Kutoka 7:1-25

  • Yehova amwimarisha Musa (1-7)

  • Fimbo ya Haruni yawa nyoka mkubwa (8-13)

  • Pigo la 1: maji yageuzwa kuwa damu (14-25)

7  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Tazama, nimekufanya kuwa kama Mungu* kwa Farao, na Haruni ndugu yako atakuwa nabii wako.+  Unapaswa kurudia kila jambo nitakalokuamuru, na Haruni ndugu yako atazungumza na Farao, naye Farao atawaruhusu Waisraeli watoke katika nchi yake.  Lakini mimi, nitauacha moyo wa Farao uwe mkaidi,+ nami nitazidisha ishara zangu na miujiza yangu katika nchi ya Misri.+  Lakini Farao hatawasikiliza ninyi, nami nitauweka mkono wangu juu ya Misri na kuyatoa makundi yangu makubwa,* watu wangu, Waisraeli, kutoka katika nchi ya Misri kwa hukumu kubwa.+  Na Wamisri watajua kwa hakika kwamba mimi ni Yehova+ nitakapounyoosha mkono wangu dhidi ya Misri na kuwatoa Waisraeli miongoni mwao.”  Musa na Haruni wakafanya mambo ambayo Yehova aliwaamuru; hivyo ndivyo walivyofanya.  Musa alikuwa na umri wa miaka 80 naye Haruni alikuwa na umri wa miaka 83 walipozungumza na Farao.+  Sasa Yehova akamwambia Musa na Haruni:  “Farao akiwaambia, ‘Fanyeni muujiza,’ mwambie Haruni, ‘Chukua fimbo yako uitupe chini mbele ya Farao.’ Itakuwa nyoka mkubwa.”+ 10  Basi Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kufanya kama tu Yehova alivyokuwa amewaamuru. Haruni akaitupa chini fimbo yake mbele ya Farao na watumishi wake, nayo ikawa nyoka mkubwa. 11  Hata hivyo, Farao akawaita watu wenye hekima na walozi, na makuhani wachawi wa Misri+ nao pia wakafanya muujiza huohuo kwa uchawi wao.*+ 12  Kila mmoja wao akatupa chini fimbo yake, nazo zikawa nyoka wakubwa; lakini fimbo ya Haruni ikazimeza fimbo zao. 13  Lakini moyo wa Farao uliendelea kuwa mkaidi,+ na kama Yehova alivyosema, Farao hakuwasikiliza. 14  Ndipo Yehova akamwambia Musa: “Moyo wa Farao ni mgumu.+ Amekataa kuwaruhusu watu wangu waende zao. 15  Nenda kwa Farao asubuhi. Tazama! Anaenda mtoni! Unapaswa kusimama kwenye ukingo wa Mto Nile; na ubebe mkononi ile fimbo iliyogeuka kuwa nyoka.+ 16  Nawe unapaswa kumwambia, ‘Yehova Mungu wa Waebrania amenituma kwako,+ naye anasema: “Waruhusu watu wangu waende ili wanitumikie nyikani,” lakini mpaka sasa hujatii. 17  Yehova anasema hivi: “Kwa jambo hili utajua kwamba mimi ni Yehova.+ Tazama ninayapiga maji ya Mto Nile kwa fimbo hii iliyo mkononi mwangu, nayo yatabadilika na kuwa damu. 18  Samaki walio katika Mto Nile watakufa, nao Mto Nile utanuka, na Wamisri watashindwa kunywa maji ya Mto Nile.”’” 19  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Ichukue fimbo yako na uunyooshe mkono wako juu ya maji yote ya Misri,+ juu ya mito yake, juu ya mifereji yake,* juu ya maeneo yake yenye umajimaji,+ na juu ya mabwawa yake yote, ili yawe damu.’ Kutakuwa na damu katika nchi yote ya Misri, hata katika vyombo vya mbao na vya mawe.” 20  Mara moja Musa na Haruni wakafanya kama Yehova alivyowaamuru. Akaiinua fimbo hiyo na kuyapiga maji ya Mto Nile mbele ya Farao na watumishi wake, na maji yote yaliyokuwa katika Mto Nile yakabadilika na kuwa damu.+ 21  Basi samaki waliokuwa mtoni wakafa,+ na mto ukaanza kunuka, na Wamisri hawakuweza kunywa maji ya Mto Nile,+ kulikuwa na damu katika nchi yote ya Misri. 22  Lakini makuhani wachawi wa Misri wakafanya jambo hilohilo kwa mazingaombwe yao,+ hivi kwamba moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyosema, Farao hakuwasikiliza.+ 23  Basi Farao akarudi nyumbani kwake, wala hakuzingatia jambo hilo moyoni mwake. 24  Kwa hiyo, Wamisri wote walikuwa wakichimba kandokando kuzunguka Mto Nile wakitafuta maji ya kunywa, kwa sababu hawangeweza kunywa maji yoyote ya Mto Nile. 25  Na siku saba kamili zikapita baada ya Yehova kuupiga Mto Nile.

Maelezo ya Chini

Tnn., “nimekufanya Mungu.”
Tnn., “majeshi yangu.”
Au “ufundi wao wa uchawi.”
Yaani, mifereji ya Mto Nile.