Kutoka 8:1-32

  • Pigo la 2: vyura (1-15)

  • Pigo la 3: mbu (16-19)

  • Pigo la 4: nzi (20-32)

    • Nchi ya Gosheni haikuathiriwa (22, 23)

8  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Nenda kwa Farao umwambie, ‘Yehova anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie.+  Ukiendelea kukataa kuwaruhusu waondoke, nitaleta pigo la vyura katika eneo lako lote.+  Nao Mto Nile utajaa vyura, nao watatoka humo na kuingia ndani ya nyumba yako, ndani ya chumba chako cha kulala, kitandani mwako, katika nyumba za watumishi wako na juu ya watu wako, ndani ya majiko yenu, na ndani ya vyombo vyenu vya* kukandia unga.+  Vyura watapanda juu yako, juu ya watu wako, na juu ya watumishi wako wote.”’”  Baadaye Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Unyooshe mkono wako ulio na fimbo juu ya mito, mifereji ya Nile, na maeneo yenye umajimaji, ili vyura waje juu ya nchi ya Misri.’”  Basi Haruni akaunyoosha mkono wake juu ya maji ya Misri, na vyura wakaanza kuja na kuifunika nchi ya Misri.  Hata hivyo, makuhani wachawi wakafanya jambo hilohilo kwa mazingaombwe yao, nao pia wakafanya vyura waje juu ya nchi ya Misri.+  Ndipo Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia: “Msihini Yehova aniondolee mimi na watu wangu vyura hawa,+ kwa maana ninataka kuwaruhusu watu waende zao wakamtolee Yehova dhabihu.”  Kisha Musa akamwambia Farao: “Kwa heshima yako niambie wakati unaotaka nimwombe Mungu awaondoe vyura kutoka kwako, kutoka kwa watumishi wako, kutoka kwa watu wako, na kutoka katika nyumba zenu. Watabaki katika Mto Nile tu.” 10  Farao akamwambia: “Kesho.” Basi Musa akasema: “Itakuwa kama unavyosema, ili ujue kwamba hakuna yeyote aliye kama Yehova Mungu wetu.+ 11  Vyura wataondoka kwako, katika nyumba zako, kutoka kwa watumishi wako, na kutoka kwa watu wako. Watabaki katika Mto Nile tu.”+ 12  Basi Musa na Haruni wakaondoka mbele ya Farao, naye Musa akamsihi Yehova amwondolee Farao vyura aliomletea.+ 13  Kisha Yehova akafanya kama Musa alivyomwomba, na vyura wakaanza kufia nyumbani, nyuani, na mashambani. 14  Watu wakakusanya marundo yasiyohesabika ya vyura, na nchi ikaanza kunuka. 15  Farao alipoona kwamba hali ni nafuu, akaufanya moyo wake kuwa mgumu,+ na kama Yehova alivyosema, Farao akakataa kuwasikiliza. 16  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Mwambie Haruni, ‘Inyooshe fimbo yako na uyapige mavumbi ya ardhi, nayo yatakuwa mbu* katika nchi yote ya Misri.’” 17  Nao wakafanya hivyo. Haruni akaunyoosha mkono wake uliokuwa na fimbo yake na kuyapiga mavumbi ya ardhi, na mbu wakawavamia wanadamu na wanyama. Mavumbi yote katika nchi yote ya Misri yakawa mbu.+ 18  Makuhani wachawi wakajaribu pia kugeuza mavumbi yawe mbu kwa mazingaombwe yao,+ lakini hawakuweza. Mbu hao wakawavamia wanadamu na wanyama. 19  Basi makuhani wachawi wakamwambia Farao: “Ni kidole cha Mungu!”+ Lakini moyo wa Farao ukaendelea kuwa mkaidi, na kama Yehova alivyosema, hakuwasikiliza. 20  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Amka asubuhi na mapema ukasimame mbele ya Farao. Tazama! Anaenda mtoni! Nawe unapaswa kumwambia, ‘Yehova anasema hivi: “Waruhusu watu wangu waende wakanitumikie. 21  Lakini usipowaruhusu watu wangu waende zao, nitakuletea nzi,* wewe, watumishi wako, na watu wako, nao wataingia katika nyumba zako; na nyumba za Misri zitajaa nzi hao, nao wataifunika hata ardhi ambayo Wamisri wamesimama juu yake. 22  Siku hiyo, hakika nitaitenga nchi ya Gosheni, wanakoishi watu wangu. Hakuna nzi yeyote atakayepatikana huko,+ na kwa jambo hilo utajua kwamba mimi, Yehova, niko humu nchini.+ 23  Nami nitatofautisha kati ya watu wangu na watu wako. Kesho ishara hii itatokea.”’” 24  Basi Yehova akafanya kama alivyosema, na makundi makubwa sana ya nzi yakaanza kuvamia nyumba ya Farao na nyumba za watumishi wake na nchi yote ya Misri.+ Nchi ikaharibiwa na nzi hao.+ 25  Hatimaye Farao akawaita Musa na Haruni na kuwaambia: “Nendeni, mkamtolee dhabihu Mungu wenu nchini.” 26  Lakini Musa akasema: “Si vema kufanya hivyo, kwa sababu dhabihu tutakazomtolea Yehova Mungu wetu zitawachukiza Wamisri.+ Tukitoa dhabihu zinazowachukiza Wamisri mbele ya macho yao, je, hawatatupiga mawe? 27  Tutasafiri kwa siku tatu nyikani, na huko tutamtolea Yehova Mungu wetu dhabihu kama alivyotuambia.”+ 28  Basi Farao akasema: “Nitawaruhusu mwende mkamtolee Yehova Mungu wenu dhabihu nyikani. Ila tu, msiende mbali sana. Msihini Mungu kwa niaba yangu.”+ 29  Musa akasema: “Sasa ninaenda zangu, nami nitamsihi Yehova, na kesho nzi wataondoka kwako Farao, kwa watumishi wako, na kwa watu wako. Lakini wewe, Ee Farao, unapaswa kuacha kutuchezea* kwa kukataa kuturuhusu kwenda kumtolea Yehova dhabihu.”+ 30  Kisha Musa akaondoka mbele ya Farao na kumsihi Yehova.+ 31  Basi Yehova akafanya kama Musa alivyomsihi, na nzi wakaondoka kwa Farao, kwa watumishi wake, na kwa watu wake. Hakubaki hata nzi mmoja. 32  Hata hivyo, kwa mara nyingine tena Farao akaufanya moyo wake kuwa mgumu naye hakuwaruhusu Waisraeli waende zao.

Maelezo ya Chini

Au “mabakuli yenu ya.”
Aina ya mbu anayeitwa hak·kin·nam’ katika Kiebrania.
Aina ya nzi anayeuma.
Au “kutuhadaa.”