkutano na madhabahu, kisha utie maji ndani ya beseni hilo.+  Halafu utengeneze ua+ kuzunguka hema hilo na kuweka pazia+ kwenye mlango wa ua.  Kisha uchukue mafuta yanayotumiwa kutia mafuta+ na kulitia mafuta hema la ibada na vitu vyote vilivyomo,+ nawe ulitakase pamoja na vyombo vyake vyote, ili liwe takatifu. 10  Utatia mafuta madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa pamoja na vyombo vyake vyote na kuitakasa, ili iwe madhabahu takatifu zaidi.+ 11  Nawe ulitie mafuta beseni na kinara chake na kulitakasa. 12  “Kisha mlete Haruni na wanawe karibu na mlango wa hema la mkutano na kuwaosha kwa maji.+ 13  Utamvisha Haruni mavazi matakatifu+ na kumtia mafuta+ na kumtakasa, naye atanitumikia akiwa kuhani. 14  Baada ya hayo walete wanawe karibu na kuwavisha kanzu.+ 15  Utawatia mafuta kama ulivyomtia mafuta baba yao,+ ili wanitumikie wakiwa makuhani, nao wataendelea kuwa makuhani daima katika vizazi vyao vyote kwa sababu wametiwa mafuta.”+ 16  Musa alifanya yote ambayo Yehova alimwamuru.+ Hivyo ndivyo alivyofanya. 17  Katika mwezi wa kwanza, mwaka wa pili, siku ya kwanza ya mwezi, hema la ibada lilitengenezwa.+ 18  Musa alitengeneza hema la ibada kwa kuweka chini vikalio vyake,+ kuweka viunzi vyake,+ kuweka fito zake,+ na kusimamisha nguzo zake. 19  Akatandaza kitambaa cha hema+ juu ya viunzi vya hema hilo na kuweka kifuniko+ juu yake, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 20  Kisha akachukua yale mabamba ya Ushahidi+ na kuyaweka ndani ya sanduku la Ushahidi,+ akatia fito+ kwenye pete za Sanduku hilo na kuweka kifuniko+ juu ya Sanduku hilo.+ 21  Akaingiza sanduku la Ushahidi ndani ya hema la ibada na kuweka pazia+ ambalo lilifunika sanduku la Ushahidi,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 22  Kisha akaweka meza+ ndani ya hema la mkutano upande wa kaskazini, nje ya pazia, 23  naye akapanga juu yake ile mikate+ kwa safu mbele za Yehova, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 24  Akaweka kile kinara cha taa+ ndani ya hema la mkutano mbele ya meza hiyo, upande wa kusini. 25  Kisha akawasha zile taa+ mbele za Yehova, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 26  Halafu akaweka ile madhabahu ya dhahabu+ ndani ya hema la mkutano mbele ya pazia, 27  ili afukize juu yake uvumba+ uliotiwa manukato,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa. 28  Kisha akaweka pazia+ la mlango wa hema la ibada. 29  Akaweka madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ kwenye mlango wa hema la ibada, yaani, hema la mkutano, ili atoe juu yake dhabihu za kuteketezwa+ na matoleo ya nafaka, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 30  Kisha akaweka beseni kati ya hema la mkutano na madhabahu na kutia maji ndani yake ili makuhani wanawe+ mikono na miguu yao. 31  Musa na pia Haruni na wanawe walitumia maji ya beseni hilo kunawa mikono na miguu yao. 32  Kila mara walipoenda kwenye hema la mkutano au kukaribia madhabahu, walinawa+ mikono na miguu yao, kama Yehova alivyomwamuru Musa. 33  Mwishowe akatengeneza ua+ kuzunguka hema la ibada na ile madhabahu na kuweka pazia la mlango wa ua.+ Basi Musa akakamilisha kazi yote. 34  Ndipo wingu likaanza kufunika hema la mkutano, na utukufu wa Yehova ukajaa katika hema la ibada.+ 35  Musa alishindwa kuingia ndani ya hema la mkutano kwa sababu wingu liliendelea kulifunika, na utukufu wa Yehova ukajaa katika hema hilo.+ 36  Kila mara wingu lilipoinuka kutoka juu ya hema la ibada, Waisraeli walivunja kambi katika hatua zote za safari yao.+ 37  Hata hivyo, wingu lilipokosa kuinuka, hawakuvunja kambi mpaka siku lilipoinuka.+ 38  Katika hatua zote za safari yao, Waisraeli wote waliona wingu la Yehova likiwa juu ya hema la ibada wakati wa mchana, na moto ukiwa juu yake wakati wa usiku.+

Maelezo ya Chini