Kutoka 5:1-23

  • Musa na Haruni wakiwa mbele ya Farao (1-5)

  • Ukandamizaji wazidi (6-18)

  • Waisraeli wamlaumu Musa na Haruni (19-23)

5  Baadaye, Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kumwambia: “Hivi ndivyo anavyosema Yehova Mungu wa Israeli, ‘Waruhusu watu wangu waende ili wanifanyie sherehe nyikani.’”  Lakini Farao akasema: “Yehova ni nani,+ hivi kwamba nitii sauti yake na kuwaruhusu Waisraeli waende zao?+ Simjui Yehova kamwe, na isitoshe, sitawaruhusu Waisraeli waende zao.”+  Lakini wakamwambia: “Mungu wa Waebrania amewasiliana nasi. Tafadhali, tungependa kusafiri kwa siku tatu kwenda nyikani tukamtolee dhabihu Yehova Mungu wetu;+ tusipofanya hivyo, atatupiga kwa ugonjwa au kwa upanga.”  Mfalme wa Misri akawaambia: “Musa na Haruni, kwa nini mnawafanya watu waache kazi zao? Rudini mkafanye kazi yenu!”*+  Farao akaendelea kusema: “Angalieni jinsi watu walivyo wengi nchini, nanyi mnataka kuwafanya waache kazi yao.”  Siku hiyohiyo, Farao akawaamuru hivi wasimamizi wa kazi na wasimamizi wa watumwa:  “Msiwape tena watu hawa nyasi za kufyatua matofali.+ Waacheni wakajitafutie nyasi wenyewe.  Lakini bado mnapaswa kuwaamuru wafyatue idadi ileile ya matofali kama awali. Msiwapunguzie idadi, kwa sababu wanastarehe.* Ndiyo sababu wanalia, ‘Tunataka kwenda, tunataka kumtolea dhabihu Mungu wetu!’  Watumikisheni zaidi, wapeni kazi zaidi ili wasisikilize uwongo.” 10  Basi wasimamizi wa kazi+ na wasimamizi wa watumwa wakaenda na kuwaambia watu: “Hivi ndivyo Farao anavyosema, ‘Siwapi tena nyasi. 11  Nendeni mkajitafutie nyasi zenu wenyewe popote mtakapozipata, lakini kazi yenu haitapunguzwa hata kidogo.’” 12  Ndipo watu wakatawanyika kotekote katika nchi ya Misri ili kukusanya vishina vya mabua ili waweze kupata nyasi. 13  Na wasimamizi wa kazi waliendelea kusisitiza hivi: “Ni lazima kila mmoja wenu amalize kazi yake kila siku, kama mlivyokuwa mkifanya mlipokuwa mkiletewa nyasi.” 14  Pia, wasimamizi wa Waisraeli, ambao walikuwa wamechaguliwa na wasimamizi wa kazi waliowekwa na Farao kuwasimamia wasimamizi hao wa Waisraeli, walipigwa.+ Waliwauliza: “Kwa nini hamkufyatua idadi ileile ya matofali mliyokuwa mkifyatua mwanzoni? Hamkufanya hivyo jana na leo.” 15  Ndipo wasimamizi wa Waisraeli wakaenda kumlalamikia Farao, wakisema: “Kwa nini unatutendea hivi sisi watumishi wako? 16  Sisi watumishi wako hatupewi nyasi zozote, lakini wanatuambia, ‘Fyatueni matofali!’ Tunapigwa, lakini kosa ni la watu wako.” 17  Lakini Farao akawaambia: “Mnastarehe,* mnastarehe!*+ Ndiyo sababu mnasema, ‘Tunataka kwenda, tunataka kumtolea Yehova dhabihu.’+ 18  Basi sasa, rudini kazini! Hamtapewa nyasi zozote, lakini ni lazima mfyatue idadi ileile ya matofali.” 19  Kwa hiyo wasimamizi wa Waisraeli wakatambua kwamba wako katika shida kubwa kwa sababu ya amri hii: “Msipunguze hata kidogo idadi ya matofali mnayopaswa kufyatua kila siku.” 20  Walipotoka kwa Farao walikutana na Musa na Haruni, waliokuwa wamesimama wakiwangojea. 21  Mara moja wasimamizi hao wakawaambia: “Yehova na awatazame ninyi na kuwahukumu, kwa maana mmefanya Farao na watumishi wake watudharau* nanyi mmeweka upanga mkononi mwao ili watuue.”+ 22  Kisha Musa akamgeukia Yehova na kumuuliza: “Yehova, kwa nini umewatesa watu hawa? Kwa nini umenituma? 23  Tangu nilipofika mbele ya Farao kuzungumza katika jina lako,+ amewatesa vikali zaidi watu hawa,+ nawe hakika hujawaokoa watu wako.”+

Maelezo ya Chini

Au “mkabebe mizigo yenu.”
Au “ni wavivu.”
Au “Ninyi ni wavivu.”
Au “ninyi ni wavivu.”
Au “mmefanya tunuke uvundo mbele ya Farao na watumishi wake.”